Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, January 11, 2014

SIMBA, SIMBA, SIMBA…KILA KONA NI SIMBA TUUUU...TANZANIA NZIMA


Kiemba akipongezwa na wenzake baada ya kufunga bao la pili


SIMBA SC wamefuzu kuingia Fainali ya Kombe la Mapinduzi, baada ya usiku huu kuilaza mabao 2-0 URA ya Uganda kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Shujaa wa Simba SC leo alikuwa ni kiungo mwenye kipaji, Amri Ramadhani Kiemba aliyesababisha bao la kwanza na kufunga mwenyewe la pili.
URA ilipata pigo mapema dakika ya 32 baada ya mshambuliaji wake hatari, Owen Kasuule kutolewa nje kwa nyekundu ya moja kwa moja kwa kumchezea rafu winga msumbufu wa Simba SC, Ramadhani Singano ‘Messi’.
Dakika 45 za kipindi cha kwanza zilimalizika timu hizo zikiwa hazijafungana na kipindi cha pili ndipo Simba SC inayofundishwa na Mcroatia, Zdravko Logarusic ilipofungua makucha yake.   

Kona maridadi ya Kiemba ilimkuta beki Donald Mosoti, aliyemsetia beki pacha wake wa kati, Joseph Owino akafunga bao la kwanza dakika ya 49.
Wakati URA wanahaha kusaka bao la kusawazisha, Simba SC walifanya shambulizi zuri na krosi maridadi ya Haroun Chanongo ikaunganishwa nyavuni na Amri Kiemba dakika ya 52 kuipatia Simba SC bao la pili.
Bao hilo liliinyong’onyesha kabisa URA, ingawa iliendelea kupambana kupata japo bao la kufutia machozi.
Kwa ujumla, URA iliathiriwa mno na kutolewa na mshambuliaji wake hatari, Owen Kasuule, kwani ndiye tegemeo lake la mabao kwa pamoja na Feni Ali.
Baada ya mechi, Kiemba alipewa king’amuzi cha Azam TV kwa kuwa mchezaji bora wa mechi hiyo.
Simba SC sasa itapambana na KCC ya Uganda pia katika Fainali Jumatatu Saa 10:00 Uwanja wa Amaan.

No comments:

Post a Comment