Pages

Tuesday, May 13, 2014

Gavana:Nina "taarifa" walipo wasichana



Gavana wa jimbo la Borno, Nigeria, Kashim Shettima
Gavana wa jimbo la Borno nchini Nigeria amesema ana taarifa za mahali walipo wasichana wanafunzi wapatao 200 waliotekwa na kundi la Kiislam la Boko Haram.
Gavana Kashim Shettima amesema amewasilisha taarifa hizo kwa jeshi kwa uthibitisho kuhusu walipo wanafunzi hao.
Bwana Shettima amesema hafikirii kuwa wasichana hao wamepelekwa nje katika mipaka na nchi za Chad au Cameroon.
Mapema, rais wa Ufaransa amejitolea kuandaa mkutano wa viongozi kuzungumzia kundi la Boko Haram.
"Nimependekeza, kwa Rais Goodluck Jonathan wa Nigeria, kufanya mkutano na nchi jirani na Nigeria" amesema Rais Francois Hollande.
"Iwapo nchi hizo zitaafiki pendekezo hilo, mkutano utafanyika Jumamosi" amesema.
Nchi jirani na Nigeria, kama vile Cameroon, Niger na Chad, zitaalikwa katika kikao cha usalama.
Taarifa zinasema Marekani, Uingereza na Umoja wa Ulaya huenda pia wakahudhuria mkutano huo.
Marekani, Uingereza na Ufaransa tayari zimeahidi msaada wa kiufundi kwa serikali ya Nigeria.
Boko Haram imekuwa ikiendesha vitendo vya vurugu dhidi ya serikali ya Nigeria tangu mwaka 2009.
Inafikiriwa kuwa wengi wa wasichana waliotekwa ni Wakristo, japokuwa katika waliotekwa wamo pia Waislamu.
Kutoka eneo la Chibok walikotekwa, ni jumuia ndogo ambako familia za jumuia hiyo zina watu wa imani zote mbili za Kikristo na Kiislamu.Chanzo BBC

No comments:

Post a Comment