Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, May 21, 2015

PART III YA ADEBAYOR: KAKA ZANGU WALINIWEKEA KISU SHINGONI KISA FEDHA NA NIMEJARIBU MARA KADHAA KUTAKA KUJIUA


Emmanuel Adebayor katika pozi na kaka yake. Picha hii ameiweka Facebook.
STRAIKA wa Tottenham Hotspur, Emmanuel Adebayor ametoa sehemu ya tatu ya historia yake ambapo ameeleza mambo mengi mazito aliyoyapitia maishani mwake.

Emmanuel Adebayor akiwaTottenham Hotspur.
Staa huyo mwenye miaka 31 raia wa Togo ameweka wazi kuwa mara kaka zake wawili Kola na Peter waliwahi kumwekea kisu shingoni wakitaka awapatie fedha.
Katika sehemu hii ya tatu, Adebayor pia ameeleza mabavyo mara kadhaa amewahi kufanya majaribio ya kutaka kujiua kutokana na kukata tamaa.

Isome historia hiyo aliyoiweka katika Ukurasa wake wa Facebook kama ambavyo alifanya kwa Part I na II:


NINAPOAMUA kuleta kwenu sehemu ya tatu ‘Part III’ leo, ni kwa sababu kaka yangu @Kola Adebayor na kaka zangu wengine pamoja na dada zangu wameamua kuongelea mambo ya familia yetu kupitia mitandao ya kijamii, barua kwa klabu nilizocheza, redioni… Ningeweza kuandika simulizi ya maisha yangu na kuiuza ila nimeona ni bora kuiweka hadharani na nyinyi muisome.


Picha hii iliwekwa Facebook na Adebayor katika sehemu ya kwanza ya historia yake.
Miaka 25 iliyopita, kaka yangu mkubwa aitwaye Kola alikwenda nchini Ujerumani na kuwa tumaini la familia yetu. Kila mmoja wetu alidhani kuwa Kola angeweza kubadili hali ya maisha yetu tuliyokuwa tukiishi.
Miaka kadhaa baada ya kuondoka Togo, tulikuwa bado hatujapata umeme na kulikuwa hakuna simu.
Kola alipohitaji kuwasiliana na sisi alilazimika kupiga simu kwenye Hoteli ya Atlantic iliyokuwa karibu na nyumbani ambapo tuliweza kukimbia hadi hotelini hapo kwa ajili ya kuongea naye.

Nilipopata fursa ya kwenda kucheza soka nchini Ufaransa kwa mara ya kwanza, tulihitaji fedha kwa ajili ya tiketi za ndege na matumizi mengine. Kaka yangu huyo hakuweza kupatikana popote. Mungu tu ndiye anajua alichokuwa anafanya huko Ujerumani.
Nilipofika nchini Ufaransa, nilikamilisha mipango yangu yote na timu yangu na waliniruhusu kuendelea kubaki katika kituo cha soka cha klabu hiyo.
Miezi michache baadaye, kaka yangu alitaka kuja kunitembelea. Kipindi hicho nilikuwa naanza kuishiwa fedha nilizokuwa nazo na nilikuwa bado naishi kwenye kituo hicho. Ilinilazimu kukopa fedha kwa ajili ya kumlipia hotelini.

Kipindi hicho, mchezaji mwenzangu Sega N’diaye kutoka Cameroon aliyekuwa na roho ya huruma aliweza kunikopesha kiasi fulani cha fedha.
Mbali na hizo pia ilinilazimu kukopa fedha nyingine zaidi maana ilibidi nimpatie kaka yangu hata fedha ya nauli ya kurudi Ujerumani. Na kumbukuka bado ni kaka yangu mkubwa.


Picha hii iliwekwa Facebook na Adebayor katika sehemu ya pili ya historia yake.
Miaka mingine baadaye,mambo yalianza kuwa mazuri. Namshukuru Mungu, nilisaini mkataba na Metz.
Kutokea hapo, kaka yangu alikuwa ananipigia simu muda wa kulipia bili zake na wakati mwingine alikuwa akiniambia kuwa kijana wake anaumwa… yote hayo ilibidi niyakabili.

Kwa mara nyigine nilipata bahati baada ya kupata ofa kutoka Monaco na nikasaini kujiunga na klabu hiyo ya Ufaransa.
Siku moja Kola na marehemu kaka yangu Peter Adebayor walikuja kunitembelea Monaco. Kaka zangu hao hawakuniambia kama walikuwa wanakuja Monaco.

Kuna msemo mmoja usemao “Damu ni nzito kuliko maji” hivyo niliwapokea. Walifika mapema asubuhi na wakati huo nilikuwa naelekea katika mazoezi.
Niliporudi nyumbani, tulikuwa na mazungumzo na walikuwa wakitaka kuanza biashara ya magari.

Ni wazi kuwa biashara hiyo ilihitaji fedha nyingi. Niliwaambia kuwa ningewasaidia mara tu baada ya kupokea mshahara wangu ujao.
Kwa muda huo, Thierry Mangwa alikuwa anaishi katika ‘apartment’ yangu nilipokuwa naishi maana alikuwa akipambana na baadhi ya changamoto zake binafsi na alihitaji sehemu ya kuishi.

Siku moja, nilirejea kutoka katika mazoezi na nikamkuta akilia. Hakunieleza kwa nini alikuwa analia. Hata kaka zangu hawakuniambia sababu ya yeye kulia.
Siku iliyofuata, mmoja wa marafiki zangu aitwaye Padjoe alikuja kunitembelea na wakati akiondoka nyumbani kwangu nakumbuka nilimpatia kama €500 sawa na shilingi milioni 1.1 za Tanzania.

Adebayor katika pozi na mama yake mzazi.
Kaka yangu Kola aliniona nikimpatia fedha hizo na akaonekana kusikitika sana.
Alikuwa akitaka kujua ni kwa nini nilimpatia rafiki yangu fedha hizo na si kumpa yeye. Jibu langu lilikuwa jepesi maana kiasi ambacho Kola alikuwa akikihitaji kilikuwa kikubwa ambacho sikuwa nacho hapo nyumbani. Tuliendelea kubishana kuhusu suala hilo.

Siku iliyofuata baada ya mazoezi… Nilikuwa nimechoka sana na niliamua kwenda kupiga picha. Nilipoamka nilikutana na kisu kikiwa kwenye koromeo langu baada ya kufumbua macho yangu.
Kaka zangu wote walikuwepo. Walikuwa wakipiga kelele na kuniambia kuwa nilikuwa nawapotezea muda.

Peter alikuwa ameshika kisu huku Kola akiunga mkono. Niliwauliza: “Hiyo ndiyo njia sahii ya kutatua tatizo lao? Kama ndiyo, basi niueni na mchukue fedha hizo”. Baada ya maneno hayo ndipo walipoweka kisu chini. Na baada ya tukio hilo, nilifanikiwa kutoka katika nyumba na kuwapigia simu wazazi wangu.
Mama yangu mzazi alinishauri niwapigie simu polisi. Na hiyo ndiyo ilikuwa salama yangu kurejea ndani ya nyumba yangu. …Nilikuwa na mazoezi siku iliyofuata. Hivyo ilinilazimu kufanya kama mama alivyonishauri. Polisi walifika na kutulia vurugu zilizokuwa zimetokea.
Kwa mara nyingine tena, “damu ni nzito kuliko maji”, hivyo niliamua kuyamaliza.
Baada ya siku chache, Peter alikwenda kumtembelea mmoja wa marafiki wa Kola jijini Paris. Hivyo nilibaki nyumbani na Kola; Kwa usalama wangu, nilitumia kila njia kupata fedha ili nimpatie haraka iwezekanavyo. Mungu tu ndiye anayejua kiasi gani nilimpatia siku hiyo.

Miezi michache baada ya sakata hilo, nilikwenda nyumbani Togo na nilishangaa pale mama yangu alipoanza kunihoji ni kwa nini niliwaitia polisi kaka zangu, aliendelea kusema kuwa mimi ni mtu mbaya katika familia.
Na hii ni mojawapo ya stori ambazo nimeziweka kwa ajili ya baadaye…..

Kila mara nilipokuwa nakwenda Togo, kila mmoja alikuwa ananiuliza kwa nini kaka zangu walikuwa hawanitembelei kwa miaka hiyo yote.
Kwa haraka, nilifanya mipango na kuandaa safari kwa ajili ya kaka yangu na alikuja kunitembelea mimi na familia yangu kwa gharama zangu.


Adebayor akiichezea timu yake ya Taifa ya Togo.
Aprili 22, 2005, tulipokea taarifa mbaya. Nilipigiwa simu na kuambiwa kuwa baba yangu mzazi amefariki. Nilipatwa na ukiwa. Nilimpigia kaka yangu mkubwa na kumueleza kuwa wote inatupasa kwenda msibani. Kwa mara nyingine niliandaa tiketi ya ndege kwa ajili yake. Tulikwenda wote Togo na niligharamia kila kitu.
Zamani kabla ya baba yangu kufariki, akiwa hospitalini siku moja aliniambia kuwa nijitahidi niwezavyo siku akifariki msiba wake usiwe wa huzuni.
Alitaka tusherehekee maisha yake. Namuachia Mola kuamua kama mazishi niliyoyaandaa kwa ajili ya baba yalikuwa kama aliyoyataka.

Mwanaume anayejiita “big man” katika familia yetu hakuchangia chochote. Badala yake bado amekuwa na ujasiri wa kusema kuwa siijali familia yetu.
Mwaka 2006, nilipata tena fursa kubwa ya kwenda kucheza soka katika Klabu ya Arsenal. Kuanzia hapo, ndugu zangu walianza kutoa milolongo ya shutuma za uongo dhidi yangu.


Adebayor akiwa Manchester City.
Julai 22, 2013 habari nyingine mbaya ziliikumba familia yetu. Kaka yangu Peter Adebayor aliaga dunia. Msiba wake ulikuwa wa kusikitisha na uliniathiri. Kitu cha pekee ambacho bado nashindwa kukihimili hadi leo ni tuhuma zinazotolewa na Kola kuwa nahusika na kifo cha Peter.
Anasema duka nililomfungulia Peter halikuwa zuri. Amekuwa akituma ujumbe akisema kuwa kazi yangu itavurugika.
Nilimfanyia Peter kila niwezalo wakati akiwa hai, Nilikwenda Metz na Monaco nikiwa pamoja naye.
Ni kitu gani Kola anaweza kueleza alichomfanyia Peter?

Hakuna. Mtu huyo hakuonekana hata msibani mbali na fedha nilizomtumia kwa ajili ya safari ya kuja msibani.
Anasema pia kuwa nilisababisha mama yangu kuugua, ila anasahau kuwa kipindi yupo Ujerumani, nilikuwa mimi peke yangu niliyekuwa upande wa mama. Na mara tu baada ya kuanza kutengeneza maisha kupitia soka, nilifanya kila ambacho mtu anafikiria kwa ajili ya mama yake. Hilo ni jambo la kawaida.


Adebayor akiwa Real Madrid.
Ila kaka yangu kamwe halidhiki. Alisema kuwa nilimnunulia mama gari lisilo na hadhi.
Kwa nini yeye hakumnunulia la kifahari? Kitu ambacho namtaka afanye ni kutimiza wajibu wake.
Maana kama sifanyi vitu sahii basi yeye inabidi aonyeshe mfano kama kaka mkubwa.

Ameishi Ujerumani kwa zaidi ya miaka 20, lakini hajawahi hata siku moja kumpeleka mama kutembea eneo hilo.
Hata kurudi nyumbani kutembea imekuwa ni shida. Kitu anachopigia kelele ni kwamba baba yetu alisema nijenge nyumba kwa kila mmoja wao.
Sina kumbukumbu kama marehemu baba aliwahi kusema kitu hicho.

Je, jambo hilo linaleta maana kwake au kwa mtu mwingine yeyote? Kama kaka mkubwa, anatakiwa kuwa anafanya yale yote ninayoyafanya mimi kwa familia. Anatakiwa kuacha kujificha na kujitokeza kubeba majukumu yake.
Alipokuja Ulaya, alikuwa kijana mdogo na angeweza kuwa mcheza soka mzuri pia.


Adebayor alipokuwa Arsenal.
Tuyaache hayo, baadhi ya watu hapa ni madereva lakini wanamudu kuzitunza familia zao. Wanaweza hata kuwaleta wazazi wao na wanafamilia huku. Kwa nini yeye hajafanya hivyo ila amekuwa mtu wa kuongea tu? 
Kama ni hivyo basi angemleta angalau Rotimi, Bidemi au mtoto wake wa kiume Aziz huku kabla ya kuanza kuongelea kuhusu kuitunza familia. Matendo huongea zaidi kuliko maneno.
Watu wengi wanasema kuwa sikuwahi kwenda shule, ila wanasahau kuwa ni kwa sababu hatukuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Sijawahi kuwalaumu wazazi wangu kuhusiana na hilo. Ila namshukuru Mungu , leo nina uwezo wa kuongea lugha zaidi ya tatu na nina uwezo wa kumpeleka binti yangu shule. Najivuia kwa hilo.
Watu wanaweza kunihukumu kwa kutokwenda shule, ila mwishoni ni kwamba kinachoangaliwa ni wewe ni mtu wa aina gani na nini unaweza kujifunza mwenyewe. Pia ni maisha gani yanakufunza nini na nini unajifunza kutokana na maisha hayo.

Adebayor akiwa Monaco.
Mara nyingi nilitaka kukata tamaa. Muulize dada yangu Iyabo Adebayor mara ngapi nimempigia simu nikitaka kujiua na yeye kunishauri nisifanye hivyo? Nimehifadhi stori hizi kwa miaka mingi…Iwapo ningefariki, hakuna mtu ambaye angejua kuhusu historia yangu, hakuna ambaye angejifunza….
Baadhi ya watu wamekuwa wakiniambia kuwa historia hizi niziache zibaki kuwa siri, ila mtu inabidi ajitoe sadaka mwenyewe; mtu inabidi aongelee kuhusu historia hii. Ninajua watu watalinganisha kuhusu historia yangu huku wengine wakijifunza kutoka kwangu.
Kwa kila mmoja anayenijua mimi, Nitafanya kila niwezalo kwa ajili ya nchi yangu na watu wangu.
Ujumbe wa mwisho kutoka kwa kaka mdogo kwenda kwa kaka mkubwa: Acha kuvuta sigara na acha kunywa pombe. Hiyo ndiyo historia yangu!

No comments:

Post a Comment