Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, September 2, 2013

Kazimoto apiga bao 2 Qatar


Mwinyi Kazimoto.
Na Mwandishi Wetu
NEEMA imeanza kumjaa kiungo wa zamani wa Simba, Mwinyi Kazimoto, baada ya kupiga mabao mawili safi akiwa na timu yake mpya ya Al Markhiya ya Qatar.
Kazimoto amefanikiwa kufunga mabao mawili katika mechi tano alizoichezea timu hiyo inayoshiriki daraja la pili nchini Qatar.
Pamoja na kufunga mabao hayo mawili katika mechi tano za kirafiki alizocheza, Kazimoto amefanikiwa kupata namba ya kudumu katika kikosi cha kwanza.
Kocha wa zamani wa Simba, Hassan Afif, aliyemsaidia Kazimoto kujiunga na timu hiyo nchini Qatar, ameliambia Championi Jumatatu kwamba kocha wake kutoka nchini Serbia amemhakikishia namba katika kikosi cha kwanza.
“Kweli amefunga mabao mawili katika mechi hizo tano, walikuwa wamekwenda kuweka kambi nchini Tunisia na sasa wamesharejea hapa Doha tayari kwa ajili ya ligi itakayoanza wiki mbili zijazo.
“Kazimoto ameonyesha uwezo mkubwa sana kwa kweli, mabao aliyofunga ni mazuri. Kilichomvutia zaidi kocha ni kwamba, katika mechi zote tano, hajacheza dakika 90 katika kila mchezo, lakini amefanya vizuri.
“Wakati mwingine alianza au kuingia katika kipindi cha pili, kocha alifanya hivyo kwa ajili ya kujaribu wachezaji lakini inaonekana kama amejihakikishia namba katika kikosi cha kwanza na kocha ametaka aendelee na juhudi hizo,” alisema Afif.
Akiyaelezea mabao ya Kazimoto, Afif alisema: “Sijayaona lakini kocha kaniambia ni mazuri na moja lilikuwa ni la shuti kali nje ya eneo la kumi na nane. Iimemfurahisha sana.”
Kazimoto amejiunga na Al Markhiya akitokea Simba ambayo ameichezea kwa misimu miwili, kabla ya hapo alikuwa kiungo tegemeo wa JKT Ruvu.
Kazimoto ambaye amechipukia kisoka mkoani Mwanza alikozaliwa, anasifika kwa kupiga mashuti makali pia pasi za uhakika zinazozaa mabao na amekuwa akifunga mabao kwa mashuti ya mbali akiwa na Simba pamoja na Taifa Stars.

No comments:

Post a Comment