Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, February 11, 2014

Wafuasi wanne wa Chadema waondolewa shitaka la mauaji

 
 
Mahakama  Kuu Kanda ya Dodoma, imewaachia huru wafuasi wanne kati ya tisa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya kuua bila kukusudia baada ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini (DPP) kutokuwa na nia ya kuendelea na kesi hiyo.
Waliofutiwa mashitaka hayo mbele ya Jaji Mfawidhi, Crecensia Makuru, ni Francis Stanley, Philipo Edward, Titho Mintwa na Paulo Nashokigwa.

Ilielezwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Karen Mrango, kuwa washtakiwa hao wamefutiwa mashitaka yao kutokana na agizo la DPP.

Kufuatia hatua hiyo, Wakili Mrango alisema sasa watabaki washitakiwa watano ambao ni Manase Daud, William Elia, Charles Leonard, Emmanuel Shila na Josia Lyanga.
Wanashtakiwa kwa kosa la mauaji ya kada na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) kata ya Ndago, Yohana Mpinga, Julai 14, mwaka 2012.
TUNAOMBA BOFYA HAPA NA ULIKE PAGE YETU KWA HABARI NYINGI MOTOMOTO(USIPITWEEEE) 
Akiwasomea shitaka lao, Wakili Mrango alidai kuwa siku hiyo, saa 10:00 jioni, washtakiwa kwa pamoja wakisikiliza mkutano wa Chadema uliofanyika eneo la Kanisa la KKKT kijiji cha Nguvumali kata ya Ndago wilayani Iramba, walimuua kada huyo baada ya kutokea vurugu kubwa mkutanoni.

Wakili Mrango alidai kuwa chanzo cha vurugu hizo ni maneno ya kashfa yaliyotolewa jukwaani na viongozi wa Chadema akiwamo Mwita Waitara na Kitilah Mkumbo, dhidi ya Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba, kwamba ni mzinzi, mhuni na ana uhusiano wa kimapenzi na wanawake nje ya ndoa yake.

Alidai kuwa kufuatia maneno hayo, baadhi ya wana-CCM waliokuwa mkutanoni walichukia kuzuka vurugu kubwa kati yao na wale wa Chadema  na hivyo kusababisha kifo cha kada huyo wa CCM aliyekimbilia kwenye nyumba ya jirani ya Chume Manase, kwa lengo la kuokoa maisha yake.

Mwili wa marehemu ulipimwa na kuthibitika kuwa kifo chake kilitokana na jeraha kubwa kichwani.

Katika kesi hiyo, mahakama ilikabidhiwa taarifa ya daktari kama kielelezo huku ramani ya eneo la tukio ikipingwa na wakili wa walalamikaji, Deus Nyabiri, kwa madai kuwa zipo ramani mbili, ombi ambalo Jaji Makuru alikubaliana nalo.

Washtakiwa wote walikana kosa hilo na upande wa mashitaka uliahidi kupeleka mashahidi 17.

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Msajili wa Mahakama Kuu takapopanga tena.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment