Meneja
Miradi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bw. Alexander Ndibalema (Kulia
aliyesimama) akizungumza katika kikao cha pamoja kati ya Timu ya Ukaguzi
wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango,
wawakilishi wa wanavijiji vya Mradi wa Bandari Mpya ya Mbegani na Timu
ya Uthamini wa Ardhi wa eneo la mradi. Waliokaa viti vya mbele ni
viongozi wa Timu ya ukaguzi, Bibi Florence Mwanri (Wapili Kulia) na
Prof. Longinus Rutasitara (Watatu Kulia). Kushoto ni Mratibu wa ziara
hiyo, Bibi Salome Kingdom.
Mmoja
wa viongozi wa Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya
Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Kulia) akizungumza katika
mkutano huo.
Mthamini Mkuu wa Ardhi ya Mradi huo, Mhandisi Emmanuel Mrema (Kulia) akizungumza katika mkutano huo.
Mwenyekiti
wa Kijiji cha Pande, Bw. Ubezi Kondo (Kulia aliyesimama) akizungumza
wakati Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya Rais, Tume ya
Mipango ilipopita kijijini hapo kujua hali ya zoezi la tathmini ya
ardhi kwa ajili ya mradi wa Bandari Mpya ya Mbegani. Kulia kwake ni
Mmoja wa viongozi wa Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya
Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri na Mthamini Mkuu wa Ardhi
ya Mradi huo, Mhandisi Emmanuel Mrema.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Pande, Bw. Ubezi Kondo (Kushoto) akionesha eneo itakapokuwepo Bandari Mpya ya Mbegani. Wanaotazama ni Meneja Miradi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bw. Alexander Ndibalema (Kulia), Mthamini
Mkuu wa Ardhi ya Mradi huo, Mhandisi Emmanuel Mrema (Wapili Kulia) na
Mmoja wa viongozi wa Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya
Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Watatu Kulia).
Meneja Miradi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bw. Alexander Ndibalema (Kulia) akitoa maelezo juu ya maendeleo ya Mradi wa Bandari
Mpya ya Mbegani katika eneo itakapokuwepo bandari hiyo.
Wanaomsilikiliza ni Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya
Rais, Tume ya Mipango.
Picha na Saidi Mkabakuli
Na Saidi Mkabakuli
Ndoto ya
kuwa na Bandari mpya ya Mbegani kufikia mwaka 2017 na kutekeleza Mpango
wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2011/12 - 2015/16) imekamilika
kwa takribani asilimia 90 kufuatia kukamilika kwa tathmini ya ardhi ya
eneo zima la mradi huo.
Hayo yamedhihirishwa na Mthamini Mkuu wa
Ardhi ya Mradi huo, Mhandisi Emmanuel Mrema wakati akizungumza wakati wa
mkutano wa pamoja na Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka
Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango ilipofanya ziara ya ukaguzi wa maendeleo
ya mradi huo.
Mhandisi Mrema alisema kuwa mpaka
sasa jumla ya kaya 1100 kutoka vitongoji vya Bisibisi, Mji Mpya,
Mlingotini na Pande vimeshafanyiwa tathmini, ambapo makadirio ya awali
yanaonesha jumla ya shilingi bilioni 23 zinatarajiwa kulipwa kupisha
mradi.
“Mpaka sasa takribani asilimia 90 ya
eneo la mradi ambalo ni sawa na hekta 2000 limeshakamilika, ambapo kwa
mujibu wa mapendekezo ya tathmini tunatarajia malipo kufanyika kufikia
mwezi Juni mwaka huu,” alisema Mhandisi Mrema.
Akizungumza katika mkutano huo, mmoja
wa viongozi wa Timu Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Ofisi ya
Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri alisema kuwa kuna haja ya
kuhakikisha fidia kwa wanavijiji hao inalipwa kwa wakati ili kuondoa
usumbufu wa kusubiri malipo ya kwa muda mrefu hali itakayochochea
kuchelewa kwa utekelezaji wa mradi.
“Nawaomba muhakikishe malipo
yanafanywa kwa wakati ili kuwaondoshea usumbufu wananchi ili kulinda
heshima ya Serikali na kuondosha kero ya kusubiri ya kusubiri kwa muda
mrefu,” alisema Bibi Mwanri ambaye ni Naibu Katibu Mtendaji
anayeshughulikia Huduma za Jamii na Maendeleo ya Idadi ya Watu.
Akijibu hoja ya ushirikishwaji wakati
wa zoezi hilo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Pande, Bw. Ubezi Kondo alisema
kuwa kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakishirikishwa katika kila hatua ya
uthamini huo. Aliongeza kuwa hali hii imewaongezea hamasa ya kuupisha
mradi huo ili kutimiza ndoto ya Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete ya
kujenga Bandari hiyo pamoja na ahadi aliyoitoa Mwalimu Julius Nyerere
mwaka 1968.
“Kwa hakika tunaukubali mradi huu kwa
mikono miwili ili kutimiza ndoto na ahadi za Rais Kikwete na ya Mwalimu
Nyerere aliyoitoa mwaka 1968 wakati akifungua Chuo cha Mbegani ambapo
aliahidi kuwa atahakikisha kunajengwa Bandari ya kisasa Mbegani,”
alisema Bw. Kondo.
Kwa mujibu wa Naibu Katibu Mtendaji
(Uchumi Jumla), Prof. Longinus Rutasitara ambaye ni kiongozi mwenza wa
ukaguzi huo, uwekezaji katika Bandari mpya ya Mbegani unatoa fursa za
kimkakati katika kufikia malengo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa
Miaka Mitano (2011/12 - 2015/16).
“Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa
Miaka Mitano (2011/12 - 2015/16) unaweka bayana kuwa uwekezaji wa
Bandari ni mojawapo ya maeneo ya kipaumbele na kimkakati ambapo
kukamilika kwa ujenzi wa bandari mpya ya Mbegani Bagamoyo kunatarajiwa
kupunguza msongamano wa meli katika bandari ya Dar es Salaam,” alisema
Prof. Rutasitara.
Serikali imeaandaa Mpango wa
Maendeleo wa Miaka Mitano ukiwa na lengo la kuwa na mfumo madhubuti wa
kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025. Lengo la Dira ni kuibadili
Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
No comments:
Post a Comment