Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Saturday, August 18, 2012

NI MTIBWA AU SIMBA BINGWA SUPER 8?


Mecky Mexime Kianga

Na Mahmoud Zubeiry
FAINALI ya michuano ya BankABC Sup8R inapigwa leo Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam, ikizikutanisha timu mbili zenye sura tofauti, Simba SC na Mtibwa Sugar ya Morogoro.
Sura mbili tofauti kwa sababu, wakati Mtibwa inatumia kikosi chake cha Ligi Kuu msimu ujao, Simba, inatumia timu yake ya vijana, maarufu kama Simba B.
Suleiman Abdallah Matola
Wakati kambi ya Simba B juzi ilipokea mchezaji mpya, kutoka wale waliocheza hatua ya makundi hadi Nusu Fainali, Ramadhan Singano ‘Messi’, Mtibwa nayo ilipata pia mchezaji mpya, Shaaban Mussa Nditi anayecheza nafasi ya kiungo pia.
Messi na Nditi walikuwa nchini na Botswana na timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars ambayo ilicheza na wenyeji juzi na kutoka sare ya 3-3.
Kama ilivyo kurejea kwa Messi ni faraja kwa kocha wa Simba B, Suleiman Abdallah Matola- pia kurejea kwa Nditi ni habari njema kwa kocha wa Mtibwa Sugar, Mecky Mexikme Silili Kianga.
Akiizungumzia fainali hiyo, Matola ambaye ni Nahodha wa zamani wa Simba SC, alisema kwamba Mtibwa ni timu nzuri aliiona vizuri wakati ikiifunga 5-1 Jamhuri ya Pemba, lakini bado kwa Simba B wataangukia pua.
“Itakuwa mechi ngumu hilo naamini kabisa, lakini nataka nikuambie, kama nilivyosema kabla ya kucheza na Azam, nasema tena kabla ya kucheza na Mtibwa Sugar, tutawafunga bila kuongezewa nguvu ya wachezaji wa timu A,”alisema Matola.
Kwa upande wake, Mexime ambaye ni Nahodha wa zamani wa Mtibwa na Taifa Stars alisema Simba B ni timu nzuri, lakini yeye ana uzoefu na wachezaji wa vijana, hivyo hana wasiwasi atawafunga na kupeleka Kombe hilo Manungu.
Simba ilitinga Fainali ya michuano ya BankABC Sup8R Jumatano, baada ya kuifunga Azam FC, mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, wakati Mtibwa Sugar, iliifunga Jamhuri ya Pemba mabao 5-1, uwanja huo huo.
Kanuni za mashindano haya ni kushirikisha timu zilizoshika nafasi tatu za juu katika Ligi Kuu za Bara na visiwani na mbili zilioongoza katika kupanda Ligi Kuu zote mbili, lakini kwa Bara, Yanga waliokuwa washindi wa tatu msimu uliopita, walijitokea na nafasi yao ikachukuliwa na Mtibwa Sugar ambayo ilishika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu.
Bingwa wa michuano hiyo mipya itakayokuwa ikifanyika kila mwaka, ataondoka na Sh. Milioni 40, mshindi wa pili Sh. Milioni 20, wa tatu Sh. Milioni 15 sawa na wa nne, wakati washiriki wengine wataondoka na Sh. Milioni 5 kila moja.
source http://bongostaz.blogspot.com

No comments:

Post a Comment