Social Icons

IMETOSHA

IMETOSHA

Sunday, January 5, 2014

Eto’o anahitajika nyumbani kwa Obama

Eto2527oclip1 77483
KEVIN McBride alikuwa bondia wa mwisho kupigana na Mike Tyson katika zama zake za ngumi. Alishinda kirahisi. Kumpiga Tyson halisi ilikuwa ni sawa na kukipiga kifo. Lakini McBride hana chochote cha kujisifia. Alimkuta Tyson amechoka!

Usiku wa Juni 11, 2005 alirusha makonde mawili matatu akiwa na umbo lake tipwatipwa. Yalimpata Tyson, lakini hayakuwa na madhara sana. hata hivyo katika raundi ya saba, ghafla Tyson alitupa taulo lake ulingoni na kuondoka zake ukumbini.


TUNAOMBA BOFYA HAPA NA ULIKE PAGE YETU KWA HABARI NYINGI ZA KILA SIKU,(USIPITWEEEEEEEE)

Alipoulizwa na waandishi wa habari alidai kwamba amepoteza hamu ya kupigana. Hana makali tena. Kwa mbali machozi yalikuwa yanamlengalenga. Yuko wapi yule jamaa aliyeandika kitabu kilichoitwa 'Mwisho wa Shujaa'? huu ulikuwa mwisho wa shujaa mwingine ambaye uso wa dunia umewahi kumuona. Ulimuona Samuel Eto'o alivyoshangilia bao lake dhidi ya Liverpool? Lilikuwa bao zuri kiasi. Lilibeba umuhimu mwingi. Lakini lilikuwa bao muhimu kwa Eto'o kuliko hata kwa timu yake Chelsea.
Eto'o ni zaidi ya kila mshambuliaji wa Chelsea. Ukifungua vitabu vya historia, anaweza kuwa juu ya Demba Ba na Fernando Torres na ana kila kitu maishani. Achilia mbali mkewe mrembo, Georgette, Eto'o ana karibu kila kitu maishani ambacho kinakonga
moyo wake.

Anaendesha Bugatti Veryon, gari la kifahari duniani. Ana takataka zote za kifahari maishani. Majuzi amenunua ndege ndogo. Amekusanya mali hizi kwa jasho lake tangu usiku ule alipotua Ulaya akiwa na umri wa miaka 14 na klabu ya Real Madrid ikamgandisha Uwanja wa Ndege kwa saa zaidi ya sita asitokee mtu wa kumpokea.
Shangilia yake ya bao dhidi ya Liverpool ilikuwa na maana moja tu. Eto'o alikuwa anajaribu kutua mzigo mzito alioubeba tangu aende Stamford Bridge. Ana deni ambalo anajua hawezi kulilipa akiwa na umri wake wa miaka 33.
Alisajiliwa afunge mabao. Lakini mpaka siku ile wakati anaifunga Liverpool, washambuliaji watatu wa Chelsea; yeye, Ba na Torres walikuwa wamefunga mabao manne tu ya Ligi. Wanazidiwa na viungo wao, wanazidiwa na mabeki wao. Aibu iliyoje!
Kabla ya mechi ya Liverpool alikuwa amecheza mechi tano mfululizo bila ya kufunga. Unamkumbuka Eto'o yule? Angewezaje kucheza mechi tano mfululizo bila ya kufunga?
Kwa ujumla, bao lake la Liverpool lilikuwa la tano kwa msimu mzima. Ina maana tangu Agosti mpaka Desemba Eto'o unayemfahamu alikuwa amefunga mabao manne tu kwa ujumla katika michuano yote?
Kwa Eto'o ni aibu zaidi. Unamkumbuka vizuri? Yule Eto'o aliyekuwa na mwendo wa umeme, jicho la kipanga na anauma kama chatu. Haiwezekani timu anayochezea iwe na ukame wa mabao kiasi
hiki. Chelsea imempa mkataba wa mwaka mmoja tu. Lakini sioni kama anaweza kupewa mkataba mwingine. Anachoweza kufanya ni kitu rahisi. Ni kama vile Mike Tyson alivyofanya kwa Kevin McBride. Kutupa taulo. Wakati Tyson aliondoka ukumbini, Eto'o asiondoke ukumbini moja kwa moja. Anapaswa kwenda Marekani au Qatar.

Maisha yanataka nini zaidi? Ndicho kitakachotokea. Jina la Eto'o Marekani au Qatar ni kubwa zaidi ya jina la Robert Mugabe ndani ya London. Anachoweza kufanya kwa sasa ni kuhamia Los Angeles na kukipiga LA Galaxy huku akiishi mtaa mmoja na Tom Cruise mitaa ya Beverley Hills. Katika nchi ya Barrack Obama.
Ndicho walichofanya Raul Gonzalez, Gabriel Batistuta, David Beckham, Thierry Henry na wengineo katika nyakati mbalimbali. Unachota kiasi kikubwa cha pesa, unapokelewa na vyombo vya habari na rundo la mashabiki ambao hawafahamu sana kuhusu soka halisi.
Baada ya hapo unapewa Lamborghini la kutembelea na unaishi mtaa mmoja na Tiger Woods au Kobe Bryant. Kuanzia hapo unakuwa Mungu mtu wa mashabiki. Baada ya likizo aliyoichukua katika soka na kwenda Anzhi Makhachkala akichota pesa za tajiri Suleyman Kerimov, nadhani Ligi Kuu England haikuwa mwafaka kwa Eto'o. Angeweza kuja wakati ule akiwa na Barcelona ya Ronaldinho na Deco, lakini kwa sasa amepoteza nguvu na wepesi.
Kusikia kwamba Chelsea iko sokoni ikitafuta mshambuliaji wa kiwango cha juu kwa ajili ya kuisaidia kupachika mabao, ni tusi la mwisho kwa Eto'o. Labda ni wakati wa kutupa taulo kama Tyson alivyofanya kwa McBridge.
Ndoto nzuri inaishia pale inaposisimua. Haipaswi kuishia pale unapoota uko ndani ya jeneza ukifukiwa. Unapaswa kuota unambusu Mariah Carey au Toni Braxton. Kama ni simulizi inapaswa pia kuishia patamu.
Eto'o anaweza kutuacha patamu zaidi akiondoka msimu huu, akisaini mkataba mpya na Chelsea ataondoka akiwa na ndoto mbaya kidogo. Huu ni muda wake wa kwenda Marekani ili tumsahau huku tukikumbuka kuwa alikuwa hatari.
Mwigizaji maarufu wa zamani wa Marekani, Orson Welles, aliwahi kusema 'Kama unataka uwe na mwisho mzuri, basi itatagemea na wapi unamalizia stori yako', inawezekana alikuwa sahihi. Chanzo: Mwananspoti

No comments:

Post a Comment