TAIFA STARS YAPANGIWA MSUMBIJI CAN 2013
Tanzania
(Taifa Stars) imepangwa kucheza na Msumbiji katika kinyang’anyiro cha
kutafuta tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika
zitakazofanyika mwaka 2013 nchini Afrika Kusini.
Upangaji
ratiba wa mechi hizo za mchujo ulifanywa juzi (Oktoba 28 mwaka huu) na
kamati ndogo ya michuano hiyo mjini Malabo, Equatorial Guinea.
Jumla
ya nchi 47 ikiwemo mwenyeji Afrika Kusini ndizo zilizothibitisha
kucheza michuano hiyo. Nchi 16 zilizofuzu kucheza fainali za mwakani
nchini Gabon na Equatorial Guinea zenyewe zimepitishwa moja kwa moja
hadi raundi ya mwisho ya mchujo itakayoanza baada ya fainali za 2012.
Raundi
ya kwanza ya awali itahusisha nchi nne ambazo kwenye ubora wa viwango
ndizo ziko chini ili kupata mbili zitakazoingia raundi ya pili ya awali
itakayokuwa na nchi 28. Nchi hizo ni Swaziland, Sao Tome, Lesotho na
Shelisheli.
Stars
imepangiwa kucheza na Msumbiji katika raundi hiyo ya pili ya awali.
Tarehe za mechi hizo ambazo zitachezwa katika nusu ya kwanza ya mwaka
2012 zitatangazwa baadaye.
Mechi
nyingine za raundi hiyo zitakuwa kati ya Ethiopia na Benin, Rwanda na
Nigeria, Congo na Uganda, Burundi na Zimbabwe, Algeria na Gambia, Kenya
na Togo, Sierra Leone na mshindi kati ya Sao Tome na Lesotho.
Nyingine
ni Guinea Bissau na Cameroon, Chad na Malawi, mshindi kati ya
Shelisheli na Swaziland dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo,
Jamhuri ya Afrika ya Kati na Misri, Madagascar na Cape Verde na Liberia
na Namibia.
Timu
14 zitakazopita hatua hiyo zitaungana na 16 zilizofuzu kwa ajili ya
fainali za Gabon/Equatorial Guinea kucheza raundi ya mwisho kupata 15
zitakazoungana na wenyeji Afrika Kusini kwa ajili ya fainali za 2013.
Raundi hiyo itachezwa kati ya Septemba na Oktoba mwakani
No comments:
Post a Comment