Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, February 12, 2014

RC Geita aleta kizaazaa



Wamiliki wa Kampuni za Kusambaza Mbegu za Pamba na Dawa za kuua wadudu Kanda ya Ziwa, wamekamatwa na polisi ndani ya mkutano wa kawaida wa wadau wa bodi ya pamba, uliofanyika jana katika ukumbi wa halmashauri wilayani hapa mkoani Geita kwa tuhuma za kuhujumu zao hilo.
Hatua hiyo imekuja kutokana na agizo la Mwenyekiti wa Bodi ya Pamba ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa, Saidi Magalula kwa kile alichodai wamiliki hao wamekiuka agizo la Serikali walilokubaliana kuwakopesha wakulima dawa za kuua wadudu, jambo lililomlazimu kuita polisi na kuwakamata wakati mkutano huo ukiendelea.
“Msitufanye sisi wajinga, tumekaa vikao vingi hapa tukakubaliana kwamba mkawakopeshe wakulima dawa na mbegu, badala yake mkakataa na kuanza kuwauzia, DC naomba umwite OCD wakatoe maelezo polisi,” alisema Magalula.
Wamiliki hao waliingia mkataba na Serikali Octoba mwaka jana kwa makubaliano na Bodi ya Pamba kwamba iwakopeshe wamiliki hao mbegu na dawa na kisha kampuni hizo zikatoe mikopo kwa wakulima kwa lengo la kuinua uzalishaji wa zao hilo lakini badala yake kampuni hizo zilikopeshwa mbegu na bodi lakini wao wakaenda kuwauzia wakulima.
“Sisi tuliwakopesha dawa na mbegu na tukakubaliana mtaenda kuwakopesha wakulima, lakini nyie mkafanya biashara na pesa mkaweka mifukoni, huo ni wizi wa mchana kweupe na sisi hatutawanyamazia, naomba mkatoe maelezo polisi, OCD kamata hao peleka polisi,” alisema Magalula.
Aidha wakizungumza kwa nyakati tofauti kabla hawajakamatwa wakati wakihojiwa na viongozi wa bodi kama wanataka ama hawataki kuwakopesha wakulima, walikana kuwa wao hawajakataa kuwakopesha wakulima isipokuwa wakulima ndiyo walikataa kukopa .
“Sisi hatujakataa kuwakopesha wakulima wenyewe ndiyo hawakuwa tayari kukopa,” alisema Wiliam Matonange Meneja wa Kampuni ya Kahama Oil Mills Limited .
Aidha Magalula alisema, wakulima hawajakataa kukopeshwa na taarifa zote wanazo kwamba kampuni hizo ndizo zilikataa kuwakopesha licha ya kuwa wao walikopeshwa na bodi.
“Msitupotezee muda kama hamtaki mseme hatutaki, nyie kama watu wazima mmeniudhi sana, hivyo sitaki maelezo mkatoe polisi,” alisema Magalula.
Baadhi ya kampuni zinazodaiwa kushindwa kukopesha wakulima hao ni pamoja na Kahama Cooperative Union (KAW) LTD, Kahama Oil Mills Ltd na Fresho Inuco Ltd. Chanzo;Mwananchi

No comments:

Post a Comment