Kamanda wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa
Mkazi wa Buguruni, Dar es Salaam (Jina linahifadhiwa) amedaiwa
kukamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)
akiwa na kete 61 za dawa za kulevya aina ya Cocaine.
Akizungumza jana, Kamanda wa Kitengo cha Kupambana
na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa alisema mtuhumiwa aliwasili JNIA
akitokea Brazil akipitia Ethiopia akiwa amepanda ndege ya Shirika la
Ethiopia.
Alisema Machi 17, mwaka huu saa 8:25 usiku,
mtuhumiwa akiwa na hati ya kusafiria AB362172 ya Tanzania, alishukiwa na
polisi kuwa amemeza dawa za kulevya.
Alisema baada ya kumtilia shaka walimhoji na
kubaini kuwa amemeza dawa hizo ambapo alizitoa kwa awamu mbili ya kwanza
akitoa kete 31 na baadaye 30.
“Aliposhuka kwenye uwanja wa ndege tulikuwa na
wasiwasi naye na tulimchukua na kumhoji kwa zaidi ya saa moja baadaye
alikubali kuwa amekula kete hizo ambazo alizitoa kwa njia ya haja
kubwa,” alisema na kuongeza:
“Ninavyoongea na wewe mtuhumiwa bado anahojiwa na anaendelea kuzitoa dawa hizo,” alisema Kamanda Nzowa.
Kamanda Nzowa alisema upelelezi ukikamilika kesi
yake itasikilizwa kwenye Mahakama Kuu kutokana thamani ya dawa aina ya
cocaine kuwa kubwa.
“Kete moja ina gramu 17, gramu moja inauzwa
Sh60,000 ambapo ipo tofauti na dawa aina ya heroine ambayo thamani yake
ipo chini,” alisema Kamanda Nzowa.
Chanzo;Mwananchi
No comments:
Post a Comment