Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Sunday, January 19, 2014

ASKARI MAGEREZA AINGIA DUKANI KWA MWARABU NA KUPORA FEDHA

 
 
Na Mohammed Mhina, wa Jeshi la Polisi, Zanzibar
Jeshi la Polisi Zanzibar linamshikilia Askari mmoja wa Chuo cha Mafunzo sawa na Magereza kwa Tanzania Bara kwa tuhuma za wizi wa shilingi 1,635,000 alizoziiba kutaka katika duka moja lililopo eneo la Makadara mjini Zanzibar.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar ACP Mkadam Khamis Mkadam, amemtaja Askari huyo kuwa ni Sajin Meja (S/Sgt) Hassan Iddi Hassan (45), wa Chuo cha Mafunzo Makao Makuu.
Kamanda Mkadam amesema tukio hilo limetokea jana majira ya saa 11.00 jioni ambapo Askari huyo akiwa amevaa kiraia, alifika dukani hapo kama mteja wa kawaida na wakati muuzaji wa duka hilo akimhudumia mteja mwingine upande wa pili, aliingia ndani na kukimbilia kwenye droo ya pesa na kuzichukua fedha hizo na kuondoka.
Amesema wakati akichukua fedha hizo, Askari huyo alionwa na baadhi ya wateja na hivyo kumshitua muuzaji huyo na kuanza kupiga kelele za mwizi na ndipo alipofukuzwa na wananchi na kwa vile eneo hilo lilikuwa karibu na Kituo cha Polisi askari waliwahi haraka na kumkamatwa kabla ya kupata kipigo kikali kutoka kwa wananchi.
Kamanda Mkadam, amesema fedha zote alizokua ameziiba mtuhumiwa huyo zimeokolewa na Polisi na zimehifadhiwa kama kielelezo mahakamani.
Hilo ni tukio la tatu kutokea mjini Zanzibar katika kipindi cha mwaka huu ambapo tukio la kwanza ni lile la jaribio la wizi katika maghala ya Bakheresa eneo la Fuoni nje kigodo ya mji wa Zanzibar ambapo watuhumiwa watatu walikamatwa wakiwa na silaha aina ya gobore linalotumia risasi za short gun.
Na tukio linguine ni la kukamtwa kwa majambazi wanne akiwemo Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini wakiwa na silaha tatu zikiwemo bastola mbili na SMG moja baada ya kumvamia mfanyabiashara mmoja na kumpora milioni 11.5 eneo la Rahaleo mjini Zanzibar.
Matukio hayo yote yakiwa na jumla ya watuhumiwa wanane na silaha nne yaliweza kukabiliwa kwa haraka na Polisi kufuatia msaada wa wananchi wa kutoa taarifa za haraka polisi na wenyewe kujitolea kusaidiana na Polisi kuwakabili watuhumiwa na kufanikisha ukamataji salama.

No comments:

Post a Comment