Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, November 23, 2015

MAZISHI YA MAWAZO BADO KIZUNGUMKUTI. CHADEMA KUTINGA MAHAKAMAN


Na:George Binagi-GB Pazzo @BMG
Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema kimesitisha shughuli za mazishi ya aliekuwa Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoani Geita marehemu Alphonce Mawazo, baada ya jeshi la polisi Mkoani Mwanza kuzuia zoezi la kuuaga mwili wake lililokuwa limepangwa kufanyika juzi jumamosi Jijini Mwanza. 

Mwenyekiti wa Chama hicho Taifa, Freeman Mbowe alibainisha hayo jana wakati akizungumza na Wanahabari Mkoani Mwanza, ili kutoa msimamo wa Chama baada ya kuwepo kwa mazungumzo baina yake na familia ya marehemu Mawazo. 



Alisema kuwa baada ya mazungumzo hayo, Chadema pamoja na familia ya marehemu Mawazo wamekubaliana kwenda Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza kufungua shauri la kuomba tafsiri ya Kimahakama juu ya zuio hilo la jeshi la polisi kuzuia mwili wa marehemu Mawazo kuagwa Jijini Mwanza kabla ya Kwenda kuzikwa Kijijini kwake Chikobe katika Wilaya ya Busanda Mkoani Geita.

Nae Mchungaji Charles Lugiko ambae ni baba mlezi wa marehemu Mawazo, alisema anasikitishwa na hatua iliyochukuliwa na jeshi la polisi ya kuzuia mwili wa marehemu Mawazo kuagwa Jijini Mwanza ambapo ameeleza kuwa na matumaini makubwa ya kwamba mahakama itatenda haki juu ya suala hilo.

Frederick Sumaye pamoja na Edward Lowasa ambao ni Viongozi Waandamizi wa Chadema, walisema hatua ya jeshi la polisi kuzuia mwili wa Mawazo kuagwa Jijini Mwanza si sawa na kwamba inaweza kuwa chanzo cha uvunjifu wa amani. 

Mwishoni mwa wiki iliyopita, Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza kupitia kwa Kamanda wake Charles Mkumbo, lilizuia zoezi la mwili wa marehemu Mawazo Kuagwa Jijini Mwanza, kwa madai kwamba limepokea taarifa za kiitelejensia za kuwepo baadhi ya vikundi vya watu kutumia mwanya huo kufanya fujo na hivyo kuhatarisha usalama wa raia na mali zao. 

Aidha Kamanda Mkumbo aliitaja sababu nyingine kuwa ni uwepo wa mlipuko wa Ugonjwa wa Kipindupindu Mkoani Mwanza, ambao umesababisha jeshi hilo kutoruhusu mikusanyiko ya aina yoyote inayoweza kusababisha ugonjwa huo kuenea zaidi kwa mjibu wa wataalamu wa afya ambapo lilishauri zoezi la kuaga mwili huo kufanyika Mkoani Geita ambapo mazishi ya marehemu Mawazo yatarajiwa kufanyika.

Katika uchaguzi uliomalizika hivi karibuni, marehemu Alphone Mawazo alikuwa mgombea ubunge Jimbo la Busanda Mkoani Geita kupitia Chadema, akiwa pia ni Mwenyekiti wa chama hicho mkoani humo ambapo aliuawa kikatili kwa kukatwa mapanga na mashoka na watu wasiojulikana jumamosi iliyopita ya Novemba 14 mchana huku kifo chake kikihusishwa na uhasama wa kisiasa.
BONYEZA PLAY HAPA CHINI KUSIKILIZA

No comments:

Post a Comment