Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, April 10, 2015

Chadema Moro kuandamana kumuunga mkono Abood


Mbunge wa Jimbo la Morogoro, Abdulaziz Abood.
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Morogoro, kimetangaza kufanya   maandamano makubwa kwenda kwa uongozi wa Manispaa ya Morogoro, kushinikiza kutekelezwa kauli ya Mbunge wa Jimbo la Morogoro, Abdulaziz Abood (pichani) (CCM) ya kutaka kutolewa taarifa ya matumizi ya Sh. milioni 720 za mradi mkubwa wa ujenzi wa stendi ya mabasi  yaendayo mikoani eneo la Msamvu.

Pamoja na fedha hizo, pia Chadema inataka maelezo mengine kutoka kwa Uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro akiwamo Meya na Mkurugenzi kuhusu fedha za miradi ya  ujenzi  wa soko kuu la Morogoro .
Hatua ya Chadema kuamua kufanya maandamano hayo imekuja siku chache baada ya  Abood kufanya ziara ya kukagua mradi huo na kunyimwa taarifa za matumizi ya fedha ungozi wa manispaa, hivyo kulazimika  kuahirisha ziara hiyo, huku akitoa  siku 14 taarifa hiyo itolewe vinginevyo suala hilo atalifikisha kwa Rais Jakaya Kikwete.
Hata hivyo, uongozi wa Manispaa ya Morogoro kupitia Meya wake, Amir Nondo ukizungumzia suala hilo kwa waandishi wa habari, ulieleza kuwa ujenzi wa mradi unafanywa kwa ubia na Mfuko wa Pensheni wa Serikali za Mitaa (LAPF) ambao ndiyo wanawajibika na fedha hizo Sh. milioni 720  walizitoa kwa ajili ya fidia ya kumlipa mtu aliyekuwa ndani ya eneo hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa jana, Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Morogoro, alisema wanakusudia kufanya maandamano hayo Aprili 14 mwaka huu kwenda ofisi hiyo ya mkurugenzi wa manispaa na meya kutaka matumizi ya fedha za mradi huo wa stendi yawekwe wazi.
Alisema katika mradi huo wa ujenzi wa stendi ya kisasa kuna harufu ya ufisadi unaofanywa na baadhi ya viongozi wa manispaa ndiyo maana wanakataa kutoa taarifa zake kwa mbunge.
“Yule ni mbunge anapaswa kujua maendeleo ya ujenzi sasa tunashangaa kwanini wanamnyima taarifa za mradi ambao ni sehemu ya fedha za serikali, kama hakuna ufisadi wanaficha nini?. Sasa sisi tutafanya mandamano ya kumuunga mkono Abood ili wananchi wapewe taarifa za mradi huo na maendeleo yake,” alisema.
Mwenyekiti wa Chadema  alilitaadhalisha Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro kuwa lisithubutu kuyazuia maandamano hayo ya amani, kwani hawatakubali kuzuiliwa kwa kuwa hizo ni fedha za wananchi ambao wengi wao wanashindwa kupata huduma nyingine kama za afya kutokana na mradi huo.
Mradi wa stendi ya kisasa ya mabasi yaendayo mikoani ya Msamvu unatalajiwa kutumia Sh. bilioni 10 katika awamu ya kwanza.

No comments:

Post a Comment