Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, February 11, 2015

Mtuhumiwa wa Escrow abadilishiwa mashtaka


Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru) imembadilishia hati ya mashtaka Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma aliyekuwa akikabiliwa na shtaka la kupokea rushwa ya Sh 323 milioni toka kwa James Rugemalira fedha ambazo ni sehemu ya fedha za Akaunti ya Tegeta Esrow.

Katika hati mpya iliyosomwa Jana  na Mwendesha



 Mashtaka wa Takukuru Leonard Swai mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Emillius Mchauru aioneshi tena kuwa fedha zilizopokelewa na Mujunangoma toka kwa Rugemalira ni sehemu ya fedha za Akaunti ya Tegeta Escrow.

Swai kupitia hati hiyo mpya alidai kuwa Februari 5, 2014 Mujunangoma akiwa mtumishi wa serikali kama Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Rugonzibwa Mujunangoma alipokea rushwa ya Sh Sh323 milioni kupitia akaunti yake namba 00120102602001 iliyopo kwenye  benki ya  Mkombozi .

Alidai kuwa mshtakiwa huyo alipokea  kiasi hicho cha fedha kutoka kwa James Burchard Rugemalira, ambaye ni mshauri huru wa kitaalamu, mkurugenzi wa VIP na mkurugenzi wa zamani wa Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL kama tuzo kwa kushughulikia mambo ya ufilisi wa muda wa kampuni hiyo.

Aliendelea kudai kuwa baada ya kujipatia kiasi hicho cha fedha alishindwa kueleza maslahi yake kwa Katibu Mkuu wa Wizara yake ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na kwenye tume ya maadili  ya Viongozi.

Baada ya kusomewa mashtaka hayo, Mujunangoma ambaye anatetewa na mawakili Deo Ringia na Jamuhuri Johnson  alikana na upande wa mashtaka ulidai kuwa upelelezi umekamilika na wapo tayari kwa ajili ya kumsomea mshtakiwa huyo maelezo ya awali (PH) yanayohusiana na shtaka hilo linalomkabili.

Wakili Deo Ringia alitoa taarifa mahakamani hapo kuwa  kutokana na uchambuzi walioufanya wameona katika kesi hiyo kuna masuala  ya Kikatiba ambayo wanapenda mahakama iyaangalie na kuyatolea maelekezo. Baada ya kutolewa kwa taarifa hiyo Hakimu Mchauru ameiahirisha kesi hiyo hadi Februari 24,2015 kwa ajili ya kuisikiliza taarifa hiyo.

Awali

Shtaka la awali, Mujunangoma alikuwa akidaiwa kuwa  Februari 5, 2014 katika Benki ya Mkombozi iliyopo wilayani Ilala, Dar es Salaam,  akiwa Mkurugenzi wa Huduma za Sheria wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alipokea rushwa ya  kiasi hicho cha fedha kutoka kwa James Burchard Rugemalira  kama tuzo kwa kushughulikia mambo ya ufilisi wa muda wa kampuni hiyo fedha ambazo ni sehemu ya fedha za Akaunti ya Tegeta Escrow.

Mshtakiwa huyo anayedaiwa kufanya kosa hilo,  kinyume na kifungu cha 15 (1)cha Sheria ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa, Namba 11 ya mwaka 2007 yupo nje kwa dhamana na akaunti yake inayodaiwa kupokea rushwa toka kwa Rugemalira imezuiwa.

No comments:

Post a Comment