Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, November 29, 2013

ZITTO AZUA BALAA, HENRY KILEWO AHOJIA NA POLISI


 Henry Kilewo (kulia), akiongozana na wakili wake, Mussa Mfinanga, walipowasili Makao Makuu ya Jeshi la Polisi
KATIBU wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Dar es Salaam, Henry Kilewo, jana alihojiwa kwa muda na maofisa wa Jeshi la Polisi kutoka makao makuu ya jeshi hilo jijini Dar es Salaam, akihusishwa kutishiwa maisha Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA).
Kilewo aliwasili katika makao makuu ya jeshi hilo jana majira ya saa 06:03 mchana, akiwa ameongozana na wanasheria wawili pamoja na Diwani wa Ubungo, Boniface Jacob, huku waandishi wa habari waliopiga kambi katika eneo hilo la makao makuu ya Polisi kwa ajili ya kufuatilia kinachoendelea wakilazimishwa  kuondoka.
Baada  ya kuwasili, Kilewo na wanasheria wake walifika katika eneo la mapokezi  na kujitambulisha, ambapo askari aliyekuwa na cheo cha sajenti aliwaelekeza idadi ya watu wanaoruhusiwa kuingia katika chumba cha mahojiano  kuwa ni Kilewo mwenyewe na mwanasheria wake.

Hata hivyo maelekezo hayo ya polisi yalipingwa na wanasheria wa Kilewo, John Malya, ambaye alishinikiza waingie wote kwa ajili ya kusikiliza kile alichoitiwa mteja wao, hali iliyozua mabishano ya muda kabla ya baadhi ya maofisa wa polisi kuridhia matakwa ya wanasheria hao kuingia wote kwa ajili ya mahojiano.

Mara baada ya kuingia ndani, Kilewo na wanasheria wake walikaa kwa zaidi ya saa mbili kabla ya kutoka, ambapo mwanasheria wake, Malya, alizungumza na waandishi wa habari na kuelezea kile kilichosababisha mteja wake kufika katika Makao Makuu ya Jeshi la Polisi.

Malya alisema mteja wake alipata wito wa polisi kupitia simu ya kiganjani kuwa anahitajika Makao Makuu ya Jeshi la Polisi kwa ajili ya mahojiano huku akiwa hajafafanuliwa ni mahojiano ya namna gani na yanahusu jambo lipi.

Alisema baada ya wito huo wa njia ya simu walifika jana kuitikia wito, huku wakitaka kujua kilichosababisha mteja wao kuitwa.

“Kiutaratibu hawakufuata sheria, kwa kuwa hawakutoa hati ya wito au ya kukamatwa na zaidi hakuna mtu aliyefungua mashitaka dhidi ya mteja wangu,” alisema.

Aliongeza kuwa walipofika polisi waligundua kuwa mtu aliyefungua malalamiko ya kutishiwa maisha na mteja wake kutakiwa kutoa maelezo katika fomu ya onyo ya Jeshi la Polisi ni Zitto Kabwe.

Alisema hali ya kutakiwa kuweka maelezo katika fomu ya onyo ilizua mjadala baada ya kutaka kujua kosa linalosababisha mteja wake kuhojiwa.

“Tuliwaambia wabadilishe fomu ya maelezo isiwe ya onyo, itumike ile ya ripoti nao wakakataa, tukakubaliana pale panapoandikwa kosa la mhusika papigwe mstari, kwa kuwa hawakutuambia mteja wetu anashitakiwa kwa kosa lipi,” alisema Malya.

Alisema maelezo ya polisi waliyoyatoa kwao ni kuwa wanafanya uchunguzi juu ya taarifa zilizoandikwa katika gazeti la Majira juu ya Zitto Kabwe kutishiwa maisha na kwamba mteja wake alitoa maelezo na kisha kujidhamini mwenyewe.

Kilewo atoa kauli
Akizungumza baada ya kutoka katika mahojiano, Kilewo alisema Jeshi la Polisi linapaswa kubadilika na kufuatilia masuala ya msingi na liache kujiingiza kwenye masuala ya siasa.

Alisema ni jambo la kusikitisha kuona polisi wanakuwa wa kwanza kuwafuata wanasiasa huku wakishindwa kuainisha hatua waliyofikia katika matukio ya kutekwa na kisha kujeruhiwa kwa mwandishi wa habari, Absalom Kibanda, tukio la kutekwa na kuteswa kwa Dk. Stephen Ulimboka na wengine.

“Nchi inakabiliwa na mambo makubwa, kuna uhalifu unaotishia maisha ya Watanzania, badala ya polisi kuhangaika na hivyo wao wanageuka kuwa wanasiasa,” alisema Kilewo.

Kwa upande wake Msemaji wa Jeshi la Polisi, SSP Advera Senso, alikanusha kuwa wito wa katibu huyo wa CHADEMA hautokani na malalamiko ya Zitto, bali ni utaratibu wa kawaida kwao kumuita mtu yeyote na kuongea naye pale wanapoona kuna haja ya kufanya hivyo.

Kuhusu waandishi kufukuzwa katika eneo la polisi,  Senso alisema polisi haikuwa na haja ya kuita vyombo vya habari katika tukio hilo, na kama mhusika aliviita, waandishi wa habari walipaswa waende katika ofisi yake.

No comments:

Post a Comment