Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, November 28, 2015

MAJIPU MATANO SUGU KWA RAIS DK. MAGUFULI,AKIWEZA KUYATUMBUA HAYA ATAKUWA AMEKATA KIU YA WATANZANIA

. Wasomi, wanasiasa na watu kutoka makundi mengine ya jamii wamesema Rais John Magufuli atapimwa katika miaka mitano ijayo kwa mambo makubwa matano yaliyoonekana kuwa ‘majipu sugu’ na changamoto kwa mtangulizi wake, Jakaya Kikwete.
Majipu (mambo matano) hayo ni kudhibiti mtandao wa wafanyabiashara wa dawa za kulevya, kukomesha rushwa na ufisadi, kufumua mtandao wa majangili, kuhakikisha Katiba Mpya inapatikana na kuua ‘mchwa’ unaoitafuna fedha za Serikali.
Maoni yaliyotolewa na wasomi, wanasiasa na wananchi wa kawaida yanaonyesha kwamba kufanikiwa kwake kutategemea aina ya ushirikiano atakaoupata kutoka kwa wananchi na wanasiasa na hasa wa kutoka chama chake.
Mhadhiri kutoka Idara ya Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Elijah Kondi alisema Dk Magufuli anahitaji kupigana vita kali kufanikisha ahadi zake na akaonya kuwa hawezi kusimama mwenyewe na kushinda vita hiyo bila kuungwa mkono na wananchi hasa chama chake, CCM.

 
“Vigogo wengi ndani ya chama chake wamekuwa wakihusishwa na majipu hayo. Hivyo, kufanikisha azma hiyo, kutategemea wingi wa wanaCCM watakaomuunga mkono, lakini kama watakuwa wachache, itakuwa vigumu. Hilo hata yeye (Magufuli) analifahamu ndiyo maana anasema vita hiyo ni kubwa,” alisema Kondi.
Pia, alisema kushughulikia mtandao wa dawa za kulevya, ujangili na kuanzisha mahakama ya mafisadi kutategemea ushirikiano atakaoupata kutoka kwa watendaji na baraza lake la mawaziri.
Kondi alisema kushindwa kwa Rais mstaafu Kikwete katika mambo hayo kulitokana na udhaifu wa baraza lake la mawaziri na watendaji wa taasisi za Serikali. “Rais anaweza kuwa na dhamira njema, lakini je, atapata mawaziri wazuri wa kumsaidia? Hao mawaziri watakuwa na ari gani ya kushiriki vita hiyo?” alihoji na kuongeza:
“Kwa sababu anaweza kuanzisha mahakama ya mafisadi lakini ikashindwa kuonyesha uhai kama anavyotarajia. Jaribio la kutumbua majipu hayo itategemea ushirikiano wa chama chake, mawaziri atakaowateua na watendaji wa Serikali.”
Mhadhiri wa Idara ya Sayansi ya Siasa, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Richard Mbunda alisema kilichosababisha marais waliomtangulia kushindwa kutumbua majipu hayo ni utofauti mkubwa ulioonekana kati yao.
“Utofauti katika uwezo wao ukoje? Dhamira zao zinatofautianaje? Lakini hata kiwango cha utashi wa kushughulikia hilo jipu kinatofautianaje na uongozi uliopita. Ukisikiliza kauli ya Rais Magufuli anaonyesha matumaini,” alisema Mbunda.
Meneja wa Soko la Machinga Complex, Nyamsukura Masondore alisema kupandishwa mahakamani kwa vigogo wa Serikali katika kashfa ya EPA ni sehemu ya juhudi zilizoonekana kwa uongozi uliopita. “Hivyo, hakuna kitakachoshindikana kwa Rais Magufuli endapo watendaji wa chini watakuwa tayari kubadilika na kutoa ushirikiano wa kushinda vita ya majipu hayo,” anasema
Profesa George Shumbusho wa Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema ana imani Rais Magufuli anaweza kushughulikia changamoto hizo sugu ambazo ameziita majipu kutokana na historia ya utendaji wake. “Rais Magufuli atafanikiwa kazi hiyo kutokana na historia yake ya kutojihusisha kwa karibu na mtandao wa wafanyabiashara wakubwa hapa nchini na nje,” alisema.
Profesa Shumbusho alisema kuwa endapo ataendelea na msimamo huo, changamoto ya ukwepaji kodi, misamaha ya kodi, biashara haramu ikiwamo ya dawa za kulevya zitakoma.
Dawa za kulevya
Aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alinukuliwa Agosti 2013 bungeni akikiri kuwapo baadhi ya majina ya wabunge miongoni mwa watu wanaoshukiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya lakini alisema Serikali haiwezi kuwataja hadharani kwa haraka.
Hata Kikwete wakati wa awamu yake ya kwanza, aliwahi kusema anawajua wauza dawa za kulevya lakini tatizo hilo limeendelea kuwa sugu hadi anamaliza kipindi chake cha pili.
Mwaka huohuo, Umoja wa Mataifa (UN) ulitoa ripoti inayobainisha Tanzania kuwa kinara wa kupitisha dawa za kulevya katika nchi za Afrika Mashariki. Kuanzia 2010 hadi 2013 ilipitisha tani 64 za dawa za kulevya aina ya heroine na ikitaja Bandari ya Tanga kuwa njia kuu ya upitishaji huo.
Je, baada ya kuanzishwa kwa Sheria ya Kupambana na Kuthibiti Dawa za Kulevya ya mwaka 2015, Rais Magufuli ataweza kusimamia mapambano dhidi ya vinara wa biashara hiyo?
Ujangili wa tembo
Kabla ya kuondoka madarakani, Rais Kikwete aliwahi kunukuliwa Februari 2014 na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC Swahili) akikiri kuwatambua majangili 40 wa meno ya tembo na kwamba kiongozi wao anaishi Arusha. Pia, alikiri kuwa vita dhidi ya ujangili ni tatizo sugu.
Vilevile, Mei 2014, ripoti iliyoitwa ‘Ivory’s Curse: The Militarization and Professionalization of Poaching in Africa’, ilieleza kuwa tangu mwaka 2000 wizara inayohusika na utalii ilikuwa imetawaliwa na kashfa za rushwa. Ripoti hiyo ilifafanua jinsi vikundi mbalimbali vya waasi barani Afrika vinavyoendesha shughuli za ujangili.
Katiba ya Jaji Warioba
Oktoba 2014, Bunge Maalumu la Katiba lilipitisha Katiba Inayopendekezwa kwa tofauti ya kura mbili tu zilizonusuru kukwamisha Katiba hiyo kwa upande wa Zanzibar. Mvutano kati ya CCM na upinzani wakati wa upitishaji wa Katiba hiyo ulitokana na tofauti za itikadi na sera kuhusu muundo wa Muungano.
Wajumbe wa CCM walipigania sera yao ya muungano wa Serikali mbili wakati wenzao wa wapinzani walipigania muundo uliopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya Jaji mstaafu, Joseph Warioba wa Serikali Tatu. Hadi sasa haijapigiwa kura ya maoni.
‘Mchwa’ Serikalini
Kila mwaka, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) amekuwa akikagua na kuibua ufisadi mkubwa katika Serikali Kuu, Idara za Serikali na mashirika ya umma. Ripoti iliyotolewa mwaka huu inaonyesha ukaguzi ulifanyika katika taasisi 176 za Serikali kuu, halmashauri 163 na mashirika ya umma 109. Kikwete amewahi kupangua baraza lake la mawaziri na kuwafukuza kazi watendaji lakini bado ufisadi umeendelea katika nyanja tofauti kama ulipaji mishahara hewa na ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo.
Mahakama ya mafisadi
Moja ya ahadi kubwa za Rais Magufuli wakati wa kampeni na Novemba 20 alipozindua Bunge la Kumi na Moja la Jamhuri ya Muungano ni kuanzisha Mahakama Maalumu ya kushughulikia mafisadi. Tayari mchakato umeanza lakini wachambuzi wanasema kinachotakiwa ni kuipa meno Taasisi ya Kudhibiti na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ili iweze kufanya kazi zake bila kuogopa mtu.

CHANZO MWANANCHI

No comments:

Post a Comment