Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, January 11, 2016

KIWIA AONDOA KESI YA KUPINGA MATOKEO YA UBUNGE JIMBO LA ILEMELA BAADA YA KUSHINDWA KULIPA GHARAMA ZA MAHAKAMA

Agrey Laban ambae ni Katibu wa Highness Kiwia akizungumza na Wanahabari nje ya Mahakama.
Na:George Binagi-GB Pazzo @BMG
Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza leo imetupilia mbali kesi ya Kupinga Matokeo ya ubunge katika Jimbo la Ilemela Mkoani Mwanza, iliyofunguliwa na aliekuwa mgombea ubunge katika jimbo hilo kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema Haighness Kiwia.

Katika kesi hiyo ambayo ni namba mbili ya mwaka 2015 iliyofunguliwa Novemba 25 mwaka jana, Kiwia alikuwa akipinga ushindi wa mbunge wa Jimbo la Ilemela Angelina Mabula kupitia Chama cha Mapinduzi CCM kutokana na madai ambayo ni pamoja na kuendesha kampeni za ubaguzi wa kikabila sanjari na kupata kura ambazo hazikuendana na idadi ya wapiga kura walioandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura.

Kesi hiyo imefutwa baada ya Kiwia kupitia kwa mwanasheria wake Paul Kipeja kuiomba Mahakama kufuta kesi hiyo kwa madai ya kwamba mteja wake ameshindwa kulipia gharama za Mahakama ambazo ni Shilingi Milioni 10 na kwamba washtakiwa walikuwa ni Angelina Mabula pamoja na Mwanasheria wa Serikali ambapo gharama ya kufungua kesi hiyo kwa kila mlalamikiwa ilikuwa ni shilingi Milioni Tano.

Kufuatia ombi hilo, Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Eugenia Gerald Rujwauka alitoa maamuzi ya kuifuta kesi hiyo kama ambavyo mlalamikaji alivyoomba.


Baada ya kesi hiyo kufutwa, Mutabanzi Julius Lugaziya ambae ni Mwanasheria Mwandamizi aliekuwa akimtetea mlalamikiwa, amebainisha kuwa baada ya maamuzi hayo anatarajia kukutana na mteja wake ili kujadiliana hatua za kuchukua na huenda akafungua kesi ya madai dhidi ya Kiwia kutokana na kufungua kesi na kisha kuiondoa mwenyewe na hivyo kumuingiza mteja wake katika gharama zisizo za lazima.

Ifahamike kwamba Angelina Mabula pamoja na Highness Kiwia hawakuhudhuria Mahakamani hapo na hakukuwa na wafuasi wengi wa vyama vya siasa kama ilivyozoeleka ambapo nje ya Mahakama hiyo, Agrey Laban ambae ni Katibu wa Kiwia ameilalamikia Mahakama kutokana na kushindwa kupunguza gharama za kesi hiyo jambo ambalo limepelekea haki kupotea.

Wakati hali ikiwa hivyo, Kheri James ambae ni Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Ilemela Angelina Mabula, amepongeza maamuzi ya kesi hiyo kufutwa na kuongeza kuwa hatua hiyo inatoa wigo wa mbunge huyo kuwatumikia wananchi.

Akiwa ofisini kwake, Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu akapata fursa ya kuzungumzia Maamuzi ya Mahakama juu ya kesi hiyo ambapo amempongeza Mabula kwa uvumilivu wake kwa kuwa kiongozi akiwa na kesi Mahakamani anakosa uimara wa kuwatumikia wananchi.

Katika uchaguzi Mkuu uliofanyika Octoba 25 mwaka jana, Angelina Mabula (CCM) aliibuka mbunge wa Jimbo la Ilemela kwa kupata ushindi wa kura 85,425 na hivyo kumshinda mpinzani wake wakaribu kutoka Chadema Highness Kiwia aliekuwa akitetea jimbo hilo ambae alipata kura 61,679.
Mutabanzi Julius Lugaziya ambae ni Mwanasheria Mwandamizi aliekuwa akimtetea  Angelina Mabula akihojiwa na Wanahabari nje ya Mahakama
Mutabanzi Julius Lugaziya ambae ni Mwanasheria Mwandamizi aliekuwa akimtetea  Angelina Mabula akihojiwa na Wanahabari nje ya Mahakama
Katibu wa Mbunge wa Ilemela Kheri James (mwenye miwani) akiwa katika mahojiano na wanahabari nje ya Mahakama
WanaCCM wakieleza namna walivyopokea maamuzi ya Mahakama
WanaCCM wakieleza namna walivyopokea maamuzi ya Mahakama
WanaCCM wakieleza namna walivyopokea maamuzi ya Mahakama
Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu akieleza namna alivyopokea maamuzi ya Mahakama.

No comments:

Post a Comment