Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, June 9, 2015

Dk.Slaa Asaka Ubani wa Urais Ulaya


WAKATI vuguvugu la kusaka mgombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) likishika kasi, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa, ameondoka kwenda barani Ulaya kusaka ubani wa urais kwa muda wa siku nane.
 
Dk. Slaa ambaye amekuwa akitajwa kuwa anaweza kuteuliwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kugombea urais Oktoba mwaka huu kutokana na rekodi yake, anafanya ziara hii ikiwa ni ya pili baada ya ziara ndefu aliyoifanya hivi karibu nchini Marekani.
 
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana na Mkuu wa Idara ya Mambo ya Nje  na Uhusiano wa Kimataifa,Deogratias Munishi, ilisema Dk. Slaa ataanzia nchini Uholanzi ambako atakutana na viongozi wa Jumuiya ya Ulaya (EU) ambapo watazungumzia mambo mbalimbali yakiwamo ya kisiasa.

“Akiwa Uholanzi anatarajiwa kukutana na kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali wa nchi za Jumuiya ya Ulaya (EU), atakutana na jopo la wataalamu wa masuala ya uchumi kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika kupata mifumo sahihi na kujenga taasisi za kusaidia uwajibikaji.
 
“Pia tunaamini mazungumzo haya yatajikita zaidi kutoa mwelekeo wa  kusukuma maendeleo ya watu katika nchi za Afrika, hususan zenye rasilimali nyingi kama Tanzania ili kuziepusha na kile ambacho kimezikumba nchi nyingi duniani,” ilisema taarifa hiyo.
 
Taarifa hiyo, ilisema Dk. Slaa pia atajadiliana kuhusu hali ya demokrasia, utawala bora na ukuzaji wa haki za binadamu.
 
Ilisema Dk. Slaa ameambatana na Mkurugenzi wa Bunge na Halmashauri, John Mrema na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano, Tumaini Makene.
 
Kabla ya ziara hiyo, Dk. Slaa ametoka kufanya ziara ya kikazi katika mikoa ya Kagera, Mbeya, Rukwa na Katavi akikagua uandikishaji wapigakura kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa mfumo wa BVR huku pia akiwahamasisha Watanzania wote wenye sifa za kupiga kura kuhakikisha wamejiandikisha.

No comments:

Post a Comment