Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, December 30, 2013

DK NGASONGWA: CCM INABABAIKA

ngasongwa1 9cf74
Ni kutokana na viongozi wake kusema hadharani bila ya kutumia vikao vya chama
Dar es Salaam. Waziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa na katika Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, Dk Juma Ngasongwa amesema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinababaika katika kutekeleza majukumu yake.
Vilevile, chama hicho kimekumbwa mgawanyiko kati ya watendaji wake na Serikali na kwamba taifa lina ombwe la uongozi.
Kutokana na hali hiyo, Dk Ngasongwa ambaye pia ni kada wa CCM amemshauri Rais Kikwete kuwa mkali katika kusimamia watendaji wake anaowateua ndani ya chama na Serikali yake na kufuatilia na kupima utekelezaji wa yanayokubaliwa .
Alikuwa akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake mkoani Morogoro anakoendesha maisha yake kwa kilimo cha mpunga baada ya kustaafu.
Dk Ngasongwa alisema kuwa mgawanyiko huo kati ya watendaji wa Serikali na CCM, umeondoa umoja siyo tu katika vyombo hivyo, bali pia miongoni mwa wabunge wa chama hicho tawala.
Alisema kuwa hali hiyo inasababisha kutokea mambo mengi ikiwamo matukio ya mawaziri kushinikizwa kujiuzulu kama ilivyotokea hivi karibuni na kwamba kwa Serikali ya Awamu ya Nne hali hiyo imekuwa ikijirudia.
"Chama tawala kinababaika sana, tena hata watendaji wa CCM, wanawasema vibaya mawaziri hadharani, wakati wote ni wateuliwa wa Rais (Jakaya Kikwete) na ndiye mwenyekiti wetu wa CCM. Hii inakigawa chama. CCM ina utaratibu wake, kwa nini wasiitwe wakahojiwa ndani ya chama, badala ya kutajana hadharani:
"Sielewi kwa nini CCM inababaika. Inachotakiwa ni kuwa na mshikamano kwa wabunge wake kukutana mara kwa mara na kujenga msimamo. Hii ni kazi ya mawaziri na wabunge pia," alisema Dk Ngasongwa na kuongeza:
"...Tatizo uongozi haufanyi kazi vizuri, ndani ya chama chetu kuna mgawanyiko mkubwa hata katika Serikali, mfano Mwanasheria Mkuu (AG) anaposema baadhi ya mawaziri hawamsikilizi, hii 'No' (hapana), lazima kanuni za uendeshaji wa Serikali zifuatwe, hii ni muhimu."
Alisema hali hiyo inaonekana hata kwenye Baraza la Mawaziri na kwamba mgawanyiko pia upo ndani ya Bunge kwa wapinzani.
"Lakini kugawanyika kwa upinzani ni afadhali kuliko CCM, kwani matokeo yake ni kupunguza imani ya watu kwa Serikali yao na chama tawala," alisema.
Akinukuu maneno ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Dk Ngasongwa alisema: "Nyerere alisema, bila CCM madhubuti nchi itayumba na ndiyo yanayotokea sasa.
"Msingi wa yote yanayotokea ni ubinafsi, ubepari...; turudi kwenye Ilani ya chama, tuzungumze, tufikie mwafaka, siyo kutukanana hadharani. CCM itoe mwongozo siyo kugawa wananchi."
Ngasongwa aliyeshika nyadhifa mbalimbali za kisiasa katika CCM na Serikali ikiwamo ujumbe wa Kamati Kuu (CC), ubunge wa Ulanga Magharibi, Waziri wa Maliasili na Utalii na baadaye Waziri wa Mipango, Viwanda na Uwezeshaji, alifafanua kwamba kuna ombwe la uongozi katika chama tawala, upinzani, Serikali hata bungeni.
"Kuna ombwe la uongozi siyo tu kwa wapinzani, hata sisi chama tawala CCM, Serikali, hata bungeni pia kuna mchanganyiko na yanaonekana waziwazi. Tunaona Spika anavyodharauliwa na wabunge. Bunge linaonyesha picha ya hali halisi ya nchi yetu ilivyo,"alisema Dk Ngasongwa.
Alipotakiwa kuzungumzia zaidi
tukio la hivi karibuni la Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa mawaziri wanne walioshinikizwa kujiuzulu kutokana na Ripoti ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili, alieleza kuwa hajaisoma kwa undani ripoti hiyo, lakini inaonyesha kuwa utekelezaji wake ulikuwa mbaya.

Hata hivyo, alisema kuwa kamati hiyo ilitakiwa kuainisha makosa ya watendaji wa operesheni hiyo na kuwaacha mawaziri wajipime na kujiuzulu wenyewe.
Alisema kwamba hatua ya wabunge na kamati kushinikiza mawaziri hao wajiuzulu iliwachongea kwa Rais Kikwete aliyeamua kuwafukuza kazi kwa lugha ya kistaarabu, hali ambayo alielezea kuwa inaweza kujenga uhasama baina ya wabunge, kamati na mawaziri walioondolewa.
Hivi karibuni Rais Kikwete alitengua uteuzi wa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamshi Vuai Nahodha, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk Emmanuel Nchimbi pia Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk Mathayo David Mathayo baada ya wizara zao kutajwa kushindwa kusimamia Operesheni Tokomeza Ujangili, iliyopoteza maisha ya watu, mifugo na vitendo vya ukatili kwa binadamu.
Kuhusu kubadilika kwa mawaziri, Dk Ngasongwa alieleza kuwa jambo hilo siyo baya, lakini akasema kwamba likifanyika mara kwa mara linadumaza wizara kwa kukosekana mwendelezo wa utendaji.
"...Ikitokea mara kwa mara inadumaza utendaji, hupati 'continuity' (mwendelezo mzuri), kwani mawaziri huhitaji kujifunza na utekelezaji huhitaji muda. Continuity ni muhimu kwa mawaziri, hata watendaji wengine," alisema.
Hii ni mara ya tatu kufanyika kwa mabadiliko ya Baraza la Mawaziri tangu kuingia madarakani kwa Serikali ya Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete, likiwamo lililotokea baada ya aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa kujiuzulu. Chanzo: Mwananchi

No comments:

Post a Comment