Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Thursday, November 21, 2013

UTAFITI: POLISI MMOJA HULINDA WATANZANIA 1, 700

 Jeshi la Polisi nchini bado linakabiliwa na changamoto ya askari polisi kwa ajili ya kulinda usalama wa Watanzania na mali zao.

Akizungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika, yaliyofanyika jana kwenye Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Polisi, Thobias Andengenye, alisema, takwimu zimelisaidia jeshi hilo katika kupanga mipango mbalimbali ikiwa ni pamoja na kujua idadi ya askari polisi wanaotakiwa kuwalinda  Watanzania na mali zao.

Kwa mujibu wa Andengenye, kutokana na takwimu za jeshi hilo, hadi sasa askari polisi mmoja anawalinda Watanzania zaidi ya 1, 700 na mali zao, uwiano ambao unakinzana na ule wa kimataifa wa askari mmoja kwa raia 400.

Alisema, takwimu kwa jeshi hilo ni za muhimu kwani zimeweza pia kuwasaidia kujua makosa ya uhalifu na kupanga mipango ya kuyadhibiti na kutokana na hizo wameweza kupunguza kiwango cha uhalifu kutoka zaidi ya 190,000 hadi 172, 795 kati ya mwaka 2008 na 2012.

Akizindua kwa niaba ya Waziri wa Fedha,  Naibu Waziri wa wizara hiyo, Saada Mkuya, alisema, maadhimisho hayo ni ya 20 tangu yale yaliyofanyika mwaka 1993, na kwamba, takwimu ni sekta mtambuka inayogusa kila eneo huku akiitaka serikali kusambaza takwimu bora kwa kila sekta ili kupanga maendeleo ya nchi.
 
CHANZO: NIPASHE



No comments:

Post a Comment