Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, September 15, 2014

ZANZIBAR YADHIMISHA SIKU YA UNYONYESHAJI DUNIANI



 Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini ‘A’ Khamis Jabir Makame akisalimiana na kina mama wanyonyeshaji waliofika katika madhimisho ya siku ya Unyonyeshaji Duniani yaliyofanyika huko kijiji cha Nungwi Kaskazini Unguja.
Kaimu katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt Jamala Adam Taib akitoa hutuba yake katika madhimisho ya siku ya Unyonyeshaji Duniani yaliyofanyika katika Kijiji cha Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja.


Baadhi ya waalikwa walioshiriki katika madhimisho ya siku ya Unyonyeshaji Duniani  wakitizama ngoma ya Mchikicho (haipo Pichani) iliyotumbuiza katika madhimisho hayo.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini ‘A’ Khamis Jabir Makame akiwahutubia wananchi katika madhimisho ya siku ya Unyonyeshaji Duniani iliyoadhimishwa septemba 13 katika Kijiji cha Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja (kusho) Mwakilishi wa Shirika la kuhudumia watoto Dunia UNICEF Bi. Francesca Morandini. 
Mgeni Rasmi Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini ‘A’ Khamis Jabir Makame wakati kati waliokaa akiwa katika Picha ya pamoja na Waalikwa waliofika katika madhimisho ya siku ya Unyonyeshaji Duniani yaliyofanyika huko kijiji cha Nungwi Kaskazini Unguja. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar
Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar 
Taasisi binafsi zimeshauriwa kutoa Likizo kwa Wafanyakazi wao pale wanapojifungua ili wapate muda wa kutosha wa kuwanyonyesha Watoto wao. Kufanya hivyo kutasaidia makuzi mema kwa Watoto hao sambamba na kuwaepushia magonjwa ambayo sio ya ulazima katika maisha yao. 
Ushauri huo umetolewa na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Khamis Jabir Makame kwa Niaba ya Waziri wa Afya katika hafla ya kilele cha Wiki ya Unyonyeshaji bora kwa watoto iliyofanyika kitaifa Nungwi Kaskazini Unguja. 
Amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar hutoa siku 82 kwa wafanyakazi wake pale wanapojifungua ili kuwanyonyesha vyema watoto wao jambo ambalo linapaswa kuigwa na Taasisi binafsi. 
Jabir amefahamisha kuwa ili kuboresha uhai na maendeleo bora ya Mtoto,Wazazi wanalazimika kufuata mipangilio bora ya unyonyeshaji ikiwa ni pamoja na kuwanyonyesha watoto wao mfululizo kwa muda wa miezi sita. 
“Utaratibu wa kitaalamu ni Mtoto kunyonyeshwa Miezi sita mfululizo bila kupewa kitu chengine” Alisema Kaimu huyo wa Mkoa. 
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt Jamala Adam Taibu amesema hali ya unyonyeshaji kwa Zanzibar hairidhishi ambapo watoto hunyonyeshwa kwa wastani wa Wiki mbili jambo ambalo ni hatari. 
Amefahamisha kuwa Watoto wanaonyonyeshwa na Mama zao kwa wastani wa miezi sita bila kupewa chakula kingingne hupata kinga nzuri ya mwili na makuzi mema katika maisha yao.
Dkt Jamala ameongezea kuwa Wazazi wanaofuata utaratibu nzuri wa unyonyeshaji huwasaidia pia kuepukana na magonjwa mbali mbali katika miili yao ikiwa ni pamoja na Ugonjwa wa Saratani ya Titi. 
Awali Mkuu wa Shirika la Kuhudumia watoto duniani UNICEF Ofisi ya Zanzibar Bibi Francesca Morandini amefahamisha kuwa Mtoto anapocheleweshwa kunyonyeshwa au kupewa vitu vingine kabla ya kutimia miezi 6 Akili na Mwili wake hudumaa jambo ambalo litasababisha Taifa kukosa nguvu kazi bora mbeleni. 
Ameshauri Wazazi wa Kiume kushirikiana vyema na Wake zao ili kuhakikisha Mtoto anapata haki yake ya Msingi ambayo imesisitizwa pia katika Vitabu vya Dini. 
Kila ifikapo Septemba 13, Zanzibar hungana na nchi nyingine Duniani kuadhimisha Siku ya unyonyeshaji Bora Dunia ambapo malengo yake makuu ni kukumbushana Mikakati bora ya unyonyeshaji ili kuboresha Uhai na maendeleo ya Watoto duniani.

No comments:

Post a Comment