Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, December 7, 2015

VIJANA WASHAURIWA KUWA NA MOYO WA KUJITOLEA


Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Prof Elisante Ole Gabriel akitoa nasaa zake kwa Vijana wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali za kujitolea katika taasisi mbalimbali hapa nchini Tanzania wakati wa maadhimisho ya siku ya kujitolea Duniani ambapo Tanzania yamefanyika jijini Dar. (Picha zote na Geofrey Adroph wa Pamoja Blog).
Mkurugenzi Mkazi wa UNDP nchini, Awa Dabo akitoa historia ya kujitolea pamoja na kuwasisitiza vijana kuwa na moyo wa kujitolea katika jamii ili kutengeneza msingi mzuri wa chini.
Mmoja wa vijana wanaojitolea Fatma Mohammed akieleza changamoto anazozipata kama mtoto wa kike kwa kipindi chake chone anapokuwa anajitolea kwenye mashirika mbalimbali.

 
Kikundi kutoka kwa vijana wanaojitolea wakitoa burudani.
Mkuu wa DFID Tanzania, Vel Gnanendran akitoa hamasa kwa vijana wanaojitolea wakati wa maadhimisho ya siku ya kujitolea.
Vijana wakifuatilia kwa makini kinachozungumzwa kutoka meza kuu wakati wa maadhimisho ya siku ya kujitolea.
Ofisa Mtendaji wa VSO, Dk Philip Goodwin akizungumza kambo wakati wa maadhimisho ya siuku ya kujitolea yaliyofanyika jijini Dar
Baadhi ya vijana waliohitimu masomo ya Elimu ya Juu wakitoa ufafanuzi kuhusu changamoto za ajira wanazokutana nazo mara baada ya kuhitimu vyuo hadi kupelekea kufanyakazi za kujitolea ili kuweza kufanikisha malengo yao waliyojiwekea. DSC_0115
Vijana wanaojishughulisha na shughuli za kujitolea katika taasisi mbalimbali hapa nchini Tanzania wakiwa wameshika baadhi ya malengo 17 ya maendeleo endelevu 17.
Mgeni rasmi akiwa kwenye picha ya pamoja na Vijana wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali za kujitolea katika taasisi mbalimbali hapa nchini Tanzania. 

  Na Mwandishi wetu
KATIBU Mkuu Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Prof Elisante Ole Gabriel wamewataka vijana kuwa na moyo wa ujasirimali kwa kuelewa umuhimu wa kujitolea. Ole Gabriel alitoa wito huo mwishoni mwa juma wakati akizungumza na vijana kwenye siku ya kujitolea (International Volunteers Day) iliyoadhimishwa kitaifa nchini Ijumaa badala ya Jumamosi. Alisema kwa kuwa na moyo wa kujitolea vijana wataongeza hamasa na kuthaminiwa na jamii kwani watakuwa wanatatua matatizo yao. 
  Pamoja na kutoa wito huo pia amewataka vijana ifikapo desemba 9 wajitokeze kwa wingi katika kumuunga mkono Rais John Pombe Magufuli ya kujitolea kufanya usafi. Alisema jamii ina matatizo mengi katika sekta ya elimu, hifadhi ya mazingira na ujenzi huku ikiwa na wahitimu wa vyuoni wengi wanaoweza kujitolea kubadili mazingira na kuchukua nafasi ya kufundisha wanafunzi wanaokosa walimu. 
  Aidha alisema kwa kujitolea katika kazi hizo vijana watakuwa wanajenga pia uzoefu na utaalamu unaotakiwa katika ajira mbalimbali zikiwemo za kujiajiri. 
  Alisema kitendo cha kukaa kimya wakati wamemaliza masomo na mafunzo yao bila kutumia ujuzi wao kwa jamii wakisubiri kuajiriwa hakuwasaidii kuwanoa na pia kuwajenga katika moyo wa kujitolea kujenga taifa. Pamoja na kuwataka vijana kujitoa katika kazi za ujenzi wa taifa kwa ajili ya kujenga uzoefu na pia kujinoa kitaalamu amewataka wananchi kuthamini vijana hao kwa kuwasaidia kufanikisha kujitoa kwao kwa taifa katika shughuli mbalimbali. 
  Aidha alisema katika mstari huo huo ni vyema wanafunzi wanapotaka mafunzo kwa vitendo kuhakikishiwa mazoezi hayo ili wawe watu wenye manufaa katika jamii. Katika hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Utalii na kushirikisha mashirika ya kujitolea yaliyopo nchini vijana wameelezwa maana na umuhimu wa kujitolea.
 Ofisa Mtendaji wa VSO, Dk Philip Goodwin aliwataka vijana wasitangulize fedha katika kujitolea kwao kwani kwa kufanya hivyo hawataweza kujipatia hamasa inayoambatana na umuhimu wa kujitolea. Aidha alisema kwamba kwa sasa vijana wana sauti kuliko zamani na hivyo upo umuhimu mkubwa wa kutambua kwamba wao ndio chachu ya maendeleo na wasipofanyia kazi hawataweza kuleta mabadiliko yanayotakiwa. 
  Alihimiza kuwapo kwa moyo wa kujitolea wakati wote kwa kuwa ndio jibu la maendeleo yao ambayo anaamini kwamba hayahitaji fedha. Alisema alishawahi kukueleza jambo nchini Ethiopia wakati vijana wanasema kwamba wana mradi lakini hawawezi kuutekeleza kwa sababu hawana fedha. Aliwaambia vijana hao kwamba wanaweza kuutekeleza mradi huo kwa kuwa wao ndio nguvu kazi na wana akili. 
  Naye Mkuu wa DFID Tanzania, Vel Gnanendran aliwapongeza vijana kwa kufanya vyema katika kuhudumia jamii na kusema shughuli za kujitolea ni sehemu ya kukabiliana na changamoto zinazojitokeza duniani kote. Alisema ni kutokana na moyo wa kujitolea Tanzania inaweza kuhifadhi wakimbizi kutoka maeneo mengine kama Burundi na kusema anaheshimu sana maamuzi hayo. Anasema inafaa vijana wakajitolea kuhakikisha kwamba maeneo yaow anayoishi yanakuwa na nisati inayojali mazingira na hilo linawezekana kutokana na uwapo wa teknolojia na vijana kuwa na uwezo wa kutenda. 
  Naye Mkurugenzi Mkazi wa UNDP nchini Awa Dabo akitoa salamu za Umoja wa Mataifa katika siku ya kujitolea duniani alisema kwamba hali ya baadae ya dunia inategemea vijana na kusema wao ndio chachu lazima waione hali ya sasa na kujikita kuleta mabadiliko yenye tija. Tanzania yenye vijana milioni 16.2 wanaweza kuleta mabadiliko makubwa kama watajitolea kufanikisha mipango mingi ambayo ipo katika jamii. 
  Washiriki wa hafla hiyo katika michango yao walitaka vijana kubadili mitazamo ili watambua kwamba mabadiliko katika mambo mbalimbali inawezekana kwa kushiriki katika shughuli za kujitolea ili kujenga uzoefu na uitaalamu wa kitu wanachokishughulikia. Aidha wametakiwa kuachana na nadharia kwamba kila kitu lazima apatiwe fedha. Vijana hao pia walitaka kuwepo na mfumo wa shughuli za kujitolea ili ionekane kwamba hata serikali inatambua uwapo kwa aina hiyo ya utendaji. 
  Sherehe hizo kubwa za siku ya kimataifa ya kujitolea ya Umoja wa Mataifa imelenga kuleta ushawishi wa kujitolea miongoni mwa vijana kwa ajili ya kutengeneza mahusiano, kukuza utaalamu na pia kujenga uzoefu. Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkazi wa UNDP, Awa Dabo alisema shughuli zakujitolea za Umoja wa Mataifa zilianza nchini tangu mwaka 1974 wakati Umoja wa Mataifa ulipozindua rasmi program hiyo. Kundi la watu wanaojitolea lipo katika miradi mbalimbali ya kiserikali na binafsi yenye lengo la kusaidia wananchi kukabiliana na umaskini, utunzaji wa mazingira na mapambano dhidi ya magonjwa ya UKIMWI. Aidha UN na serikali ya Tanzania kwa sasa inafanya taratibu ya kuragibisha kujitolea na pia kutoa nafasi hiyo katika sekta mbalimbali.

No comments:

Post a Comment