Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, February 8, 2014

WanaCUF watakiwa kutovunjika moyo na matokeo ya uchaguzi mdogo jimbo la Kiembesamaki


Na Khamis Haji , OMKR
Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF, Maalim Seif Sharif Hamad amewataka wanachama na viongozi wa chama hicho wasivunjike moyo na matokeo ya uchaguzi mdogo wa jimbo la Kiembesamaki na badala yake waendelee na juhudi za kukiimarisha chama, ili kiweze kukamata dola katika uchaguzi mkuu wa mwakani.Akifungua mkutano wa viongozi wa matawi, majimbo na Wilaya kwa Wilaya za Wete na Micheweni uliofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete, Maalim Seif amesema kilichotangazwa Kiembesamaki si matakwa ya wananchi, kwa vile  kimsingi wananchi wa jimbo hilo walisusia uchaguzi huo.
Maalim Seif amesema idadi kubwa ya wapiga kura walioshiriki katika uchaguzi huo si wakaazi wa eneo hilo, ambao walichukuliwa katika maeneo mbali mbali, baada ya kubainika wananchi wenyewe hawatashiriki kwa sababu hawakuridhishwa na maamuzi yaliyochukuliwa hadi kufanyika uchaguzi huo.
“Kama kuna wananchi wa Kiembesamaki waliokwenda kupiga kura basi hawazidi 1000, wengi walichukuliwa katika maeneo tafauti, kama vile Makunduchi, Mtende, Kitope na Bumbwini na wakapelekwa kupiga kura huku wakilindwa na vikosi vya Serikali”, alisema Maalim Seif.
Amesema mbali na hayo kuna baadhi ya wananchi wa Kiembesamaki walipewa vitisho kabla ya kufanyika uchaguzi huo, kwa kutumiwa ujumbe unaowaonya wasijitokeze kwenda kupiga kura, vyenginevyo watapatwa na matatizo makubwa.
Katika uchaguzi huo mdogo wa Kiembesamaki ambao uliofanyika Februari 2, mwaka huu, baada ya aliyekuwa Mwakilishi wa jimbo hilo, Mansour Yussuf Himid kutimuliwa uanachama wa CCM, mgombea wa CCM, Mahmoud Thabit Kombo alitangazwa mshindi, ambapo vile vile idadi kubwa ya wapiga kura hawakujitokeza kwenda kupiga kura.
Akizungumzia Katiba Mpya, Maalim Seif amewahimiza wajumbe wa Bunge la Katiba kuweka kando maslahi ya vyama au makundi yao, na badala yake wahakikishe Tanzania inakuwa na Muungano wa haki, ambapo Wazanzibari na Watanganyika kila upande uridhike kuwa unapata haki sawa na mwengine.
“Kwa upande wetu Wazanzibari tusisahau tuna kilio kikubwa cha miaka mingi kutotendewa haki ndani ya Muungano huu, wajumbe wote wajali maslahi ya Zanzibar na waweke pembeni maslahi binafsi au ya vyama vyao”, alionya Maalim Seif.
Kuhusu uchaguzi mkuu unaoendelea ndani ya CUF, Katibu Mkuu huyo amesema kwa wale viongozi ambao tayari wamechaguliwa katika ngazi za matawi na Majimbo wajiepushe na tabia ya kuwatenga wale ambao hawakushinda, na wafanyekazi kwa pamoja kwa ajili ya kukiimarisha zaidi chama.
Amesema kitendo cha kuwatenga walioshindwa katika shughuli za kichama itakuwa ni dhambi kubwa ambayo itasababisha mifarakano na kupelekea hata hao walioshinda wasiweze kufanya kazi kwa ufanisi na matokeo yake ni kudhorota ufanisi katika utekelezaji wa malengo ya chama.
Mapema, Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Hamad Masoud akizungumza katika mkutano huo amesema matumaini ya ushindi wa chama hicho yapo kwa viongozi hao wapya, hivyo wajipange vizuri na wadumishe mashirikiano ya hali ya juu na hatimaye wakipe ushindi chama chao

No comments:

Post a Comment