Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, December 18, 2013

Mazishi ya Mabina kesho, JK atuma salamu


1525078_628074627256535_244985913_n
Clement Mabina, enzi za uhai wake
Mwanza.Wakati maziko ya aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM mkoani hapa na Diwani wa Kata ya Kisesa, Clement Mabina yakifanyika kesho katika kilima cha Kanyama, ikiwa ni eneo ambalo alilouawa na kundi la watu Jumapili iliyopita,Rais Jakaya Kikwete ametuma salaam za rambirambi kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza kutokana na msiba huo.
Mabina, aliyekuwa Mwenyekiti CCM Mwanza hadi Oktoba 2012, aliuawa na kundi la watu wenye hasira katika kilima cha Kanyama, katika kata ya Kisesa, kiasi cha kilometa 10 Mashariki ya jiji la Mwanza.
Msemaji wa familia, Timothy Gregory aliiambia Mwananchi jana kuwa, mipango ya mazishi imekamilika kabla ya watu kutoa heshima zao za mwisho na mazishi yatafanyika kesho (Alhamisi) mchana.
“Baadhi ya watu muhimu katika familia wamekwishawasili akiwamo binti yake mdogo aliyekuwa Ulaya,” alisema msemaji wa familia.
Alisema binti mkubwa wa marehemu alikuwa akitarajiwa kufika Mwanza muda wowote jana tayari kwa mazishi ambayo yatashirikisha pia viongozi wa chama na Serikali kutoka ndani na nje ya Mkoa wa Mwanza.
Wakati huo huo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, SACP Valentino Mulowola alisema, kulikuwa hakuna mtuhumiwa aliyeongezeka jana baada ya saba waliokamatwa juzi katika maeneo ya Kisesa na Kanyama.
Salaamu za rambirambi
Katika taarifa yake kupitia Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, Rais Kikwete alisema: “Nimemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Evarist Ndikilo kutokana na vifo vya watu wawili vilivyotokea Desemba 15, mwaka huu katika Kitongoji cha Kanyama Kata ya Kisesa Wilaya ya Magu, Mkoani Mwanza.”
Taarifa hiyo ilisema kuwa Rais ametuma salamu hizo kutokana na vifo vya Mabina na Tenery Malimi vilivyotokea baada vurugu zilizosababishwa na mabishano ya ardhi. Rais amemuomba mkuu wa mkoa kuwatahadharisha wananchi kutokuchukua sheria mikononi na pia kuwa waangalifu na matumizi ya silaha za moto.
“Nimesikitishwa na kufadhaishwa na taarifa za vifo vya wananchi hao wawili vilivyosababishwa na mgogoro wa ardhi ambao ungeweza kupata suluhu kwa njia za amani. Ni vyema wananchi wakawa na subira na kuwa waangalifu katika kutatua migogoro yao,”. Rais alisema na kuongeza kuwa ni “subira na busara ndiyo ziwe muongozo wa kutatua migogoro yetu katika jamii badala ya hasira”.
Mabina aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali zikiwamo Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Magu mwaka 2000 – 2005, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza, mwaka 2007 – 2012. Rais ameziombea nyoyo za marehemu wote Mungu azilaze mahali pema peponi Amen.
CHANZO: MWANANCHI


No comments:

Post a Comment