Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, October 24, 2015

NEWALA WAHAKIKISHIWA USALAMA WA KUTOSHA KWA RAIA NA MALI ZAO SIKU YA UCHAGUZI



Na Father Kidevu Blog
WANANCHI wilayayani Newala wamehakikishiwa usalama wa kutosha siku ya kupiga kura na kutakiwa kujitokeza kupiga kura na kuwachagua viongozi wao bila wasiwasi wowote.

Akizungumza na Habarileo kwa njia ya simu, Mkuu wa Wilaya ya Newala, Christopher Magala amesema wakazi wa Newala husususani katika majimbo ya uchaguzi ya Newala Mjini na Newala vijini wasiwe na hofu juu ya amani siku ya kupiga kura.

“Nitumie nafasi hii kuwatoa hofu wananchi na kuwahakikishia usalama wenu na mali zenu, kwamba siku ya kupiga kura hakutakuwa na vurugu zozote, Hivyo wale wote waliojiandikisha kupiga kura wajitokeze kwa wingi kwenda kupiga kura siku hiyo bila wasiwasi wowote,”alisema Magala.

Magala amesema wananchi waendelea kuilinda na kuitunza amani katika kipindi hiki cha kumalizia kampeni na kipindi chote cha siku ya Uchaguzi na baada ya Uchaguzi pasipo kuvuruga amani na utulivu uliopo Wilayani humo.

“Katika kipindi hiki cha kumalizia kampeni na kipindi chote cha siku ya Uchaguzi na baada ya Uchaguzi, tuendelee kuitunza amani iliyopo katika Wilaya yetu; upendo na mshikikamano tuliona siku zote tuuimarishe zaidi kipindi hiki ili tuvuke salama na kubaki salama baada ya zoezi la uchaguzi kukamilika,”alisema Magala.


Aidha amesema Serikali imejipanga vizuri kuimarisha doria katika kipindi cha  siku za mwisho za kampeni, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.

Magala amesema ni haki ya kila mwananchi aliyejiandikisha kupiga kura kutimiza haki yake ya kumchagua kiongozi anayemtaka katika nafasi ya Urais, Ubunge na Udiwani katika mazingira tulivu yasiyo nafujo na hivyo kuwataka wananchi kufanya hivyo na wakishapiga kura warudi majumbani na kusubiri kutangazwa matokeo.

“Niwatahadharishe, kama wapo, Wananchi wanaokusudia kuvuruga Uchaguzi kwa namna yoyote ile kwamba Serikali haitawavumilia. Hatua stahiki zitachukuliwa dhidi yao. Vyombo vya Ulinzi vyote vipo ‘standby’ kuhakikisha utulivu unakuwepo wakati wa kwenda kupiga kura na baada ya Uchaguzi kukamilika,”alisema Magala.

Magala pia amewaomba wananchi kutoa taarifa kwa viongozi watakaokuwa jirani nao au vyombo vyausalama vitakavyokuwa karibu, pale watakapoona dalili zinazoashiria kuvunjika kwa amani na kuwataka wachague viongozi bora, waadilifu, wachapaka kazi, watakao waletea maendeleo katika maeneo yenu ya Kata na Wilaya yetu ya Newala kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment