Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Ernest Mangu amelifumua Jeshi la Polisi nchini kwa kupanga na kupangua vigogo wake, huku baadhi wakipandishwa nyadhifa.
Pangapangua hiyo imewagusa pia maofisa waandamizi wa jeshi hilo walioko makao makuu, makamanda wa mikoa, wakuu wa upelelezi wa mikoa (RCO) na wakuu wa polisi wa wilaya (OCD).
Habari za uhakika kutoka ndani ya makao makuu ya Jeshi la Polisi zinasema pangapangua hiyo imewagusa pia wakuu wa vikosi, wakuu wa polisi wa vituo (OCS) na polisi wa vyeo cha chini.
Akizungumza na Mwananchi jana, msemaji wa polisi, Advera Bulimba alisema: “Mabadiliko hayo ni ya kawaida ya ndani, hayana uhusiano na kasi ya Rais John Magufuli ila kazi lazima ifanyike.”
Mabadiliko hayo yamekuja ikiwa ni siku chache baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kukutana na maofisa wa polisi kwenye Bwalo la Maofisa wa jeshi hilo Oysterbay jijini Dar es Salaam na kati ya mambo yaliyotajwa ni kukumbushana utendaji, uwajibikaji na mpango wa kulifumua jeshi hilo.























