Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, December 31, 2015

Waziri akuta ofisi nzima wako likizo

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula amefanya ziara ya kushtukiza Ofisi za Baraza la Ardhi na Nyumba za Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam na kukuta zaidi ya nusu ya watendaji wake wako likizo.

Naibu Waziri huyo aliwasili ofisini hapo jana saa 8.30 mchana na kupokewa na mtunza kumbukumbu, Bahati Kassim ambaye ni mtumishi pekee aliyekuwapo ofisini.

Baada ya kusaini kitabu cha wageni, naibu waziri aliuliza waliko watumishi wengine.
Naibu Waziri: Watumishi wengine wako wapi?
Bahati: Wako likizo na mmoja ametoka kikazi.
Naibu Waziri: Baraza lina watumishi wangapi hapa Kinondoni.
Bahati: Tupo watumishi sita.
Naibu Waziri: Wangapi wako likizo.
Bahati: Wanne, tumebaki wawili, mmoja ambaye ni mwenyekiti ametoka ana kazi za nje.

Baada ya kujibiwa hivyo, Mabura alisema haiwezekani watumishi wanne wakawa likizo kwa wakati mmoja, wakati baraza lina watumishi sita.

 
“Kuna mpangilio mbaya wa likizo, hii ina maana kuna siku ofisi zitafungwa kwa sababu watumishi mtakuwa likizo,” alisema.
Mtunza kumbukumbu pia alimueleza kati ya mwaka 2004 hadi sasa, kuna kesi zaidi ya 2,000 zilizofikishwa mbele ya baraza hilo na kati ya Januari hadi sasa, wamepokea kesi 300.
Awali, Mabula alitembelea kijiji cha King’azi kinachogombewa na wilaya za Kisarawe na Kinondoni ambako aliunda timu ya wataalam watakaochunguza mipaka ya vijiji vya King’azi, Msopwa na Mloganzila ili kubaini viko upande gani.

No comments:

Post a Comment