Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Tuesday, December 30, 2014

BASTOLA TISHIO DAR ZALETA MAAFA NA KUJERUHI,RIPOTI HII HAPA








Madaraka.
Stori:Waandishi wetu IKIWA  imebakia siku moja kabla ya mwaka 2014 kumalizika, jiji la Dar es Salaam limejikuta likigubikwa na mauaji ya mara kwa mara, hasa ya kutumia silaha baada ya kubainika kuzagaa kwa bastola zilizo mikononi mwa watu waovu.
Silaha hizo sasa zimekuwa kama simu za mikononi ambazo karibu kila mtu jijini Dar es Salaam anayo na hivyo kuwapa hofu kubwa wananchi  ambao hawajui lini na wapi litatokea tukio la ujambazi, hasa kutokana na msongamano mkubwa wa watu.
Matukio mengi ya ujambazi yanayofanyika nyakati za mchana kweupe, yanafanywa na majambazi ambao wanatajwa kutumia pikipiki hasa aina ya Boxer, zinazoaminika kuwa na kasi kuliko aina nyingine na usafiri ambao hauwezi kukwama kwenye foleni.
Baadhi ya matukio yanayomaliza mwaka na kuzidisha hofu kwa watu ni kama lile lililotokea Tabata Kisukuru, mwishoni mwa wiki iliyopita, ambapo kijana aliyetajwa kwa jina la Mahamud Ally (19) kuuawa kwa kupigwa risasi na mtu mmoja anayedaiwa kukerwa na kelele za majirani kwenye sherehe za send off.
Ilidaiwa kwamba mtu huyo hakupendezwa na kelele hizo na mara kadhaa alitoka nje na kuwaamuru watu kukaa mbali na nyumba yake, lakini hawakutaka kusikia. Alipoona watu wanakaidi, anadaiwa kwenda kuchukua bastola yake na kuanza kupiga risasi ovyo hewani, ambayo mojawapo ilienda kumkuta marehemu, ambaye alikuwa ni mpita njia.

Ochola.
“Nakumbuka siku ya tukio majira ya saa tano na nusu usiku nikiwa na wenzangu kwenye sherehe, tukijitayarisha kukusanya vifaa vya muziki ili tufunge, ndipo jirani yetu alitoka nyumbani kwake na kuanza kufyatua risasi ovyo, ya kwanza ilimpata Mahamud kichwani na nyingine bega la kushoto akawa 



amedondoka chini, risasi zilizidi kumiminwa na moja ikanipata shavuni,” alisema mmoja wa majeruhi, aliyejitambulisha kwa jina la Goodluck.
Kaka wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Salim Ally alisema mdogo wake alikuwa na miezi miwili tu tokea aje Dar kwa ajili ya kufanya kazi za ujenzi akitokea kwao Morogoro na siku ya tukio, alikuwa ametoka kuachana naye kumsindikiza kwenda kulala.
Katika tukio lingine, huko Tabata Mawenzi, mtu mmoja aitwaye Richard Shukuru Mwaikimba (26) naye alipigwa risasi na kufa baada ya kujaribu kumsaidia mfanyabiashara mmoja wakala wa mitandao ya fedha ya simu za mikononi, aliyevamiwa na majambazi hao wapatao watatu.
Ilidaiwa kuwa Richard na wenzake walishuku kuwepo kwa uporaji dukani kwa Tatu, hivyo wakajikusanya ili kwenda kusaidia, lakini walipokaribia, jambazi mmoja alichomoa bastola na kumpiga marehemu kabla ya wote watatu kupanda pikipiki moja na kutokomea kusikojulikana baada ya kupora fedha.
Gloria.
Marehemu ambaye alikuwa mwenyeji wa Bukoba, na aliyetarajiwa kuzikwa Dar wiki hii, aliwahishwa hospitalini Amana kwa ajili ya kupatiwa matibabu, lakini alifariki muda mfupi baada ya kufikishwa.
Katika tukio lingine, majambazi waliokuwa na bastola, walivamia na kupora mamilioni ya fedha katika baa ya Mawela iliyopo Sinza baada ya kuwalazimisha watu kutoa fedha na simu walizokuwa nazo wakati wakinywa huku wakitazama mpira.
Mlinzi wa baa hiyo, Peter Otieno Ochola, akiamini amejificha, alijaribu kupiga simu Polisi ili kuomba msaada, lakini majambazi hao walimuona na kumpiga risasi ya kichwani iliyosababisha mauti yake.
Meneja wa baa hiyo, Steven Richad alisema kwamba majambazi hao walifika katika eneo hilo wakiwa na pikipiki nne na kufyatua risasi wakiwataka walale chini na kila mmoja atoe simu na fedha alizokuwa nazo.
“Siku hiyo watu walijaa sana kwa vile kulikuwa na mpira, walichukua vile walivyovitaka na hata huku kaunta waliingia na kupora zaidi ya shilingi milioni tatu, deki na lap top,” alisema.


Shukulu.
Kana kwamba haitoshi, amani na utulivu umeendelea kuwa tete jijini Dar es Salaam, baada ya dada mmoja aliyefahamika kwa jina la Gloria Uroki,  naye kuuawa kwa kupigwa risasi kichwani mchana wa Jumatatu iliyopita, baada ya majambazi hao kumshuku kuwa alikuwa akiwasiliana na polisi kuhusu tukio lao.
Tukio hilo lilitokea Kinondoni Morocco baada ya majambazi hao waliokuwa wanne, kumfuatilia mwanamke mmoja aliyekuwa amepanda daladala kutoka kusikojulikana. Mara baada ya kushuka, kijana mwingine naye alishuka kutoka katika gari hilo na kumtaka kumkabidhi mkoba huo, alipokataa alitolewa bastola na hivyo kumkabidhi.
Lakini baada ya kuporwa mkoba huo, mwanamke huyo alianza kupiga mayowe yaliyosababisha majambazi hao waliokuwa na pikipiki mbili kuanza kukimbia. Akiwa hajui hili wala lile, Gloria alikatisha barabara akizungumza kwa simu yake ya mkononi.
Wakiwa wametaharuki, majambazi hao walipomuona na simu sikioni, waliamini alikuwa akiwasiliana na polisi hivyo kumfyatulia risasi zilizosababisha kifo chake, miezi mitatu tu baada ya kufunga ndoa.
Wananchi mbalimbali waliozungumza na gazeti hili wameilaumu serikali kwa kushindwa kudhibiti ongezeko kubwa la silaha aina ya bastola, kwani hivi sasa ni nyingi mithili ya simu za mikononi.

“Tunajua baadhi ya silaha hizi siyo halali kwa maana wamiliki wamejipatia kwa njia za panya, lakini ni jukumu la serikali kuhakikisha kunakuwepo na udhibiti. Ongezeko hili la silaha liangaliwe, hasa sehemu za mipakani na kwenye kambi za wakimbizi,” alisema Zabanga Komu wa Mwenge, jijini Dar es Salaam.CHANZO GPL

No comments:

Post a Comment