Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, July 27, 2013

TCRA YATOA ONYO KALI::NI KOSA KUFANYA YAFUATAYO


 

Msemaji toka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania(TCRA) Innocent Mungy(kushoto)akieleza kwa waandishi wa habari kuhusu madhara ya kutumia visivyo huduma ya mawasiliano na utumiaji wa majina yasiyo sahihi katika usajili wa namba za simu kwenye mkutano uliofanyika ukumbi wa Idara ya Habari leo Jijini Dar Es Salaam,kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari Zamaradi Kawawa. (Picha na Hassan Silayo)
MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

MATUMIZI MABAYA YA MAWASILIANO NA UDANGANYIFU KATIKA USAJILI WA NAMBA ZA SIMU ZA MKONONI NCHINI NIKOSA LA JINAI

1.    Huduma za mawasiliano nchini katika kipindi cha miaka kumi iliyopita zimekuwa sana na kuwafikia watu wengi zaidi. Ni ukweli usiopingika kuwa watanzania wengi hivi sasa wanafaidika kwa huduma za mawasiliano, hususani katika mawasiliano ya simu za mikononi, utangazaji, intaneti na huduma za ziada kama kutuma na kupokea fedha kwa kutumia mitandao na simu za mkononi. Wananchi wengi wanapata huduma za kibenki kwa kutumia simu zao, wanawasiliana kwa kutumia simu zao kupitia sauti, SMS na kadhalika.

2.    Aidha kumekuwa na ongezeko la matumizi ya intaneti kwa watanzania walio wengi hususani matumizi ya mitandao ya kijamii kama vile Facebook, twitter, BBM, LinkedIn na blog mbalimbali. Matumizi haya yamewanufaisha watanzaia kwani ni fursa murua ya kujifunza kupitia mitandao hiyo ya kijamii kwa kupata habari mpya, kujifunza na kuelimishana kuhusu shughuli za maendeleo na kuleta amani miongoni mwa watanzania.

3.    Pamoja na maendeleo haya chanya kwa nchi yetu, kumekuwepo na baadhi ya watu wachache wanaotumia mawasiliano ya simu, mitandao ya kijamii, redio, TV na mawasiliano mengine kwa lengo la 
kuvuruga amani, kuchocheo ugomvi, kuchonganisha watu, kusababisha ugomvi, kuwaumiza wengine kwa mambo yasiyo na ukweli, kupotosha jamii na hata kuvuruga maendeleo kwa ujumla.

4.    Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inawatahadharisha wananchi kwamba ni kosa la jinai kutumia mawasiliano vibaya kama ilivyoainishwa katika sheria ya Mawasiliano ya Kielectroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010. Wananchi wanashauriwa kuhakikisha wanatumia mawasiliano vizuri na kuhakikisha tunadumisha amani na upendo miongoni mwa watanzania.

5.    Aidha mamlaka inapenda kuwakumbusha wananchi kuwa kusajili laini yako ya simu, kwa kutumia utambulisho wa udanganyifu pia ni kosa la jinai. Mtumiaji wa huduma za mawasiliano unatakiwa kwenda kwa mtoa huduma au wakala wake ukiwa na kitambulisho sahihi chenye picha yako na kutoa taarifa sahihi. Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010, kifungu cha 131, kimeainisha kuwa ni kosa la jinai kutumia au kuwezesha kutumika namba ya simu isiyosajiliwa. Adhabu ya faini ya shilingi laki tano (Tshs 500,000.00) au kifungo cha miezi mitatu itatolewa kwa yeyote atakayekiuka sheria hii.

6.    Kuanzia tarehe 1 Juni 2013 saa sita usiku, laini zote za simu ambazo hazijaanza kutumika zilifungwa (locked) na haziruhusiwi kutumika hadi mtumiaji atakapoisajili laini yake mpya kwa watoa huduma. Kama kuna mwananchi atakaenunua laini, na kuweza kuitumia bila ya kuisajili, anaombwa kutoa taarifa kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA). 

7.    Watumiaji wote wa simu za mkononi ambao hawakuwa wamesajili namba zao za simu wafanye hivyo mara moja. Ifahamike kwamba ilipofika tarehe 10 Julai 2013 saa sita usiku, laini za simu ambazo zilikuwa zinatumika na zilikuwa bado hazijasajiliwa hadi wakati huo, zilifungwa. Kufungua laini iliyofungwa, mtumiaji atapaswa kwenda kwenye ofisi ya mtoa huduma wake au wakala wake kusajili upya na kuthibitishwa ili laini yake ifunguliwe.

8.    Watumiaji wa simu za mkononi na wananchi wanashauriwa kuunga mkono juhudi zinazofanyika ili kufanikisha usajili wa namba za simu kwa ajili ya kudumisha na kuendeleza amani na usalama na kuharakisha maendeleo ya sekta na ya Taifa kwa ujumla.

9.    Faida za kusajili laini ya simu ni nyingi zikiwemo usalama katika huduma za kutuma na kupokea pesa kwa mitandao ya simu. Kununua na kulipia gharama mbalimbali zikiwemo za bili za umeme, maji, na ushuru na pia kusaidia upelelezi iwapo kuna matumizi mabaya ya simu.

10.  Mamlaka inapenda kuukumbusha umma kuwa ni kosa la jinai:

a)   Kuuza laini za simu kama wewe si wakala wa mtoa huduma: Iwapo mtu atakamatwa na kutiwa hatiani akiuza laini za simu ikiwa yeye si wakala wa kampuni ya simu atahukumiwa kulipa faini ya shilingi milioni saba au kufungwa jela miaka miwili au adhabu zote mbili kwa pamoja.

b)   Kutumia simu isiyosajiliwa: Mtu yeyote anayetumia simu isiyosajiliwa anatenda kosa la jinai na akitiwa hatiani atahukumiwa kulipa faini isiyozidi shilingi laki tano, au kifungo cha miezi mitatu jela.

c)    Kutoa taarifa za uongo wakati wa kusajili namba ya simu: Mtu yeyote atakayetoa taarifa za uongo akijua kuwa taarifa hizo si za kweli anatenda kosa la jinai na akitiwa hatiani atahukumiwa kulipa faini ya shilingi milioni tatu au kifungo cha miezi kumi na miwili au adhabu zote kwa pamoja.

d)   Kumsaidia mtu mwingine atende kosa kwa mujibu wa sheria za mawasiliano naye anatenda kosa na akitiwa hatiani atahukumiwa kulipa faini isiyozidi shilingi milioni tatu au kufungwa jela miezi kumi na miwili au adhabu zote mbili kwa pamoja.

e)   Kutumia njia yeyote ya mawasiliano kuvuruga amani, kugombanisha watu, kufanya uchochezi wa kidini au kisiasa, kueneza chuki, kusambaza uongo na kuleta vurugu katika jamii ni kosa la jinai na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya watakaobanika kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria.

f)    Mwananchi ukipokea ujumbe wowote wa kueneza chuki, unaopelekea kuvuruga amani, uchochezi na kuvuruga amani, toa taarifa kwa vyombo husika, kasha futa ujumbe huo. Usiueneze kwa wengine kwani utakuwa sehemu ya uhalifu.

Imetolewa na:


MSEMAJI MAMLAKA YA MAWASILIANO
MAMLAKA YA MAWASILIANO TANZANIA
26 July 2013

No comments:

Post a Comment