Pages

Friday, February 13, 2015

HOSEA: HAKUNA ATAKAYEPONA ESCROW

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imesema kuwa haikurupuki katika kuwashughulikia na kuwafikisha mahakamani viongozi wanaotuhumiwa kujipatia fedha kutoka kwenye akaunti ya Tegeta Escrow na kwamba ushahidi pekee ndiyo utakaofanya kuwafikisha mahakamani watuhumiwa.
Akizungumza mara baada ya kuzindua jengo la ofisi 


ya mkoa la taasisi hiyo mjini hapa juzi, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hosea alisema hakuna atakayeachwa katika sakata hilo, iwapo ushahidi utathibitisha pasi na shaka kwamba alihusika.
Alisema uchunguzi dhidi ya viongozi na watu mbalimbali, waliohusika na uchotaji wa fedha hizo, unaendelea na kwamba ushahidi utakapokamilika, kila mmoja atapata kile anachostahili bila kumuonea.
“Hatutaki kukurupuka katika kushughulikia watuhumiwa wa sakata la Escrow na muhimu ni ushahidi ambao utawatia hatiani watuhumiwa, ni aibu kwangu kumfikisha mtuhumiwa mahakamani na mwisho wake siku ushahidi hautoshi na mtuhumiwa kuachiwa huru,” alisema Dk Hosea.
Aliwataka wananchi kuwa na imani na chombo hicho katika kushughulikia suala hilo na kwamba haki itatendeka kwa kuwashughulikia watuhumiwa wote kwa haki.
Aliwataka wananchi waache kusikiliza kelele, zinazopigwa na baadhi ya watu kwamba hawafanyi kitu au kuwashughulikia watuhumiwa wakubwa.
Tangu kuibuka kwa sakata la kuchotwa kwa fedha katika Akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa imefunguliwa katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) baada ya kuwepo kwa mgogoro wa kibiashara baina ya Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) na kampuni binafsi ya kufua umeme ya IPTL, hatua kadhaa zimechukuliwa na Serikali.
Hatua hizo ni pamoja na kuvunjwa kwa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco na kutenguliwa kwa Uwaziri Profesa Anne Tibaijuka aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Pia, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alijiuzulu mwishoni mwa mwaka jana akidai kuwa ushauri wake katika suala hilo haukueleweka, hivyo kuchafua hali ya hewa.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo pia alijiuzulu mwezi uliopita na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Eliakim Maswi amesimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yake juu ya ushiriki wake katika sakata hilo.
Katika mkutano wake wa 16 na 17, Bunge lilitoa maazimio manane, yakiwemo ya kuwawajibisha viongozi waliotajwa kuhusika kwa namna moja ama nyingine na uchotwaji wa karibu Sh bilioni 300 katika akaunti ya Tegeta Escrow.
Akaunti ya Tegeta Escrow ilifunguliwa BoT mwaka 2006 kwa ajili ya kuhifadhi fedha za malipo ya tozo ya uwekezaji (capacity charges) zilizokuwa zinalipwa na Tanesco, kabla hazijakabidhiwa kwa anayelipwa, ambaye ni IPTL.

HABARI LEO

No comments:

Post a Comment