Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, January 20, 2016

DAR, BAGAMOYO KUKOSA MAJI KWA SIKU MBILI


SHIRIKA LA Majisafi na Majitaka Dar es salaam (DAWASCO), imetangaza kuwapo tatizo la upatikanaji wa huduma ya Maji katika maeneo yote yanayohudumiwa na mtambo wa Ruvu chini ya jiji la Dar es salaam, pamoja na baadhi ya maeneo  ya mji wa Bagamoyo mkoani Pwani kutokana na mtambo huo kuzimwa kwa wastani wa saa 48 kuanzia siku ya Jumamosi 23/01/2016 hadi Jumapili 24/01/2016.

Taarifa ya kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na kaimu meneja uhusiano wa DAWASCO, Bi  Everlasting Lyaro, imeeleza kuwa sababu ya kuzimwa kwa mtambo huo, ni kuruhusu mkandarasi kuunganisha bomba jipya na bomba la zamani katika tanki la Maji wazo-Tegeta, zoezi ambalo linaashiria kukamilika kwa upanuzi wa mtambo wa Ruvu Chini, hivyo kuondoa  tatizo la upatikanaji wa huduma ya Maji katika maeneo yanayohudumiwa na mtambo wa Ruvu chini.


“Tunaelekea kwenye hatua za mwisho za kupokea Maji mengi kutoka mtambo wa Ruvu Chini baada ya kazi ya upanuzi inayoelekea kukamilika mapema mwezi February mwaka huu, na kiasi cha Maji kitaongezeka kutoka wastani wa Lita Milioni 182,000 zinazozalishwa sasa hadi Lita Milioni 270,000. 

Hivyo kuzimwa kwa mtambo huu ni moja ya hatua za mwisho-mwisho katika ukamilishaji wa Mradi wa Ruvu Chini” alisema Lyaro
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, DAWASCO imetoa wito kwa wateja na wananchi wote kuhifadhi Maji ya kutosha na kuyatumia kwa matumizi muhimu ili kukidhi mahitaji husika kwa kipindi hicho chote.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa matengenezo hayo yatasababisha maeneo mengi ya jiji la Dar es salaam kukosa Maji, pamoja na mji wa Bagamoyo vijiji vya Zinga, Kerege na Mapinga, Bunju, Boko, Tegeta, Kunduchi, Salasala, Jangwani,  Mbezi Beach na Kawe.

Maeneo mengine ni Mlalakuwa, Mwenge, Mikocheni, Msasani, Sinza, Kijitonyama, Kinondoni, Oysterbay, Kigogo, Mburahati, Hospitali ya Rufaa Muhimbili, Buguruni, Chang’ombe na Keko

No comments:

Post a Comment