Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Wednesday, January 15, 2014

KAGAME: TUTAMSHUGHULIKIA YEYOTE ANAYEISALITI RWANDA

Rais Paul Kagame wa Rwanda ameonya kwamba yeyote atakayewasaliti Wanyarwanda na Serikali yake anastahili kuchukuliwa hatua kali na kwamba amejitolea maisha yake kuijenga na kuhakikisha Rwanda inakuwa salama dhidi ya wote wasio na mapenzi mema.Akizungumza katika ibada maalumu ya kuliombea taifa juzi, Kagame aliwataka Wanyarwanda wote kuungana katika kusimamia misingi sahihi na msimamo wao kama taifa, bila kujali tetesi zinazotoka katika mataifa ya nje kuhusu wale waliotangaza kuisaliti Serikali yake.
Japokuwa hakutaja moja kwa moja kuhusu tuhuma zinazoikabili Serikali yake kuhusiana na mauaji ya aliyewahi kuwa Mkuu wake wa Ujasusi aliyeuawa Januari mosi akiwa hotelini huko Afrika Kusini, Patrick Karegeya, alisema wale wote wanaoigeuka nchi yao na kuchagua kuua raia wasio na hatia kwa sababu zao binafsi wanastahili kushughulikiwa ipasavyo.
"Sitakuwa na huruma na watu ambao wanasahau namna Rwanda ilivyowatengeneza na kuwa hapo walipo na hatimaye wanaamua kuisaliti kwa kuua raia wa Rwanda wasio na hatia, wakiwemo kinamama na watoto," aliongeza.
Alisema Rwanda haina sababu ya kuhusishwa au kuwajibishwa kwa ajili ya wale walioamua kuchukua njia zaidi na kufanya mambo yao kwa nia ya kuharibu yale yaliyofanyika kwa ajili ya kuliimarisha taifa la Rwanda.
Aliwataka viongozi wa Rwanda kutokusumbuliwa kwa yanayowakuta 'maadui wa taifa' kwa kuwa Mungu aliwapa nguvu ya kujenga na pia kukilinda kile walichokijenga, hivyo wale wanaosahau kwamba wana dhamana kwa Wanyarwanda na kuamua kutenda mambo mabaya dhidi ya taifa lao ni hakika kwamba wamesahau kuwa hawataweza kuwa juu ya watu wao.
"Mliponiapisha kuwa kiongozi wenu mliniagiza kwamba wakati wote niilinde nchi hii, kwa maana ya kusimama kwa ajili ya watu wake.
Lakini kila mmoja miongoni mwenu ana wajibu, aidha kwa njia ya kuhubiri au kukanusha tuhuma zozote za uongo kuhusu Rwanda," alisema Kagame kama alivyokaririwa na gazeti la New Times la Rwanda.
Alisema watu wa mataifa ya nje ambao wamekuwa wakiinyooshea kidole Kigali wamekuwa wakifanya hivyo mara 1000 zaidi kwa ajili ya kulinda nchi zao.
Hakusita kukumbusha kwamba wapo baadhi ya watu ambao wamekuwa wakitishia wazi hadharani kutaka kuipindua Serikali na wamekuwa wakishiriki katika mikakati ya ulipuaji wa mabomu yaliyosababisha mauaji ya raia kwenye Mji wa Kigali.
Tutapambana
Mtandao wa Chimreports.com uliripoti kwamba Kagame alionekana 'mwenye hasira' aliposema: "Kwa wale waliotengenezwa na kuwa juu na Rwanda kisha kutugeuka kama taifa tutapambana nao. Yeyote anayeidharau Rwanda atashughulikiwa ipasavyo popote alipo."
Serikali ya Afrika Kusini
Msemaji wa Wiara ya Mambo ya Nje ya Afrika Kusini, Clayson Monyela alisema hajapata taarifa zozote kuhusu kauli hizo za Kagame na hata hivyo hawezi kusungumzia suala hilo kwa kuwa liko nje ua uhusiano wa kidiplomasia baina ya Rwanda na nchi yake.
Hiyo ni kwa sababu Kagame hakutaja nchi yoyote katika hotuba yake hiyo ya jumapili na Afrika Kusini haiwezi kuchukua hatua ya kujihisi kwamba labda ndiyo inayohusika.
"Tukio lililotokea Johannesburg liko chini ya uchunguzi wa polisi na wote tunasubiri matokeo ya uchunguzi huo. Hatuna sababu ya kuanza kumhisi mkuu yeyote wa nchi, hatuendeshi diplomasia yetu kwa mtindo huo," alisistiza.
Kejeli
Jumamosi iliyopita, Waziri wa Ulinzi wa Rwanda, Jenerali James Kabarebe alikaririwa na mtandao wa AFP akizungumzia yaliyomkuta Karegeya aliyeuawa huko Afrika Kusini akisema: Unapochagua kuishi kama mbwa, utakufa kama mbwa."
Alikaririwa akisema, "Msipoteze muda wenu kwenye ripoti kwamba fulani aliuawa kwa kutumia kamba katika gorofa ya saba kwenye nchi fulani. Unapochagua kuwa mbwa, utakufa kama mbwa, na wafanya usafi watasafisha na kutupa kwenye pipa la taka ili usiwachafue.
"Kimsingi hayo ni mambo yanayowapata waliochagua kupitia njia hiyo. Hatuna la kufanya juu yao, na hatuwezi kulaumiwa kwa ajili ya yanayowakuta," alisema.
Mauaji ya Karegeya
Mwili wa Patrick Karegeya aliyekuwa mshirika wa Rais Kagame kisha kutofautiana na kukimbilia uhamishoni nchini Afrika Kusini ulikutwa ukiwa kwenye chumba cha hoteli mjini Johannesburg huku kukiwa na kitambaa chenye damu na kamba kando yake.
Baada ya polisi kueleza kwamba Karegeya aliuawa kwa kunyongwa, wasaidizi wake waliituhumu Serikali ya Rwanda kwa kuhusika na mauaji hayo.
Karegeya alikuwa mkuu wa usalama wa taifa akihusika na usalama wa nje wa Serikali ya Rais Kagame. Mwaka 2004 alishushwa cheo kisha kukamatwa na kuswekwa jela kwa miezi 18 kwa madai ya kwenda kinyume na mkuu wake wa kazi. Alikimbia nchini Rwanda mwaka 2007.
Pamoja na wapinzani wa Kagame kumtuhumu moja kwa moja kuhusika na mauaji hayo, Serikali yake haikuwahi kukubali au kukanisha moja kwa moja, lakini kwa kauli yake alisema juzi kwamba 'Hahitaji kuomba ruhusua kwa yeyote anaposimamia ulinzi wa taifa lake."

No comments:

Post a Comment