Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, January 9, 2014

Askari wanyamapori avunjika mguu akiwakabili majangili

Askari wa wanyamapori katika pori la akiba Ugalla, mkoani Tabora, amejeruhiwa vibaya akiwa na wenzake wakikabiliana na majangili. Meneja wa pori hilo, Japhary Lyimo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo jana. Lyimo alifafanua kuwa tukio hilo lilitokea wakati timu ya askari kutoka pori hilo, askari kutoka kikosi maalum cha kupambana na ujangili (KDU), askari wanakijiji wanaozunguka pori hilo (VGS) na wale wa kampuni ya uwindaji wa kitalii ya Game Frontiers ambao wanamiliki vitalu viwili vya uwindaji vya Ugunda na Ugalla vilivyoko kwenye pori hilo wakiwa katika doria.


TUNAOMBA BOFYA HAPA NA ULIKE PAGE YETU KWA HABARI NYINGI ZA KILA SIKU,(USIPITWEEEEEEEE)
“Askari wetu Richard Temu, amevunjika mguu wake wa kushoto baada ya kuteleza na kutumbukia mtaroni wakati wakifukuzana na majangili,” alifafanua Meneja huyo kwa njia ya simu.
Alisema siku moja kabla ya tukio hilo, walisikia milio ya risasi kwenye eneo la hifadhi, na hivyo kuamua kufanya msako.
Aliongeza kuwa kampuni ya uwindaji ya Game Frontiers, ilitoa magari kusaidia usafiri ikiwa ni pamoja na askari wake ambao hata hivyo, wao hawaruhusiwi kubeba silaha za moto.
“Pori letu linapakana na makazi ya wakimbizi ya Katumba, na taarifa tulizo nazo wengi wa majangili hujipanga kutokea huko kwa vile wana silaha nzito," alisema.
Alifafanua kuwa askari Temu aliyejeruhiwa, alikuwa na wenzake watano, ambapo yeye alikuwa nyuma yao na kutokana na mvua zinazonyesha hivi sasa, aliteleza na kutumbukia mtaroni na kuvunjika mguu.
"Tunawashukuru wenzetu wa Game Frontiers kwa msaada wao waliotupatia wa kumsafirisha kwa ndege hadi Dar es Salaam na sasa anatibiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili Taasisi ya Mifupa," alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Game Frontiers, Muhsin Abdallah Sheni, alisema askari wake walikuwa wakishirikiana na wale wa Idara ya Wanyamapori, KDU na VGS kuwasaka majangili hao na kampuni yake kama wadau wakuu kwenye sekta ya wanyama pori na uhifadhi wa wanyama, waliona wanao wajibu mkubwa wa kushirikiana nao katika kuwasaka majangili hao.
“Sisi tuna vitalu vya uwindaji kwenye pori hili, majangili wametuvamia, kwa hali hiyo hatuwezi kukaa chini tu na kusubiri, ndiyo maana tulijitolea magari na vifaa vingine ili kuongeza nguvu kukabiliana na wahalifu hao.
Aidha, Meneja wa pori hilo, Lyimo, ametoa wito kwa wanakijiji wanaoishi kuzunguka hifadhi hiyo, kuendelea kutoa ushirikiano kwa Idara ya Wanyamapori kwa kuwa walinzi namba moja kwani uhifadhi wa wanyamapori ni faida kwao kutokana na mapato yatokanayo na uwapo wa wanyama hao.
“Kwa mfano, asilimia 25 ya mapato yanayotokana na uwindaji wa kitalii huenda moja kwa moja kwenye halmashauri na kwa maana nyingine huwasaidia wanakijiji katika maeneo ya afya na elimu,” alifafanua.
Wiki iliyopita, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alifanya ziara kwenye mapori ya akiba Selous na Maswa, ili kuwapa moyo askari wa wanyamapori kutokana na mazingira magumu wanayokabiliana nayo katika kuwatunza wanyamapori.
Nyalandu alisema serikali inaandaa utaratibu wa kupeleka muswada bungeni ili kuanzisha Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania ambayo itakuwa inajitegemea.
Kwa sasa, askari wa wanyamapori wote wako chini ya Idara ya Wanyamapori, Wizara ya Maliasili na Utalii na utaratibu wa ajira hufuata misingi ya utumishi wa umma. Aidha, Nyalandu alisema kwa sasa Idara ya Wanyamapori ina upungufu wa askari 4,700. 

SOURCE: NIPASHE

No comments:

Post a Comment