Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, November 3, 2015

WATU WAWILI WAFARIKI KUTOKANA NA MAFURIKO YA MVUA KUBWA MWANZA

Watu wawili wamefariki dunia kutokana na mafuriko ya mvua kubwa iliyonyesha kwa saa kadhaa jana jijini Mwanza, akiwamo mwanafunzi wa kidato cha nne aliyesombwa na maji wakati akiwahi kufanya mitihani ya mwisho lakini mwili wake haujapatikana mpaka sasa.



Mvua hiyo iliyoanza kunyesha saa 12 asubuhi, ilikatika saa 4:30 asubuhi na kusababisha baadhi ya barabara kuziba kutokana na maji kuporomoka kutoka milimani.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Charles Mkumbo, amethibitisha kutokea kwa vifo hivyo ingawa hadi wakati anatoa taarifa hizo, mwili mwanafunzi wa kidato cha nne wa shule ya sekondari Nyamanoro, ulikuwa haujapatikana.

“Mvua kubwa ilinyesha kwa masaa manne katika maeneo mbalimbali ya jiji iliyosababisha maporomoko kutoka milimani na kusababisha watu kukosa sehemu ya kupita hasa eneo la Kirumba ambako mwendesha bodaboda namba MC861 AHK aliyewapakiza wanafunzi wawili wa kidato cha nne, kusombwa na maji na dereva huyo kufariki lakini wanafunzi wakiokolewa,” alisema Mkumbo.



Kamanda Mkumbo amemtaja mwanafunzi wa shule ya sekondari Nyamanoro ambaye mwili wake haujapatikana ni, Zainabu Shabani (18) aliyekuwa na wenzake wawili waliokuwa wakivuka daraja llilopo maeneo ya Nyamanoro wilaya ya Ilemela.





“Wenzake walifanikiwa kuvuka daraja salama, lakini Zainabu hakumaliza safari yake na kusombwa na maji mpaka na sasa hajulikani kama amekufa ama yupo hai kutokana na mwili wake kutoonekana,” alisema.



Mkumbo aliwataka wananchi kuacha tabia ya kuvuka mitaro na maeneo yaliyojaa maji pindi wanapoona mvua kubwa inanyesha ili kuepuka vifo na mataizo yanayoweza kuepukika.

No comments:

Post a Comment