Kiongozi
wa Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya
Mipango, Bibi Florence Mwanri (Wapili Kushoto) akipata maelezo ya
maendeleo ya Mradi wa Maji ya Mtiririko Kijiji cha Igurusi kutoka kwa
Mshauri wa Mradi huo Mhandisi Kimambo.
Wakaguzi walipata bahati ya kujionea chanzo cha maji hayo kutoka nje kidogo ya Kijiji cha Igurusi.
Kikazi Zaidi.. Timu
ya ukaguzi pia ilikagua maendeleo ya Tanki la kuhifadhia maji la mradi
huo. Pichani, Kiongozi wa Ukaguzi, Bibi Florence Mwanri akipanda ngazi
kwenda kujionea maendeleo ya ujenzi wa Tanki.
Ujenzi unaendelea.. Mafundi
wakiendelea na kazi ya ujenzi huku wakaguzi hao wakikagua. Tanki hilo
lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita laki tano ambalo limeshakamilika kwa
asilimia 90. Hadi kukamilika kwake Mradi utagharimu jumla ya Shilingi
zaidi ya Milioni 830.
Naibu
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango (Uchumi Jumla), Prof. Longinus
Rutasitara (Aliyenyanyua Mkono) akisisitiza jambo wakati wa ukaguzi wa
Mradi wa Maji wa Iwalanje wakati Timu ya Ukaguzi ilipotembelea Mradi
huo.
aonja Maji..
Kiongozi wa Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume
ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Mwenye nguo nyeusi) akionja maji
kutoka moja ya njia za kusambazia maji ya Mradi wa Maji wa Iwalanje.
Kukamilika kwa Mradi huo kumetoa suluhisho la adha ya muda mrefu
iliyokuwa ikiwakabili wakazi wa Kijiji cha Iwalanje na Taasisi
mbalimbali za Serikali zinazohudumiwa na Mradi huo.
Timu
ya Ukaguzi pia ilishuhudia Tanki la kuhifadhia maji la Mradi huo lenye
uwezo wa kuhifadhi lita 43,000. Mradi huo umegharimu jumla ya Shilingi
milioni 273, ambapo mpaka sasa Mradi unahudumia zaidi ya kaya 2, 506.
Viongozi
wa Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya
Mipango, Prof. Longinus Rutasitara (Wanne Kushoto aliyenyanyua mkono) na
Bibi Florence Mwanri (Watatu Kushoto) wakipata maelekezo ya Mradi wa
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe. Pichani ni ujenzi wa sehemu wa
kukaa abiria ukiendelea.
Meneja uwanja wa ndege wa Songwe jijini Mbeya, Eng. Valentino Kadeha (Kulia) akitoa maelekezo kwa Timu yaUkaguzi
wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango
ilipotembelea Mradi huo. Kwa Mujibu wa Mhandisi Kadeha Uwanja huo
umeshakamilika kwa aslimia 70 na utakuwa na uwezo wa kuhudumia abiria
zaidi ya 300 kwa saa.
Ukaguzi wa Hospitali.. Kwa kutambua umuhimu wa afya kwa maendeleo ya nchi, Timu ya Ukaguzi
wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango pia
ilitembelea Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Mbeya. Timu hiyo ilishuhudia
maendeleo ya ujenzi wa jengo la Kitengo cha Dharura (linaloonekana
nyuma).
Aliyekuwa
Mkurugenzi wa wa hospitali ya rufaa Mbeya Dr Sankey (Wapili Kulia)
akieleza changamoto zinazozikabili Hospitali hiyo kwa Timu ya Ukaguzi wa
Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango pia
ilipotembelea Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Mbeya. Aliyeambatana nae ni
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa hospitali hiyo, Dk Humphrey Kiwelu (Kulia). Picha zote na Saidi Mkabakuli
====== ===== =======
MBEYA WAANZA KUNEEMEKA NA
MPANGO WA MAENDELEO
Na Saidi Mkabakuli
Wakazi
wa mkoa wa Mbeya na vitongoji vyake wameanza kufaidi matunda ya uwekezaji wa
kimkakati uliobainishwa na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011 – 2016)
kupitia ujenzi wa miundombinu ya maji, ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa
wa Songwe, pamoja na ujenzi wa jengo la Kitengo cha Dharura katika Hospitali ya
Rufaa iliyopo mkoani humo.
Hayo
yalibainika wakati Timu ya Ukaguzi wa
Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango ilipofanya ziara ya
ukaguzi wa baadhi miradi ya maendeleo kushuhudia hali ya utekelezaji wa miradi iliyopo
mkoani humo.
Akizungumza
wakati wa ukaguzi huo mmoja wa Kiongozi wa Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo
kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri anayeshughulikia
Huduma za Jamii na Maendeleo ya Idadi ya Watu, alisema kuwa katika kutambua
changamoto zinazowakabili wakazi wa mkoa huo, Mpango wa Maendeleo uliweka
bayana uanzishaji na uendelezaji miradi ya maendeleo ili kutoa huduma za kijamii
kwa Watanzania wote.
“Mpango
wa Kwanza wa Maendeleo wa Miaka Mitano unawianisha katika mfumo mmoja wa
mipango mbalimbali ya maendeleo ya kitaifa ili kutoa mwongozo wa utekelezaji na
kuipa Serikali fursa na mfumo rasmi wa ufuatiliaji na tathmini wa miradi ya
maendeleo kitaifa ikiwemo miradi hii tunayokagua leo,” alisema Bibi Mwanri.
Bibi Mwanri aliongeza kuwa kwa kutambua changamoto za
uhitaji wa maji kwa baadhi wakazi wa vijijini wa mkoa wa Mbeya, Serikali
iliwekeza zaidi ya bilioni moja kwa ajili ya uwekezaji katika miradi ya maji ya
Mradi wa Maji ya Mtiririko Kijiji cha Igurusi na Mradi
wa Maji wa Iwalanje.
“Hii
ni baadhi ya miradi inayonufaisha wakazi wa mkoa huu ambayo tumetembelea. Kukamilika
kwa Miradi hii kumetoa suluhisho la adha ya muda mrefu iliyokuwa ikiwakabili
wakazi wa Mbeya na vitongoji vyake pamoja na taasisi mbalimbali za Serikali
zinazohudumiwa na Miradi hii,” alisema.
Naye Naibu Katibu Mtendaji (Uchumi Jumla), Prof.
Longinus Rutasitara ambaye alikuwa kiongozi mwenza wa ukaguzi huo, alisema kuwa
maendeleo ya miradi hiyo ni ishara tosha kuwa wakazi wa Mbeya na vitongoji
vyake wataanza kuneemeka na uwekezaji huo wa Serikali kwa kupata fursa
mbalimbali za kimaendeleo kupitia miradi hio.
Akitolea mfano wa uwekezaji
katika Mradi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Songwe, Prof. Rutasitara alisema
kuwa kukamilika kwa Uwanja huo ambao
umeshakamilika kwa zaidi ya asilimia 70, sio tu kutaongeza shughuli za kiuchumi
mkoani Mbeya bali kunatoa fursa za kufungulia za
kuwezesha ukuaji mpana wa uchumi wa nchi.
“Uwanja wa Songwe unatoa fursa za
misingi wa uchumi kwa watu walio wengi, hizi ni juhudi za makusudi za Serikali
za kuondoa vikwazo vilivyopo hivi sasa katika kutumia utajiri mkubwa wa
rasilimali zilizopo mkoani Mbeya,” alisema Prof. Rutasitara.
Serikali imeaandaa Mpango wa
Maendeleo wa Miaka Mitano ukiwa na lengo la kuwa na mfumo madhubuti wa
kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025. Mpango huu utadumu kwa mwaka
2011/12 - 2015/16 na utakuwa wa kwanza
katika mfululizo wa mipango mitatu
itakayotekelezwa kwa awamu. Lengo la Dira ni kuibadili Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati
ifikapo 2025.
No comments:
Post a Comment