SAKATA
la beki Mbuyi Twite wa APR ya Rwanda kudaiwa kunyakuliwa na watani zao,
Yanga, limechukua sura mpya baada ya Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden
Rage, kuamua kubwaga manyanga nafasi yake ya ujumbe wa Kamati ya Katiba,
Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF), kwa madai ya kuikandamiza klabu yake.
Akizungumza
na waandishi wa habari mjini hapa jana, Rage alisema, kamati hiyo ni
miongoni mwa taasisi za TFF, zinazoikandamiza Simba.
Rage
alisema, Twite alisaini mkataba wa miaka miwili na Simba na alilipwa
dola 30,000 za Kimarekani, lakini wakati wakisubiri kupewa barua ya
kumruhusu kutokea APR, wamepata taarifa za kuchanganya kutoka Rwanda
kuwa, mchezaji huyo amesaini mkataba na Yanga.
Alifafanua
kuwa, wamepata taarifa kutoka APR kuwa, hawawezi kumruhusu mchezaji
huyo kuchezea Simba, kwa sababu wamezuiwa na mtoto wa kigogo, ambaye
hakumtaja jina - ila anafahamika.
"Nasema
kweli na hapa nimefunga (mwezi mtukufu wa Ramadhani), tumepata taarifa
kutoka APR kuwa, kuna mtoto wa kigogo wa serikali kutoka Tanzania,
amemzuia mchezaji huyo kutua Msimbazi...
"Sitaki
kumkisia mtu yeyote vibaya na sitasema jina la mtoto huyo wa kigogo wa
juu wa serikali...mchezaji analazimishwa kutoichezea Simba na kupelekwa
timu ya kigogo huyo pasipo kufuata taratibu za soka.
"Huu
ni uonevu mkubwa tuliofanyiwa kwa jumuia ya wapenda michezo kwa ujumla
na hali hii inaonesha wazi kuwa, mchezo wa soka hapa nchini unaelekea
kubaya," alisema huku akitokwa na machozi.
Alisema, mtoto huyo wa kigogo amekuwa akitajwa mara kwa mara kwenye tuhuma za kurubuni wachezaji wa Simba kujiunga na Yanga.
Rage
alisema, vitendo vya aina hiyo vya kutumia mamlaka ya mtu, yawe ya
kiserikali au kifedha, ni kinyume cha taratibu, pia ni hatari kwa
maendeleo ya soka nchini.
"Sitapenda
kuwa Mwenyekiti wa Simba wakati mashabiki wa klabu yangu na watani wetu
wa jadi watakapogeuka kuwa maadui...huku tunakokwenda sasa ni kwenye
kujenga uadui, chuki na kinyongo baina ya mashabiki wetu," alisema.
Alisema,
Simba haitakubali kuona Twite akisajili kuichezea Yanga au timu
nyingine yoyote Tanzania kwa namna yoyote ile, kwani amesajiliwa na
Simba na mkataba wake upo.
Hata
hivyo, alisema, kutokana na mchezaji huyo kutokuwa mwaminifu, Simba
inamtaka arejeshe fedha alizochukua, ikiwemo gharama ya usafiri na mali
ambazo walitumia kwenda Rwanda.
Aliongeza
kuwa, Simba inaitaka serikali kuwa makini katika suala hilo na kwamba,
kitendo kilichofanywa na Yanga kupitia mtoto huyo wa kigogo,
kitahatarisha amani na utulivu wa nchi.
"Naomba
niseme wazi, kwenye hili Simba haitaacha kupambana hata kwa dakika
moja, na kama busara itashindwa kuchukua mkondo wake, suala hili
nitalipeleka kwa wanachama wetu ili waamue watakavyo," alisema.
Wakati
tunakwenda mitamboni, kulikuwa na habari kuwa wawakilishi wa mchezaji
huyo kutoka DR Congo, wametua nchini jana kurejesha fedha za Simba kiasi
cha dola 30,000 za Marekani ambazo zimekabidhiwa kwa TFF.
SOURCE TANZANIA DAIMA
No comments:
Post a Comment