Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, July 12, 2013

Toka Kenya:::Waendeshaji Matatu watoa huduma ya bure ya intaneti isiyotumia waya kwa abiria,Tanzania vp Tumejipangaje?


Dereva wa matatu akijaribu kupata intaneti isiyotumia waya katika simu yake ya mkononi. [Na Rajab Ramah/Sabahi]
Magari ya usafiri wa umma mjini Nairobi -- yanayojulikana kwa mziki wake wa sauti kubwa, kupiga honi na uendeshaji mbaya -- yanabadilisha mwenendo.
Waendeshaji wa mabasi madogo na magari madogo ya kuchukua abiria, kienyeji yanayojulikana kama matatu, yanaifanya safari ya abiria kuwa ya kufurahia na wa rahisi zaidi baada ya kuanzisha huduma za intaneti bure bila ya kutumia waya ndani ya mabasi.
"Tumekuwa tukijulikana kwa mambo yote mabaya," alisema Daniel Masava, dereva anayefanya kazi njia No. 125 kutoka katikati ya jiji la Nairobi kuelekea kitongoji cha Ongata Rongai.
"Tunaitwa madereva jeuri ambao tunapuuza sheria za barabarani na kutojali," aliiambia Sabahi. "Lakini tangu kuingizwa kwa Wi-Fi katika magari yetu, sasa tunaonekana kama kibanda cha intaneti kinachotembea tukiwa na mchango kwa uchumi."

Huduma ya Vuma Online inatangazwa nyuma ya matatu mjini Nairobi. Huduma hiyo ni ya bure kwa mabasi ya abiria na shilingi 1,500 kwa mwezi kwa waendeshaji mabasi. [Na Rajab Ramah/Sabahi]

Hapo tarehe 14 Juni, kampuni ya utoaji wa mawasiliano ya simu Safaricom Limited ilitoa huduma za intaneti bila ya kutumia waya, inayoitwa "Vuma Online", kwa kushirikiana na waendesha matatu mjini Nairobi.
Huduma hii itawapa abiria intaneti ya bure bila kutumia waya kwa matatu 200. Magari madogo yanayotumiwa kwa usafiri wa umma kwa kawaida huchukua abiria 14 wakati mabasi madogo yanaweza kuchukua hadi abiria 32.
Huduma hii iliibuka kama mpango wa majaribio ambayo ilijaribu matumizi ya intaneti bila ya kutumia waya na mwitiko wa watumiaji kwa magari 20 ya usafiri wa umma. Sasa, waendeshaji wa mabasi madogo na magari madogo ya abiria wanaweza kujiandikisha kwa huduma hii na kulipa shilingi 1,500 (dola 17) kwa mwezi, ikiwa ni pamoja na kifaa kisiyotumia waya ya kuleta intaneti.

"Wakati wa programu ya majaribio, tuligundua kwamba wateja wetu wanaotumia zaidi matatu kama njia yao ya usafiri ya kila siku wanayoipenda, walitaka wawe mtandaoni, hata pale wanapokuwa wanasafiri," alisema Afisa Mtendaji Mkuu wa Safaricom Bob Collymore.

"Kwa hivyo, kwa sisi kusisitiza hadithi ya intaneti na kuifanya kuwa ni njia ya maisha, ilitubidi tuwapelekee intaneti hiyo kwa kuwapatia Wi-Fi bure katika njia yao za usafiri."

Mpango huu ni wa kwanza wa aina yake barani Afrika na una dhamiri ya kuunganisha mgawanyiko wa kidigitali nchini Kenya, Collymore alisema. Vuma Online inawaruhusu watu wasioweza kumudu huduma za intaneti majumbani kwao kuweza kutumia intaneti kupitia simu zao za mkononi wakati wanasafiri, alisema.

Safaricom pia itategemea uunganishaji wa intaneti isiyotumia waya ndani ya mabasi ili kutoa habari za barabarani na kufuatilia iwapo mabasi ya umma na magari madogo yanakwenda kwa mujibu wa ratiba, Collymore.

Utoaji wa huduma za intaneti kwa vyombo vya usafiri wa umma unaongeza thamani kwa sekta hii, Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Matatu Simon Kimutai alisema, akikana wasiwasi kwamba hii itapelekea kupanda kwa ada.

"Nairobi ni mji wenye matatizo ya msongamano wa magari. Watu [wanaweza] kutumia masaa matatu barabarani, na hii imekuwa ikiwaudhi wasafiri," aliiambia Sabahi. "Lakini sasa hii imebadilika. Wanaweza kuzungumza wakiwa kwenye Facebook, kutuma ujumbe na kutumia intaneti jambo linalowafanya safari yao iwe imejaa furaha."

"Kwa sisi, ni wakati wa kusisimua kwa magari ya umma," Kimutai. "Tuna mageuzi mengi yanayoendelea nchini, lakini mbali na uvumbuzi huu mara hii kuwa unafaa sana kwa abiria, unatufanya tuwe sehemu ya safari ya kuigeuza nchi kuwa ya dijitali."

Wasafiri watathmini huduma hiyo mpya
Kwa Caroline Omondi, mwenye umri wa miaka 26, intaneti bila ya waya ndani ya matatu inamweka mbele kwa siku yake ya kazi na inamruhusu kupata masaa ya ziada ya kulala asubuhi.

Omondi alisema alikuwa anaamka saa tatu mapema zaidi ili kusafiri kutoka Kayole hadi kazini kwake mjini Nairobi kama opereta wa safari na utalii ili aweze kujibu barua pepe za kampuni kabla ya kufika saa ya harakati nyingi.

"Sasa ninaondoka nyumbani saa 2 asubuhi, na wakati ninapokuwa ofisini kiasi cha saa 3:30 asubuhi, ninatumia intaneti inayotolewa na matatu ili kujibu mahitaji yangu yote," alisema. "Kwa sasa sina wasiwasi tena wa kuamka nimechelewa."

Omar Said, mwanafunzi wa sheria mwenye umri wa miaka 23 katika Chuo Kikuu cha Nairobi, anatumia huduma za intaneti bila ya kutumia waya ndani ya basi kwa kupakua programu za matumizi kwa ajili ya simu na kompyuta yake, miongoni mwa shughuli nyengine ambazo zinamfanya awe na harakati wakati wa safari yake baina ya nyumbani na shule.

"Ninatumia angalau saa nne kwa siku katika gari la umma," aliiambia Sabahi. "Katika muda huu, ninafanya utafiti wangu na kupakua nyaraka mtandaoni ambazo ninazitumia kujenga mradi wangu ambao unatakikana mwezi ujao."

Hata hivyo, Viola Maingi, 22, alikuwa mmoja wa wasafiri walioeleza wasiwasi wao kwa huduma hii mpya, alisema ilisababisha kuongezeka kwa wizi wa simu.

"Wiki iliyopita, simu yangu iliporwa na mtu aliyejidai kuwa mtembea kwa miguu katika Barabara ya Jogoo. Simu yangu ilikuwa kiganjani na madirisha ya gari yalikuwa wazi," aliiambia Sabahi. "Woga huu ni wa kweli na ni jukumu ya wasimamizi wa matatu kuhakikisha usalama wetu ili huduma hii iweze kuwa yenye mafanikio."

Chanzo - sabahionline.com

No comments:

Post a Comment