Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, August 25, 2015

WASIOONA WATISHIA KUTOMPIGIA KURA MWANASIASA AMBAYE HAJAWAWEKEA MAZINGIRA RAFIKI YA WAO KUPIGA KURA WAKATI WA UCHAGUZI MKUU

 Mwenyekiti wa Chama cha Wasioona Tanzania (TLB), Luis Benedicto (katikati), akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam , kuhusu wasiona kutengwa katika mchakato mzima wa uchaguzi kuanzia kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa chama hicho, Jonas Lubago na Katibu Mkuu wa TLB, Emmanuel Simon
 Wanahabari wakichukua taarifa hiyo.

 
Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali wakiwa katika mkutano huo.

Na Dotto Mwaibale

CHAMA cha Wasioona Tanzania (TLB), kimetishia kutompa kura mgombea urais au mwanasiasa yeyote kupitia chama chochote cha siasa ambaye hajaandaa mazingira wezeshi na rafiki kwa ajiri ya kundi hilo kupiga kura.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Luis Benedicto wakati akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam , kuhusu wasiona kutengwa katika mchakato mzima wa uchaguzi kuanzia kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura.

"Ndugu wanahabari kundi la sisi watu tusioona tumetengwa katika mchakato mzima kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015 wa kuchagua rais, wabunge na madiwani kuanzia kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura" alisema Benedicto.

Alisema mambo ya msingi kuhusu mchakato mzima wa uchaguzi mwaka huu hayajatazamwa wala kuzungumziwa ama na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) au vyama vya siasa nchini.

Alisema zipo changamoto nyingi ambazo zinajidhihirisha hasa wakati huu wa uchaguzi mkuu ambazo kwa vyovyote vile zinawanyima fursa na haki ya kupiga kura kama watu wasiona ambao ni sehemu ya jamii.

Benedicto alisema kwamba baadhi yao walihamasishana kadri walivyoweza kujiandikisha katika daftari hilo ambapo walikumbana na changamoto luluki.

Alitaja baadhi ya changamoto walizokumbana nazo kutokana na kutokuona kwao ni hawakutumia alama ya vidole gumba na badala yake walilazimishwa kushika kalamu na kusaidiwa kuweka sahii kwa kusaidiwa na baadhi ya waandikishaji jambo ambalo litaathiri taarifa zao nyingine zilizo katika mfumo waliouzoea wa dole gumba.

Alisema kutokana na kutotendewa haki hiyo wao kama Chama cha Waioona Tanzania (TLB) kwa kauli moja wanatamka hawatawapa kura zao wanasiasa ambao hawajaandaa mazingira hayo wezeshi na rafiki kwa ajili ya wao kupiga kura.

Alisema wanamashaka makubwa kama vyama vya siasa nchini vimeweka katika ilani zao sera au kanuni zinazoelekeza utekelezwaji wa maslahi yao yanayogusa moja kwa moja na changamoto za kimaendeleo wanazokabiliana nazo watu wasiona.

Aliongeza kuwa watu wasiona wana haki ya kushiriki na kuwepo katika vyombo vya maamuzi ndio maana wanaviuliza vyama vya siasa kwamba vina mpango gani wa kuwawezesha katika kushiriki katika majukwaa ya siasa katika kipindi hiki na siku za usoni.

"Tunasikitika kuona hata kanuni ndogo hazijatungwa ili kuwashirikisha watu wasioona katika mchakato, jambo ambalo linatengeneza mazingira ya unyanyapaa ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa gharama kubwa za uchaguzi ambazo walemavu wengi hawazimudu.

Alisema kuwa elimu ya uraia, vifaa vya kupigia kura na miundombinu wezeshi kufika vilipo vituo vya kupigia kura ni vitendawili ambavyo mpaka sasa bado havijapatiwa hivyo kujiona wapo njia panda na hawajui itakuweje.

No comments:

Post a Comment