Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, July 23, 2015

Mwakyembe, Malila wapeta kura za maoni Chadema



Waandishi Wetu, Mwananchi

Dar es Salaam/Sumbawanga. Mkutano Maalumu wa Chadema Jimbo la Temeke umempitisha Bernard Mwakyembe kugombea ubunge katika jimbo hilo. Mwakyembe (33) alipata ushindi wa asilimia 66.7 kwa kuvuna kura 80 kati ya 120 katika mkutano uliotaka kuingia rabsha baada ya wajumbe kutoka Kata ya Sandari kuzuiwa kupiga kura kutokana na kutokidhi vigezo vya katiba.

Msimamizi wa uchaguzi huo, Halfan Milambo alisema mgombea Emmanuel Msuya alipata kura 39 sawa na asilimia 32.5 huku Mhandisi Samson Msambaza akipata kura moja sawa na asilimia 0.8. Mwakyembe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Temeke, iwapo atafanikiwa kupitishwa na Kamati Kuu ya chama hicho, atasubiri kihunzi cha mwisho ndani ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kabla ya kuvaana na CCM na vyama vingine. Hata hivyo, baadaye wagombea hao walipopigiana kura wenyewe kwa wenyewe kumchagua anayefaa kupeperusha bendera ya Chadema, mgombea wa mwisho wa kura za mkutano mkuu aliibuka mshindi. Milambo alisema katika kura hizo za kupigiana, Mwakyembe alishika nafasi ya pili huku Msuya akifunga pazia. 
 
Wajumbe 120 kati ya 145 wa Mkutano Mkuu Jimbo la Temeke ndiyo waliopiga kura jana mchana.

Sintofahamu Ukonga

 Hali ya sintofahamu iliibuka jana wakati wa mchakato wa upigaji kura ya maoni Jimbo la Ukonga baada ya baadhi ya wajumbe wa Serikali za Mitaa na wanachama wengine kutoruhusiwa kuingia mkutanoni. Hali hilo ilisababisha shughuli kusimama kwa muda huku viongozi wakijitahidi kueleza taratibu za mkutano huo na watu wanaotakiwa kushiriki. Hata hivyo, Mjumbe wa Mtaa wa Kivule, Chacha Marwa alisema walifika eneo hilo kuwasikiliza wagombea.  Mwanachama mwingine, Abdallah Khalfan alisema viongozi wameanza kuwagawa wanachama bila sababu za msingi. Akitoa ufafanuzi juu ya utaratibu wa mkutano huo, Kaimu Mratibu wa Chadema Kanda ya Pwani, Casmir Mabina alisema waliotakiwa kupiga kura ni wajumbe wa kamati ya utendaji na wenyeviti wa Serikali za Mitaa katika jimbo husika. Baada ya ufafanuzi huo, mkutano ulianza na hadi saa moja usiku ulikuwa ukiendelea.

Malila apeta Sumbawanga

Katika Jimbo la Sumbawanga Mjini, Shadrick Malila aliibuka na ushindi wa kishindo. Msimamizi wa uchaguzi huo, Ofisa wa Chadema Kanda ya Nyasa, Paschal Ngaiza alimtangaza Malila ambaye ni mfanyabiashara maarufu kwa jina la Ikuwo kuwa ni mshindi kwa kura 280 akifuatiwa na mfanyabiashara mwingine, Cassiano Kaegele ‘Upendo’ aliyepata kura 30. Wagombea wengine, na kura zao Mussa Ndile (10) Baraka Lyimo (3), Eliud Mwasenga (2) na James Kusula (1).

 Imeandikwa na Nuzulack Dausen, Peter Elias na Mussa Mwangoka.

No comments:

Post a Comment