Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Monday, February 8, 2016

JAJI DAMIAN LUBUVA AMTAKA ' LOWASSA' AACHE KUUPOTOSHA UMMA



Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva amewataka wanasiasa walioshindwa kwenye Uchaguzi Mkuu waache kujitangaza kuwa walishinda, akisema wanapotosha wananchi.

Kauli hiyo ya Jaji Lubuva imekuja siku chache baada ya aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa kudai kuwa kama si matokeo kuchakachuliwa, alikuwa na nafasi kubwa ya kushinda kwa sababu wananchi walishaichoka CCM na wakawa wanataka mabadiliko.



Lowassa alisema hayo katika mahojiano maalum na waandishi wa habari ofisini kwake, akisema yeye na Ukawa walishinda kwa kishindo isipokuwa matokeo yalivurugwa makusudi ili CCM iendelee kubaki madarakani.

Jana, akiwa kwenye mkutano wa tathmini kati ya NEC na asasi za kiraia kuhusu utoaji elimu kwa mpigakura uliofanyika Dodoma, Jaji Lubuva alisema uchaguzi umeshapita na kilichobaki sasa ni kufanya kazi tu.

Bila ya kutaja jina la mwanasiasa huyo, Jaji Lubuva alisema kama kuna mtu alishindwa katika uchaguzi uliopita, ajipange kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao mwaka 2020.


“Hata wananchi wanawashangaa kwa kuwa wao ndio walioamua ni nani anafaa kuwaongoza,” alisema Jaji Lubuva.


Alisema kuwa NEC ilikuwa inapokea matokeo ya uchaguzi kutoka majimboni na kuyasoma kama yalivyotumwa na katika hilo hakuna wakala hata mmoja wa chama ambaye aliyapinga matokeo hayo.

“Sasa nashangaa kuna baadhi ya wagombea wanaotaka Tume ifukuzwe kazi eti tu kwa sababu wao hawakushinda. Naomba ifahamike kwamba katika kila uchaguzi duniani kuna kushinda na kushindwa.


"Sasa kama kila atakayeshindwa atataka tume ifukuzwe kazi hapatakuwa na tume ya uchaguzi kwa sababu kila atakayekuwa anashindwa atakuwa anataka tume ifukuzwe kazi,” alisema Jaji Lubuva.


Chadema, ambayo iliungana na vyama vitatu kuunda Ukawa, iliitaka NEC kusitisha utangazaji matokeo ikidai kuwa kilichokuwa kikitangazwa ni tofauti na takwimu walizokusanya kutoka majimboni. Lakini NEC ikaendelea kutangaza.

Baadaye, Chadema ililalamika ikidai kituo chao cha kukusanya na kujumlisha matokeo kilivamiwa na polisi na kompyuta kuchukuliwa na hivyo kuvuruga ufuatiliaji wao wa matokeo.

Kwa upande wake mkurugenzi wa huduma kutoka NEC, Emmanuel Kavishe alisema kuwa Tume inafanya kazi kwa mujibu wa sheria na Katiba na kwamba hata siku moja haijawahi kumpendelea au kumuonea mtu yeyote.


Katika uchaguzi wa urais, John Magufuli alipata kura milioni 8.8 huku Lowassa akipata milioni 6.07.

No comments:

Post a Comment