Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, February 23, 2016

FISI WALA WATU WAUA, KUJERUHI MKOANI TABORA


Kikosi cha Kuzuia Ujangili Kanda ya Magharibi kinamsaka fisi mmoja kati ya wawili waliowashambulia Samwel Gamalaya na kusababisha kifo chake na kumjeruhi Kusekwa Ngeleja wakati wakikata kuni katika pori lililopo Kitongoji cha Isukamahela Manispaa ya Tabora.

Fisi hao wawili walimshambulia kwa kumng’ata Gamalaya maeneo mbalimbali ya mwili na kusababisha kifo chake, huku wakimjeruhi Ngeleja mikono na miguu.

Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia Ujangili Kanda ya Magharibi, Charles Msilanga alisema jana (juzi) kuwa baada ya polisi kumpiga risasi fisi mmoja na kumuua, mwingine alikimbia.


Alisema wanaendelea kumsaka fisi huyo ili kuzuia madhara zaidi kwa wakazi wa kitongoji hicho.

“Fisi aliyekimbia anaweza kuleta madhara kwa watu na ndiyo maana tunamsaka kwa udi na uvumba,” alisema Msilanga.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Iddi Cheyo alisema Gamalaya alifariki dunia baada ya kukaa muda mrefu bila matibabu tangu aliposhambuliwa na fisi hao.

Baadhi ya wakazi wa kitongoji hicho, Sophia William na Juma Kapambala walisema tukio hilo limewastaajabisha kwani kwa miaka mingi wanafanya shughuli zao ndani ya msitu huo bila kushambuliwa na wanyama.

“Tunafanya shughuli zetu katika msitu huu kwa miaka mingi bila kuvamiwa, lakini hatujaona mnyama kuingia eneo hilo,” alisema Sophia.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment