Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, November 21, 2013

MAGUFULI APIGA MARUFUKU MAGARI YA SERIKALI GEREJI BINAFSI


Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, amepiga marufuku magari ya serikali kutengenezwa kwenye gereji binafsi na badala yake Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa) afanye kazi hiyo. 
Kadhalika, Waziri Magufuli amesema ipo harufu ya rushwa kwa mameneja wa Temesa mkoa kwa kutoa vibali kwa magari ya serikali kutegenezwa gereji za watu binafsi na hivyo kuikosesha serikali mapato.
 Aliyasema hayo jana wakati wa kukabidhi vitendea kazi vya karakana za mikoa na vituo kwa mikoa kumi ya Tanzania Bara.
Alisema ipo tabia iliyoota mizizi kwa mameneja kutoa vibali magari ya serikali yatengenezwe gereji za watu binafsi ambazo nyingine ni bubu huku wataalamu walioajiriwa na serikali wakishindwa kuwajibika.

Alisema kwa mujibu wa sheria namba 30 ya mwaka 1997, hairuhusiwi gari yoyote ya serikali kutengenezwa nje ya karakana zake, lakini kwa maslahi binafsi imekuwa kawaida kwa magari hayo kutengenezwa hadi gereji bubu.
Alisema Wizara itaendelea kutoa vifaa zaidi ili kuboresha karakana hizo kwa kuwa kumekuwa na malalamiko ya ukosefu wa vifaa hali iliyotumika kama fursa kwa mameneja kupeleka magari kwenye gereji binafsi.
Alisema lipo tatizo sugu la taasisi za serikali kutengenezewa magari na kugoma kulipa hali ambayo imekuwa kikwazo kwa ukuaji wa Temesa kwani inadai mamilioni ya fedha.

Bila kuzitaja taasisi hizo, alisema zinafanya makusudi kwa kutengenezewa magari na wanapokumbushwa kulipa huyakana madeni na ufuatiliaji huwa mgumu kutokana na kukosekana kwa nyaraka muhimu.


Pia, wanapokuja kutengeneza kwa awamu ya pili huomba kibali cha kwenda gereji za nje na mameneja huvitoa hali inayozua utata
“Gari ya serikali ikitengenezwa Temesa haitaki kulipa ila ikipelekwa gereji binafsi wanalipa kwa wakati…kuanzia sasa hakuna kutengeneza gari pasipo makubaliano rasmi kwa kuchukua taarifa za aliyepeleka gari ili fedha hizo zikatwe moja kwa moja kwenye fungu la matumizi ya ziada kutoka Wizarani,” alisisitiza Magufuli.
Aidha, alizitaka karakana hizo kuongeza ufanisi wa kazi  ikiwa ni pamoja na kumaliza kazi kwa haraka kwani kumekuwa na malalamiko ya ucheleweshwaji wa kazi ikiwa ni pamoja na kukosa lugha ya biashara.
“Ifike mahali Meneja wa karakana ya Vingunguti na Mt mjiulize kwanini magari ya serikali Dar es Salaam, yanatengenezewa Kibaha, inaonyesha karakana hiyo imejiaminisha inafanyakazi kwa ufanisi,” alibainisha.
Aidha, aliagiza magari ya miradi ya barabara yaliyo chini ya Wakala wa Barabara Nchini (Tanroads), yasajiliwe na kuuza kwa Temesa na Wakala wa majengo Tanzania (TBA), ambako kuna upungufu mkubwa na maeneo mengine hakuna magari.

Awali, Mtendaji Mkuu wa Temesa, Mercelline Magesa, alisema utoaji wa vifaa hivyo ni endelevu na ni awamu ya pili baada ya mikoa kumi ya awali vilivyogharimu zaidi ya Sh. milioni 823.8.

No comments:

Post a Comment