Pages

Thursday, June 5, 2014

IRINGA WALISHWA NYAMA YA MIZOGA YA PUNDA, PAKA NA MBWA JIONEE HAPA


Mwananchi huyu alikutwa akiuchuna mzoga wa punda huyu huko Migori wilayani Iringa. Maeneo mengi ya vijijini katika Mkoa wa Iringa yanalalamikiwa na wananchi kwamba wanalishwa mizoga ya punda, paka na mbwa. (Picha na Said Ng’amilo).



Na Mathias Canal, Iringa

WAKAZI wa Kitongoji cha Lugofu katika Kijiji cha Ilandutwa, Wilaya ya Iringa Vijijini, mkoani Iringa wamelaani kitendo cha baadhi ya wafanya biashara wa nyama kijijini hapo kuwalisha nyama ya paka, mbwa na punda pasipo kujua.Wakizungumza na Kwanza Jamii kijijini hapo, wanakijiji hao walisema mara ya kwanza walipopata taarifa ya kulishwa nyama ya paka hawakutoa taarifa kwa mtu yeyote kutokana na kuamini kwamba wafanyabiashara hao watajirekebisha kwa kuacha uuzaji wa nyama hizo haramu.


Hata hivyo, vitendo hivyo vimeendelea kushika kasi ambapo wafanyabiashara hao wamekuwa wakiokota hata mizoga ya punda, paka na mbwa waliogongwa na magari au kukamata mbwa wa watu kijijini hapo na kuiuza nyama hiyo kwa wananchi kinyume cha sheria na taratibu za afya.

Vincent Mtale mkazi wa Kitongoji cha Lugolole “A” amesema Balozi wa Kitongoji cha Lugofu, Ngojea Ng’alla, hivi karibuni aliiba mbwa wa Angelina Kanyika na kumpeleka kwa kijana anayefahamika kwa jina la Manati Dunda.“Mtu mmoja anayeitwa Nung’uniko alimfukua punda aliyekufa akazikwa, hivyo yeye akamchuna na kutengeneza supu ya mchanganyiko wa nyama ya punda, nyama ya nguruwe na viazi mviringo na kuiuza kwenye kijiji hicho ambacho nyama hiyo ilishambuliwa kwa kasi na wanakijiji bila wao kufahamu.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Lugolole “A” amekiri kuibiwa kwa mbwa wa mama huyo na kuuzwa Shs. 12,000 kwa makubaliano ya kuchanganya na nyama ya nguruwe na viazi ili watu wasitambue kama kuna mchanganyiko huo ili waweze kugawana fedha zitakazopatikana baada ya mauzo.Angelina Kanyika mwenyewe amewataja vijana wawili waliohusika na wizi huo wa mbwa wake aliyekuwa na mimba, kuwa ni Ngojea Ng’alla na mwenzake Manati Dunda ambapo baada ya kumchinja wakawatupa watoto waliokuwa tumboni.“Baada ya kufanya upelelezi juu wa mbwa wangu niligundua watu hao ndio waliokwiba, nimesikitishwa sana kwa kitendo hicho kwani mbwa wangu aliuawa kwa kupigwa marungu hadi kufa kabla ya kumchuna,” alisema kwa masikitiko.

Hata hivyo, Dunda amekiri kuiba mbwa, kuchinja na kuuza vibudu kijijini hapo na kwamba amekuwa akifanya hivyo kwa miaka mitano sasa.Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Ilandutwa, Isack Nganingo, amekiri kuuzwa kwa nyama hizo haramu kijijini hapo huku akikiri kuibwa na kuchinjwa kwa mbwa wa Angelina Kanyika na hatimaye nyama yake kuuzwa katika kijiji hicho.Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa wananchi wanaotaka kuchinja mnyama wa aina yeyote kijijini hapo kufika ofisini kwake ili kupewa kibali cha kuchinja mnyama huyo kwa kuzingatia taratibu na kanuni za afya.

No comments:

Post a Comment