Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, March 1, 2014

ANELKA AFUNGIWA MECHI 5, FAINI £80,000!!


KUFUATIA kusikilizwa kwa Siku mbili Kesi ya Mchezaji wa West Bromwich Albion, Nicholas Anelka, Tume Huru ya FA, Chama cha Soka England, imempata na Hatia kwa kutumia ishara ya Saluti ambayo inahusishwa na Ubaguzi wa Mafashisti wa Nazi. 

Anelka amepewa Adhabu ya kufungiwa Mechi 5 na kumpiga Faini £80,000 kwa kutumia Saluti hiyo inayoitwa 'Quenelle'. 
Pamoja na Adhabu hizo, pia Straika huyo kutoka Ufaransa ametakiwa kuhudhuria Elimu ya Lazima. 
Anelka, mwenye Miaka 34, alikana kwamba 'Quenelle' ni ya Kibaguzi na kudai Saluti hiyo ni kupinga Serikali. 
Mara baada ya Adhabu hizo za FA, Klabu yake, West Brom, imeamua kumsimamisha hadi hapo Rufaa yake na Uchunguzi ndani ya Klabu kukamilika. 
Hata hivyo, Adhabu zake zitasimamishwa ikiwa ataamua kukata Rufaa. 
Anelka atapewa Siku 7 tangu atakapopata kwa Maandishi sababu za kuadhibiwa kwake za kukata Rufaa ikiwa atapenda. 

Mbali ya Adhabu zake, Anelka pia ametakiwa kulipa Gharama za Uendeshwaji wa Kesi yake. 
Sakata la Anelka lilianza Desemba 28 wakati akishangilia Goli lake Timu yake, West Bromwich Albion, ilipotoka Sare 3-3 na West Ham, kwa kutumia ishara ya Saluti ambayo inahusishwa na Mafashisti wa Nazi. 
Saluti hiyo [Pichani] ambayo Mkono wake wa kushoto aliupitisha Kifuani na Mkono wa Kulia kuelekezwa chini huchukuliwa kama Saluti ya Nazi kwa kinyume lakini mwenyewe Anelka amekiri hiyo inaitwa ‘Quenelle’ ili kumsapoti Rafiki yake wa France, Dieudonné M'Bala M'Bala, ambae ni Mchekeshaji, anaesakamwa Nchini humo kwa kuwa Mbaguzi. 
Saluti hiyo ya Anelka imezua kizaazaa kikubwa huko Ufaransa kiasi ambacho Waziri wa Michezo Nchini humo, Valérie Fourneyron, amesema inatia kinyaa. 
Anelka alitumia hiyo ‘Quenelle’ akisheherekea Bao lake la Kwanza kati ya mawili iliyofunga kwenye Sare hiyo ya 3-3 kati ya Timu yake West Brom na West Ham na hilo likiwa Bao lake la Kwanza kwa Klabu hiyo tangu ajiunge nayo mwanzoni mwa Msimu. 
Lakini Anelka si Mwanasoka wa kwanza kupigwa Picha akitoa hiyo ‘Quenelle’ kwani Samir Nasri wa Manchester City na Mamadou Sakho wa Liverpool walishanaswa wakiwa pamoja na Dieudonné wakitoa Saluti hiyo ingawa Sakho baadae alisisitiza hakujua maana yake na alihadaiwa kuitumia.
 
MECHI ATAKAZOZIKOSA ANELKA:
-Manchester United (home) March 8
-Swansea (away) March 15
-Hull (away) March 22
-Cardiff (home) March 29
-Norwich (away) April 5

No comments:

Post a Comment