Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, August 17, 2015

BRN YAIPA CHANGAMOTO SERA YA UGATUAJI MADARAKA

DSC_0734
Profesa Fortunata Makene wa idara ya tafiti za mikakati na machapisho wa Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF), akifungua warsha hiyo ya siku moja iliyowakutanisha wataalamu kujadili matokeo ya utafiti wa ufanisi wa mfumo wa ugatuaji madaraka ambapo mamlaka yanapelekwa kwa wananchi (Efficiency and Effectiveness of Decentralization and Local Government Capital Development Grant LGCDC systems in Tanzania).(Picha zote na Zainul Mzige wa Modewjiblog)
Na Mwandishi wetu,
HATUA za haraka zinapaswa kuchukuliwa ili kuwezesha mpango wa matokeo makubwa sasa (BRN) kutovuruga matunda ya sera ya ugatuaji madaraka uliofanywa mwaka 1998 na kuanzwa kutekelezwa mwaka 2004.
Sera ya ugatuaji madaraka imelenga kuwezesha wananchi kupanga mipango yao ya maendeleo kwa kuzingatia mahitaji yao na kupigwa jeki na serikali kuu.
Lengo la sera hiyo ni kupeleka sauti ya maendeleo kwa wananchi wenyewe badala ya sera za awali ambapo utekelezaji wa mipango ya maendeleo ulifanywa na serikali kuu.
Kauli hiyo imetolewa mwishoni mwa juma katika mkusanyiko wa wataalamu kujadili matokeo ya utafiti wa ufanisi wa mfumo wa ugatuaji madaraka ambapo mamlaka yanapelekwa kwa wananchi (Efficiency and Effectiveness of Decentralization and Local Government Capital Development Grant LGCDC systems in Tanzania) ulioendeshwa na timu ya watafiti wakiongozwa na Profesa Godius Kahyarara wa Sayansi Jamii idara ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
 
Katika utafiti huo ilibainishwa kwamba pamoja na ubora wa mfumo huo uliotoa mabadiliko ya watu kujitengenezea wenyewe mipango yao ya maendeleo, sasa hivi unakabiliwa na changamoto ya BRN.
Akiwasilisha utafiti huo, mmoja wa watafiti hao, Victor Geofrey, alisema kwa kutumia methodolojia ya maswali na majadiliano walibainisha kwamba katika utekelezaji wa BRN maeneo ambapo mipango ya wananchi ilikuwa sawia na vipaumbele vya BRN miradi ilifanikiwa lakini kwingine haikuwa hivyo.
DSC_0808  
Alisema katika uwasilishaji wake wa utafiti huo uliofanyika katika mikoa mitano kwa wilaya mbili katika kila mkoa, hatari ya watanzania kurejea katika mfumo wa mwanzo wa maagizo ya juu kutekelezwa, unanukia kama kusipooitafutwa njia ya kuoanisha BRN na mfumo wa utekelezaji wenye matokeo bora ya ufanisi ya serikali za mitaa na mikoa.
Alisema madhumuni ya utafiti huo ambao ulitaka kujua ufanisi wa mfumo wa LGCDG nchini Tanzania na mwingiliano wa mifumo ya utawala katika ugatuaji madaraka na athari chanya au hasi za mifumo hiyo katika utekelezaji wa mipango ya BRN na ya miaka mitano ya maendeleo ikiwemo Mkukuta.
Mikoa iliyohusika na utafiti huo na wilaya zao katika mabano ni Tanga ( halmashauri ya Jiji na Korogwe); Mwanza ( Ilemela, Nyamagana); Mara ( Bunda, Musoma);Dodoma ( Chamwino, Manispaa ya Dodoma) na Morogoro (Kilombero, Manispaa ya Morogoro).
Alisema takwimu zikiwa zimetolewa katika maeneo ya BRN, watawala mbalimbali na wananchi zilibainisha kwamba miradi ambayo wananchi tangu awali walikuwa wameipendekeza kutekelezwa katika maeneo yao ndiyo iliyoonesha ufanisi.
Aidha ilionekana wazi katika muda wote wa utekelezaji malengo yaliyopewa kipaumbele na mpango wa ugatuaji madaraka na LGCDC yalifanikiwa kuwa kuwa uasilia wao ulitambulika na wananchi wenyewe kupitia mifumo ya wao kujadili nini wanakihitaji kama maendeleo yao.
     
DSC_0750
Pichani juu na chini mmoja wa watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Victor Geofrey, akiwasilisha mada katika mkusanyiko wa wataalamu kujadili matokeo ya utafiti wa ufanisi wa mfumo wa ugatuaji madaraka ambapo mamlaka yanapelekwa kwa wananchi (Efficiency and Effectiveness of Decentralization and Local Government Capital Development Grant LGCDC systems in Tanzania) wakati wa mkutano huo uliofanyika mwishoni mwa juma katika ukumbi wa mikutano wa ofisi za Taasisi Huru ya Utafiti wa Uchumi na Jamii (ESRF).
Hata hivyo katika utafiti huo waliona changamoto nyingi ikiwamo za fedha kuchelewa kufika au kutofika kabisa na pia BRN ilileta mkanganyiko kutokana na fedha za miradi ya LGCDG zilitumika kutekeleza BRN na kufanya miradi mingi kutokuwa na ufanisi na kuwa kati ya asilimia 20 na 25.
Kutofikishwa kwa fedha za CDG pia kumesababisha wananchi kuchangia utekelezaji wa miradi ya BRN kama maabara na madesk.
Aidha hali hiyo iliathiri kaya mbalimbali kushiriki katika uzalishaji wa kiuchumi kutokana na ukweli kuwa wale ambao hawakushiriki katika kutoa fedha kwa ajili ya mradi wa BRN wa maabara walikamatwa na kusekwa lupango, kufungwa au kutozwa faini.
Kutekelezwa kwa miradi ya BRN ambayo mingi haikuwa kipaumbele cha serikali za maeneo husika kumetibua mfumo wa mpango na utekelezaji kwa kufuata sera ya ugatuaji madaraka.
Kutokana na ukweli huo ufanisi wa sera ya ugatuaji unaathiriwa na uwapo wa BRN.
Hata hivyo sehemu nyingine ya changamoto za mfumo wa ugatuaji kuwezesha maendeleo umeathiriwa na baadhi ya wanasiasa kuwashawishi wananchi kwamba serikali ina fedha za kutosha kwa hiyo wasichangie nguvu zao kama sera inavyohimiza.
Kwa mfano wilaya ya Kilombero ambayo kipaumbele chake kilikuwa kujenga nyumba za walimu ilijikuta inaachana na kipaumbele hicho na kuanza kutekeleza agizo la serikali la ujenzi wa maabara, kitu ambacho kimo katika BRN.
 
DSC_0765
Hata hivyo mtafiti huyo alisema pamoja na uzuri wa BRN katika maeneo ambayo mipango ilienda sawia na ile iliyokuwapo tangu awali iliyotakiwa na wananchi bado wengi wa wananchi hawafahammu BRN wakati walikuwa wanajua vyema utaratibu wa mipango na utekelezaji katika mfumo wa ugatiuaji madaraka.
Ingawa watafiti walipendekeza kwamba LGCDG katika hali ya uwapo kwa BRN, BRN itengewe fedha zenyewq, washiriki walishauri watafiti kuangalia kwa undani zaidi suala hilo kwani BRN si mradi bali ni kionjo kilicholenga kuharakisha utekelezaji wa mipango ya maendeleo.
Hata hivyo walikubaliana, washiriki hao kwamba ipo haja ya halmashauri kuwa na vyanzo vyake vyenyewe vya mapato ingawa wanahitji fedha za serikali kuu kuanzia vyanzo vya mapato.
Watafiti walisema kwamba halmashauri nyingi hazihitajhi kusubiri fedha za serikali kwa miradi yake kwani nyingi zina vyanzo vizuri vya fedha kama ilivyo wilaya ya Chamwino.
 
DSC_0763
Mmoja wa washiriki wa mkusanyiko wa wataalamu kujadili matokeo ya utafiti wa ufanisi wa mfumo wa ugatuaji madaraka ambapo mamlaka yanapelekwa kwa wananchi (Efficiency and Effectiveness of Decentralization and Local Government Capital Development Grant LGCDC systems in Tanzania) akiuliza swali kwa mtoa mada (hayupo pichani).
Alisema wilaya hiyo imetiliana saini na TIB kuanzisha kiwanda cha mvinyo katika wilaya hiyo huku Wamarekani wakiwa wamekubali kuanzisha kiwanda cha asali.
Aidha watafiti walisema kama sehemu ya kuimarisha mfumo wa sasa wa mipango kuanza kwa wananchi ipo haja kwa watu kuelewa BRN na kuangalia namna bora ya kuihuisha na utaratibu wa ugatuaji ili kuwepo na mafanikio ynayotakiwa katika miradi mbalimbali ya maendeleo.
Awali akifungua warsha hiyo ya siku moja, Profesa Fortunata Makene wa idara ya tafiti za mikakati na machapisho wa ESRF, aliwataka washiriki kuipa nguvu zaidi tafiti hiyo ili iweze kupanuliwa zaidi na matokeo yake kusaidia kuimarisha mfumo wa ugatuaji madaraka pamoja na kuwepo kwa miradi mbalimbali inayoletwa nchini.
Alisema haja ya kushiriki katika mawazo kunatokana na ukweli kuwa maamuzi ya serikali ya mwaka 1998 yaliyotengeneza ugatuaji madaraka, yaani kupeleka mamlaka ya kupanga mipango katika ngazi ya chini kabisa ya wananchi wenyewe na kuipeleka juu bado ni makini na kwamba kunahitajika kuondoa kasoro zinazotishia ufanisi wake.
Alisema kutokana na umuhimu wa sera hiyo ya serikali ya ugatuaji ambayo ilianza kazi mwaka 2004 baada ya kupitishwa na bunge, ESRF, inaona muda umefika wa kufanya utafiti wa kina ambao utawasaidia watengeneza sera na wafanya maamuzi kuwa na taarifa za kutosha kuhusu changamoto zinazokabili serikali za mitaa katika kutekeleza sera ya ugatuaji na namna ya kufanya ili kuimarisha mfumo wa madaraka kwa wananchi katika kupanga maendeleo yao.
DSC_0757
Muwasilishaji mada ambaye ni mmoja wa watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Victor Geofrey akijibu maswali kutoka kwa washiriki (hawapo pichani).
DSC_0758
DSC_0821
Picha ya pamoja.

No comments:

Post a Comment