Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, November 30, 2015

SHEKH ISSA PONDA AACHIWA HURU......

MAHAKAMA ya hakimu mkazi Morogoro imemuachia huru leo Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda aliyekuwa akituhumiwa kwa makosa ya uchochezi baada ya mahakama kutoridhishwa na ushahidi wa upande wa mashtaka na hivyo kuonekana hana hatia.

********
Historia ya kesi ya Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda.
Hati ya Mashitaka ya Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya Mashitaka matatu  lakini Julai 22 mwaka 2015, Hakimu Mkazi Mary Moyo  alitoa  uamuzi wa kumfutia shitaka la kwanza kwasababu lilishatolewa uamuzi na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, na hivyo mahakama hiyo ya Morogoro siku hiyo ilitoa uamuzi wa kumuona ana kesi ya kujibu  katika mashitaka mawili yaliyosalia ambalo ni kosa la pili na la tatu .
Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro  ilimfungia dhamana Sheikh Ponda baada ya kukubaliana na hati ya aliyekuwa  Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP), wakati huo Dk.Eliezer Feleshi ambaye kwasasa ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar Es Salaam liloomba Mahakama hiyo imfungie dhamana mshitakiwa huyo chini ya Kifungu cha 148(4) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya jinai ya Mwaka 2002.


Hatua hiyo ya kufunguliwa kesi katika Mkoa wa Morogoro ilikuja ikiwa ni muda mfupi baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, Agosti 19 Mwaka 2013 saa Tatu asubuhi,  kumfutia kesi ya jinai  Na.144/2013 katika maeneo mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano baada ya DPP kudai kuwa hana nia ya kuendelea kumshitaki katika kesi hiyo No.144/2013  kwa mujibu wa kifungu cha 91(1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002.

Hata hivyo baada ya hakimu Liwa kumwachilia huru,Ponda ambaye aliletwa mahakamani hapo saa 12 asubuhi na wanausalama wa polisi na magereza chini ya ulinzi mkali, alikamatwa tena na kupakizwa kwenye magari ya wanausalama hao ambapo baadhi ya wanausalama hao waliliambia gazeti hili kuwa wanampeleka Ponda mkoani Morogoro kwaajili ya kufunguliwa makosa matatu ya uchochezi, kufanya mkusanyiko haramu na kisha akarejeshwa gereza la Segerea Dar es Salaam , lakini baadae Uongozi wa Jeshi la Magereza uliamua kumuamisha Ponda kutoka Gereza la Segerea na kumuamishia Katika Gereza Moja Mkoani Morogoro.
Sheikh Ponda alifikishwa mahakamani hapo akiwa chini ya ulinzi mkali wa polisi, baada ya kuwasili kwa helikopta ya Jeshi la Polisi katika uwanja wa gofu mjini Morogoro.
Akisoma mashitaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa wa Morogoro, Richard Kabate, Mwanasheria Kiongozi  wa Serikali, Bernard Kongola, alidai  kuwa Agosti 10, mwaka 2013, katika eneo la Uwanja wa Ndege, Manispaa ya Morogoro, Ponda aliwaambia Waislamu wasikubali uundwaji wa kamati za ulinzi na usalama za misikiti, kwa madai kuwa zimeundwa na BAKWATA, ambao ni vibaraka wa CCM na serikali.
Alidai kuwa Sheikh Ponda ambaye anatetewa  na wakili wa kujitegemea Juma Nassor aliwaagiza waumini hao kuwa endapo watu hao watajitokeza kwao na kujitabulisha kwamba ni kamati za ulinzi na usalama za misikiti, wafunge milango na madirisha wawapige.
Ilielezwa kuwa kauli hiyo ni kinyume cha agizo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, iliyotolewa na Hakimu Victoria Nongwa Mei 9, mwaka 2010, ambayo ilimtaka Ponda ndani ya mwaka mzima kuhubiri amani na Kuwa Raia Mwema.
Katika shitaka la pili, Kongola alidai kuwa Agosti 10, mwaka huu, katika eneo la Uwanja wa Ndege, Morogoro, Ponda aliwaambia Waislamu kuwa serikali ilipeleka jeshi Mtwara kushughulikia suala la vurugu iliyotokana na gesi ili kuwaua, kuwabaka na kuwatesa wananchi, kwa sababu asilimia 90 ya wakazi hao ni Waislamu.
Kwamba, Ponda aliwaambia wafuasi wake kuwa serikali haikufanya hivyo kwa wananchi wa Loliondo walipokataa Mwarabu asipatiwe kipande cha ardhi ya uwindaji baada ya kudai ni mali yao, kwa sababu asilimia 90 ya wakazi wa huko ni Wakristu.
Shitaka la tatu ambalo linafafana na lile la pili, ambalo nalo linadaiwa kutendwa Agosti 10, mwaka huu, ambapo kauli ya Ponda inadaiwa kuumiza imani za watu wengine kinyume cha kifungu cha sheria namba 390 na kanuni ya adhabu namba 35 cha mwaka 2002.
Oktoba 18 mwaka 2012, Ponda na wenzie 49 walifikishwa Katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa Mara ya kwanza   wakikabiliwa na makosa matano, kosa la kwanza ni la kula njama, kujimilikisha mali, kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Chang'ombe  Markas,wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh. Milioni 59 na kosa la uchochezi ambapo katika kesi hiyo Jamhuri ilikuwa ikiwakilishwa na wakili Mwandamizi wa Serikali , Tumaini Kweka .Mahakama pia iliwafunga dhamana ya Ponda na mshitakiwa wa pili tangu 0ktoba 18 Mwaka 2012 hadi siku Kesi hiyo iliyotolewa hukumu Mei 9 Mwaka 2013.
Mei 9 mwaka 2013 Hakimu Mkazi Victoria  Nongwa akitoa hukumu yake katika kesi hiyo ya Ponda na wenzake alisema anawaachiria huru washitakiwa 49  kwasababu upande wa jamhuri  umeshindwa kuthibitisha kesi dhidi yao na kwamba anamtia hatiani Ponda kwa kosa moja tu  la kuingia kwa jinai na kwamba na anamuachiria huru katika makosa manne yaliyosalia kwasababu pia jamhuri ilishindwa kuthibitisha mashitaka hayo dhidi ya Ponda.
Sheikh Ponda alikataa rufaa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kupinga hukumu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Mei 9 mwaka 2013 ambapo alishinda rufaa yake.
Hata hivyo siku Chache baada ya Kufungwa Kifungo hicho cha nje Mei 9 mwaka 2013, Ponda alikwenda Mkoani Morogoro na kufanya mkutano ambao alidai wa Kutenda makosa ya jinai ambao alikamtwa  Agosti Mwaka 2013 na kuwekwa chini ya ulinzi na kufunguliwa Kesi Mahakama ya Kisutu Na.144/2013 ikafutwa na DPP na ndipo akafunguliwa kesi hiyo Mkoani Morogoro ambayo imetolewa hukumu Leo na kuachiwa huru.

CHANZO : OTHMANI MICHUZI

No comments:

Post a Comment