Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, October 28, 2015

IDD AZZAN APIGWA CHINI KINONDONI, CUF YACHUKUA



Wimbi la vyama vya upinzani kushinda ubunge jijini Dar es Salaam limeendelea baada ya mgombea ubunge kwa tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), Maulid Mtulia kutangazwa mshindi wa nafasi hiyo katika jimbo la Kinondoni, akimshinda mgombea wa CCM, Idd Azzan.
Akitangaza matokeo hayo usiku wa kuamkia leo, msimamizi wa uchaguzi katika jimbo hilo ambaye pia ni mkurugenzi wa manispaa ya Kinondoni, Mussa Natty amesema, Mtulia amepata kura 70, 337 huku Azzan aliyekuwa anatetea kiti chake akipata 65,964.
Kwa matokeo hayo, Kinondoni linakuwa jimbo la pili kunyakuliwa na chama hicho katika matokeo rasmi ambayo yamekwishatangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) baada ya kulitwaa jimbo la Temeke lililokuwa linashikiliwa na mwanasiasa mkongwe, Abbas Mtemvu mapema jana.
Ushindi wa chama hicho, unafuatia ule ulioandikishwa na Chadema kwa kunyakua majimbo ya Kawe, Ubungo, 

 
Kibamba na Ukonga, hali inayoashiria kuimarika kwa nguvu za vyama vya upinzani jijini Dar es Salaam hasa vilivyo chini ya mwamvuli wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Kwa mujibu wa Nec, CCM imeibuka vinara katika majimbo ya Ilala, Kigamboni na Segerea huku matokeo ya jimbo jipya la Mbagala yakiwa hayajatangazwa.
Hadi jana, Nec imeshatangaza matokeo katika majimbo 194 ambapo CCM imeshinda viti vya ubunge katika majimbo 135, Chadema majimbo 34, CUF majimbo 23, NCCR-Mageuzi jimbo moja na ACT-Wazalendo jimbo moja.
Hadi Nec inaahirisha utangazaji wa matokeo jana, mgombea urais wa CCM, Dk. John Magufuli alikuwa anaongoza kwa kura 2, 461, 771 sawa na asilimia 57.21 huku mgombea wa Chadema, Edward Lowassa akifuatia kwa kupata kura 1, 764, 785 sawa na 41.01.

No comments:

Post a Comment