Na Baraka Mbolembole, Dar es Salaam,
Mchezaji ambaye amecheza timu ya Taifa wa miaka 12 mfululizo
huku akichezea klabu moja tu maishani na kubeba majukumu ya unahodha klabuni na
timu ya Taifa anaweza kushindwa kuwa kocha bora mwenye mafanikio endapo tuhuma za kuomba
pesa kwa wachezaji ili awapange katika mechi zitafika mbali na kuainika ni za
kweli.
Kila kitu kina madhara Fulani kwa kitu kingine, mathalani ‘ Nondo ni mharibu wa vitambaa au
nguo za manyoya, na Kutu hula chuma kigumu bila shida yo yote’. Kuna wakati
akili zetu wanadamu huwa
kamili na wakati mwingine huwa si nzima-huwa leguvu
kwa kujiendesha. Hivyo basi, ‘ Sumu ya Mtu ni Kijicho na Chuki’ Chuki ina
madhara na kijicho kina aibu kubwa kuliko kitu chochote ambacho si halali kwa
fikra au kwa tendo la kushawishi mtu kula kitu hicho hata kama kina ‘ ladha’
nyingi kinywani.
Kiungo mshambulizi wa Mtibwa Sugar ( Jina linahifadhiwa kwa
sasa) amesema kuwa kuvurunda kwa timu hiyo msimu huu ni sababu ya kocha mkuu wa
timu hiyo, Mecky Mexime. Mchezaji huyo anayejiandaa kuachana na timu hiyo mara
baada ya kumalizika kwa msimu ameweka wazi kuwa Mecky ( mchezaji –nahodha wa
zamani wa timu hiyo na timu ya Taifa, Taifa Stars) amekuwa akiwapanga timu yake
kwa sababu zisizo za kimpira- Kifupi ni lazima umpatie pesa ili upate nafasi ya
kucheza Mtibwa Sugar.
“ Tatizo la Mtibwa ni kocha ( Mecky), ukitoa sababu
nyingine, mwalimu huyo amekuwa akipanga timu yake kama mchezaji utampatia pesa”
anasema mchezaji huyo alijiunga na Mtibwa mwaka 2011 wakati timu hiyo ikinolewa
na Mkenya, Tom Olaba. Kwanza niseme wazi kuwa Mecky ni mchezaji wa zamani
ambaye Taifa linamchukulia kama mfano wa kuigwa kutokana na mchango wake mkubwa
alioutoa wakati alipokuwa mchezaji wa Stars kwa miaka 12 mfululizo.
Nyakati za mwisho za uchezaji wake, Mecky alijiingiza katika
mafunzo ya ukocha huku akiichezea klabu yake ya Mtibwa na mara baada ya
kustaafu soka la ushindani miaka mitatu iliyopita Mecky alipewa kazi ya ukocha
msaidizi katika klabu hiyo aliyoichezea kwa maisha yake yote na kushinda mara
mbili ubingwa wa ligi kuu, 1999 na 2000. Wakati akiwa msaidizi wa Olaba, Mecky
alisimamishwa na uongozi wa klabu hiyo baada ya kundi kubwa la wachezaji kwenda
kwa utawala wa juu na kulalamikia kitendo cha Mecky kuwashawishi wachezaji
kucheza chini ya kiwango ili timu ifanye vibaya na kocha mkuu Olaba aonekane
hafai.
Mecky alihitaji haraka nafasi ya ukocha mkuu pale Mtibwa
Sugar, akiamini kuwa uzoefu na mbinu za ufundishaji alizowahi kupata kutoka kwa
walimi John Simkoko, Mshindo Msolla, Burkard Pape, James Siang’a, Salum
Mayanga, Olaba, Marcio Maximo, Jan Poulsen
zingeweza kumpatia mafanikio ya haraka. Mtibwa ilimuajiri Mecky kama
kocha mkuu mara baada ya kumalizika kwa mkataba wa Olaba msimu wa 2011/12 na
timu hiyo iliporomoka hadi nafasi ya Tano ikimaliza nyuma ya Simba SC waliotwaa
ubingwa, Azam FC waliomaliza nafasi ya pili na Yanga SC na Kagera Sugar ambazo
zilikamilisha orodha ya timu nne za juu.
Yalikuwa ni matokeo mabaya zaidi kwa Mtibwa katika kipindi
cha ‘ Muongo Mmoja’ lakini imani kwa Mecky ilikuwa kubwa kwa kuwa aliingia
klabuni na mtazamo wa kuijenga upya Mtibwa ikitumia zaidi wachezaji vijana
kutoka timu ya pili na si kusajili wachezaji wengi wanaotemwa katika klabu za
Yanga na Simba. Lakini mpango kama huo unahitaji muda zaidi, bila shaka klabu
na Mecky mwenyewe walikuwa wakitambua hilo ndiyo maana wameendelea kufanya kazi
pamoja licha ya timu hiyo kuporomoka hadi nafasi ya Tisa msimu uliopita.
“ Ili kocha akupe namba
ni lazima umpe kocha pesa, hafanyi kwangu tu ni wachezaji wengi
wanakutana na hali hiyo” anaendelea kusema mchezaji huyo ambaye alifanya vizuri
mno msimu uliopita licha ya timu kumaliza katika nafasi mbaya tangu ilipopanda
daraja mwaka 1997. Mtibwa itacheza na Kagera Sugar katika uwanja wa Kambarage,
Shinyanga Jumatano hii wapo nafasi ya nane katika msimamo baada ya kucheza
michezo 18 na kukusanya alama 23 ilianza vizuri msimu huu na kuongoza ligi kwa
miezi mitatu mfululizo lakini wamefanikiwa kushinda mara moja tu tangu kuanza
kwa mwaka huu na sababu kubwa wachezaji wanasema ni Mecky. Naendelea kumtafuta
mwalimu huyo na chochote atakachosema nitawajuza .
0714 08 43 08 CHANZO SHAFIH DAUDA
No comments:
Post a Comment