Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Friday, September 18, 2015

UONGOZI WA CHAMA CHA NCCR-MAGEUZI WATOFAUTIANA NA TARATIBU ZA UKAWA

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-MAGEUZI, Reticia Ghati Mosore akizungumza na vyombo mbalimbali vya habari katika Hoteli ya Land Mark jijini Dar es Salaam  kuhusiana na ukiukwaji wa taratibu katika umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) na kutangaza kuendelea na mapambano nje ya umoja huo wa vyama pinzani. 
Katibu Mkuu wa NCCR-MAGEUZI, Mosena Nyambabe akizungumza na waandishi wa habari juu ya hatima yao ya kupambana kama wenyewe NCCR-MAGEUZI bila ya UKAWA na  kuwa  chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA  kuwa inavibana  vyama vishiriki vya UKAWA  katika wagombea wa Ubunge majimboni na wagombea wa udiwani katika kata.


 Na Chalila Kibuda
Sintofahamu imeibuka ndani ya chama cha NCCR-Mageuzi ambapo viongozi wake wamedai kuwa taratibu zilizo ndani ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) zimekiukwa na kufanya chama hicho kuingia katika mgogoro wa majimbo. 
 Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho,Leticia Ghati Mosore amesema  kuwa NCCR-Mageuzi wamezidiwa idadi ya majimbo kutokana na taratibu nyingi kukiukwa kuanzia serikali ya Mtaa na sasa uchaguzi Mkuu.

 
 Mama Mosore amesema baada ya kuona mambo hayaendi sawa, na ingawa wataendelea kuwa UKAWA, lakini sasa wameamua kupambana wenyewe kama NCCR-Mageuzi katika kugombea viti vya ubunge pamoja na udiwani katika mgawanyo huo ambao amedai chama hicho kimepata majimbo pungufu ndani ya umoja wa vyama vinavyounda Ukawa. 
Amesema kuwa ili kukamilisha ushirikishwaji kulitakiwa kuundwa kamati zitakazoendesha uchaguzi ndani ya UKAWA na mambo mengine mengi ikiwemo uwazi wa matumizi ya fedha, lakini hayajaweza kufanyika hivyo . 
“Mchakato wa kumpata mgombea Urais haukufuata utaratibu katika ushirikishwaji wa vyama vyote vitakavyoweza kutambua mgombea gani anaweza kusimama katika kupeprusha bendera ya UKAWA”, amesema Mama Mosore.
Mama Masore pia ametaka Mwenyekiti wao Mhe. James Mbatia asiwe msemaji wa CHADEMA wakati anakiacha chama chake (NCCR-Mageuzi) kinadhoofika, akidai kwamba wananchi wanashindwa kututoufautisha UKAWA na CCM na wataamua kuchagua zimwi walijualo. “Tunasisitiza upinzani wa kweli nchini hauwezi kujengwa kwa njia za hila, kwa kukiuka taratibu za kidemokrasia, tutachangishana ili tusafiri kwenye majimbo na kata za wagombea wetu na kuwasaidia” alisema. 
Mama Masore amesema”Tunamshauri Mwenyekiti James Mbatia aitishe vikao vya kikatiba haraka  ili tuweze kujadiliana kuhusu hatima ya Chama chetu.Upinzani wa kweli haujengwi kwa kuweka mbele tamaa na maslahi binafsi kuliko taifa, na kwa kutegemea propaganda. 
 “Tangu UKAWA ianze, matokeo yake yamekuwa ni mabaya kwa uhai na ustawi wa Chama chetu cha NCCR”, amesema mama Masore. 
 Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Chama hicho,Bw. Mosena Nyambabe amesema kuwa chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimekuwa ndio kinafanya uandaji wa masuala yote bila kuwa na ushirikiano na NCCR-Mageuzi licha kuwa na udogo katika muungano huo. 
 Bw. Nyambabe amewataka wanachama wote wa NCCR-Mageuzi kushikamana katika uchaguzi mkuu ili kupata majimbo hayo licha ya kuwepo kwa changamoto ya kufanyiwa vurugu na Chadema. Bw. Nyambabe amehoji juu ya hatima ya NCCR-MAGEUZI baada ya uchaguzi na UKAWA wakiwa madarakani huku changamoto zikiwa bado hazijamalizika, akitolea mfano itakuwaje kwenye mgawanyo wa wakuu wa mikoa ,pamoja na wakuu wa Wilaya. 
 Amesema NCCR-Mageuzi imepoteza matumaini katika muungano huo ya kupata wabunge wengi, na kusisitiza kuwa chama hicho kitakuwa na wakati mgumu bila kutafuta ufumbuzi kukiwa bado mapema 
Mgawanyo wa majimbo ambao unaleta mkanganyiko katika UKAWA ni Chadema –Majimbo 148; CUF (Majimbo 99) ,NCCR-Mageuzi (Majimbo 12) na NLD - Majimbo matatu.

CHANZO: MICHUZI BLOG

No comments:

Post a Comment